Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ukweli Kumhusu Mungu na Kristo

Ukweli Kumhusu Mungu na Kristo

Ingawa wanadamu huabudu miungu mingi, kuna Mungu mmoja tu wa kweli. (Yohana 17:3) Yeye ndiye “Mkuu Zaidi,” Muumba wa vitu vyote na ndiye Chanzo cha uhai. Yeye pekee ndiye anayestahili ibada yetu.—Danieli 7:18; Ufunuo 4:11

Mungu Ni Nani?

Jina la Mungu linapatikana katika nakala za kale MARA 7,000 HIVI

YEHOVA Ni jina la Mungu

BWANA, MUNGU, BABA Ni baadhi ya majina ya cheo ya Yehova

Mungu Anaitwa Nani? Mungu mwenyewe anasema: “Mimi ni Yehova. Hilo ndilo jina langu.” (Isaya 42:8) Jina la Mungu linapatikana mara 7,000 hivi katika Biblia. Hata hivyo, tafsiri nyingi za Biblia zimeondoa jina hilo na badala yake zinatumia majina ya cheo kama vile “Bwana.” Mungu anataka uwe rafiki yake, hivyo anakutia moyo ‘uliitie jina lake.’—Zaburi 105:1.

Majina ya Cheo ya Yehova. Biblia humrejelea Yehova kwa kutumia majina ya cheo kama vile “Mungu,” “Mweza-Yote,” “Muumba,” “Baba,” “Bwana,” na “Mwenye Enzi Kuu.” Watumishi wengi wa Mungu waliposali kwa Yehova walitumia jina lake binafsi au majina ya cheo, na sala hizo zimeandikwa katika Biblia.—Danieli 9:4.

Jinsi Mungu Alivyo. Mungu ana mwili wa roho usioweza kuonekana. (Yohana 4:24) Biblia inathibitisha kwamba “hakuna mwanadamu ambaye amemwona Mungu.” (Yohana 1:18) Hata hivyo, Biblia hufunua hisia za Mungu. Watu wanaweza kumhuzunisha au ‘kumfurahisha.’—Methali 11:20; Zaburi 78:40, 41.

Sifa za Pekee za Mungu. Mungu hana ubaguzi. Anawakubali watu kutoka mataifa yote na malezi mbalimbali. (Matendo 10:34, 35) Pia, yeye ni ‘mwenye rehema na huruma, si mwepesi wa hasira, naye ana upendo mwingi mshikamanifu na kweli.’ (Kutoka 34:6, 7) Hata hivyo, Mungu ana sifa kuu nne zenye kutokeza zaidi.

Nguvu. Kwa kuwa yeye ni “Mungu Mweza-Yote,” ana nguvu zisizo na mipaka za kutimiza jambo lolote analoahidi.—Mwanzo 17:1.

Hekima. Hekima ya Mungu haiwezi kulinganishwa na ya mtu yeyote. Hiyo ndiyo sababu Biblia husema kwamba yeye “peke yake ndiye mwenye hekima.”—Waroma 16:27.

Haki. Sikuzote Mungu hutenda yaliyo sawa. Matendo yake ni ‘makamilifu,’ na “kamwe hana ukosefu wa haki.”—Kumbukumbu la Torati 32:4.

Upendo. Biblia inasema kwamba “Mungu ni upendo.” (1 Yohana 4:8) Mungu haonyeshi tu upendo, bali upendo ndio utu wake. Upendo wake wa hali ya juu huongoza kila jambo analofanya, nao hutunufaisha katika njia nyingi.

Urafiki wa Mungu na Wanadamu. Mungu ni Baba yetu wa mbinguni mwenye upendo. (Mathayo 6:9) Tukiwa na imani kwake tutakuwa marafiki wake. (Zaburi 25:14) Kwa kweli, Mungu anakualika umkaribie katika sala na ‘kumtupia mahangaiko yako yote, kwa sababu yeye anakujali.’—1 Petro 5:7; Yakobo 4:8.

Kuna Tofauti Gani Kati ya Mungu na Kristo?

Yesu si Mungu. Yesu ni wa pekee—yeye tu ndiye aliyeumbwa moja kwa moja na Mungu. Hiyo ndiyo sababu Biblia humwita Mwana wa Mungu. (Yohana 20:31) Baada ya kumuumba, Yehova alimtumia Yesu, mzaliwa wake wa kwanza, kuwa “mfanyakazi stadi” ili kuumba vitu vyote na viumbe wote.—Methali 8:30, 31; Wakolosai 1:15, 16.

Yesu Kristo hakuwahi kudai kamwe kuwa yeye ni Mungu. Badala yake, alieleza hivi: “Mimi ni mwakilishi kutoka [kwa Mungu], naye Ndiye aliyenituma.” (Yohana 7:29) Alipokuwa akizungumza na mmoja wa wanafunzi wake, Yesu alimwita Yehova “Baba yangu na Baba yenu” na “Mungu wangu na Mungu wenu.” (Yohana 20:17) Yesu alipokufa, Yehova alimfufua na kumpa mamlaka kubwa mbinguni akiwa katika mkono Wake wa kuume.—Mathayo 28:18; Matendo 2:32, 33.

Yesu Kristo Anaweza Kukusaidia Kumkaribia Mungu

Yesu alikuja duniani ili kutufundisha kumhusu Baba yake. Yehova mwenyewe alisema hivi kumhusu Yesu: “Huyu ni Mwanangu, mpendwa. Msikilizeni.” (Marko 9:7) Yesu anamjua Mungu vizuri kuliko mtu mwingine yeyote. Alisema hivi, “Hakuna anayemjua Baba isipokuwa Mwana, na yeyote ambaye Mwana anapenda kumfunulia.”—Luka 10:22.

Yesu humwiga Mungu kikamilifu. Yesu aliiga sifa za Baba yake kikamilifu hivi kwamba alisema: “Yeyote ambaye ameniona mimi amemwona Baba pia.” (Yohana 14:9) Yesu aliwasaidia watu wamkaribie Mungu kwa kuwaonyesha upendo kama wa Baba yake kupitia maneno na matendo yake. Alisema hivi: “Mimi ndiye njia na kweli na uzima. Hakuna mtu anayekuja kwa Baba bila kupitia kwangu.” (Yohana 14:6) Pia, alisema hivi: “Waabudu wa kweli watamwabudu Baba kwa roho na kweli, kwa maana kwa kweli, Baba anawatafuta watu wa namna hiyo wamwabudu.” (Yohana 4:23) Hebu fikiria hilo! Yehova anawatafuta watu kama wewe wanaotaka kujua ukweli kumhusu yeye.