Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

HABARI KUU

Tumaini kwa Watu Maskini na Wasio na Makao

Tumaini kwa Watu Maskini na Wasio na Makao

Joe ni mwanajeshi mstaafu wa Marekani. Yeye pamoja na familia yake walikabili janga ambalo limewaacha bila makao kwa miaka 18. Kwa mwaka mmoja Joe alitembelea maktaba ya umma katika eneo lao, na kuzungumza na mhudumu wa maktaba hiyo. Mazungumzo hayo yalibadili maisha yake.

Martín, kijana kutoka nchini Argentina alikuwa na njaa ya kiroho. Maisha yake yalikuwa bila kusudi. Alipokuwa akitafuta kusudi la maisha aliamua kuondoka nyumbani na kuanza kuishi katika ufuo wa bahari. Hata hivyo, alivunjika moyo sana kwa sababu hakupata majibu ya maswali aliyokuwa akitafuta. Alilia na kumsihi Mungu hivi: “Ikiwa upo, tafadhali nisaidie nikujue.” Matokeo yalikuwaje? Tutaona.

WATU hukosa makao kwa sababu mbalimbali. Baadhi yao, kama vile Joe, walipatwa na majanga fulani. Na wengine kama Martín huamua kuacha maisha ya “kawaida” wakiyaona kuwa ni utaratibu usio na maana. Hata hivyo, wengine hawana makao kwa sababu ya umaskini, misiba ya asili, jeuri ya nyumbani, matumizi mabaya ya dawa za kulevya au pombe, magonjwa ya akili, kukosekana kwa nyumba au kupoteza kazi.

Katika nchi zinazoendelea au zile zilizo na vita au zenye matatizo ya kiuchumi, ukosefu wa makazi “limekuwa tatizo kubwa katika nchi nyingi zinazoendelea,” anasema profesa wa saikolojia, Paul Toro. * Sababu zinazochangia zinaweza kutia ndani sera za serikali kuhusu misaada kwa watu wenye kipato cha chini na tofauti inayoongezeka kati ya matajiri na maskini.

Watu wengi wanahangaikia wakati wao ujao. Hata hivyo, baadhi yao wameacha kuhangaika kwa kuchunguza kile inachosema Biblia kuhusu wakati ujao. Tutazungumzia jambo hilo. Biblia inaweza pia kutusaidia sasa kwa kutupatia kanuni bora tunazoweza kufuata. Kanuni hizo zinaweza kutusaidia kuboresha hali yetu ya kiuchumi na kihisia, kama Joe na Martín walivyofaidika.

BIBLIA ILIBADILI MAISHA YAKE

Cindi aliyekuwa akifanya kazi katika maktaba alisema hivi: “Joe alionekana kuwa mwenye akili, mwenye adabu, na mnyenyekevu.” Akiwa Shahidi wa Yehova, Cindi alimpatia Joe magazeti ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni! na kumwalika kuhudhuria mikutano ya Kikristo. Alipohudhuria mikutano hiyo, alitendewa kwa heshima na fadhili hivyo akaanza kuhudhuria mikutano hiyo kwa ukawaida. Pia, alikubali kufundishwa Biblia na Shahidi wa Yehova.

Kujifunza Biblia kulimsaidia Joe kuanza kujiheshimu

Joe alifarijiwa sana na aliyojifunza, naye akaanza kutumia mafundisho ya Biblia, ingawa kufanya hivyo kungemaanisha kufanya mabadiliko makubwa maishani mwake. Kwa mfano, alijifunza kwamba uhai ni zawadi yenye thamani kutoka kwa Mungu inayopaswa kuheshimiwa, na kwamba kuvuta sigara huchafua mwili. (Zaburi 36:9) Hivyo, akaacha kuvuta sigara, kulingana na kanuni inayoelezwa katika 2 Wakorintho 7:1: “Acheni tujisafishe wenyewe kila unajisi wa mwili na roho.” Bila shaka, uamuzi wa Joe haukuwa na faida tu kiafya bali pia uliokoa pesa zake.

Baada ya kufikiria kwa uzito ushauri wa Biblia unaotaja kwamba tunahitaji kufanya kazi ili kupata riziki, Joe alianza kutafuta kazi. * (1 Wathesalonike 4:11, 12) Andiko la Mhubiri 2:24 linasema hivi: “Kwa mwanadamu hakuna jambo bora kuliko kwamba ale, naam, anywe na kuifanya nafsi yake ione mema kwa sababu ya kazi yake ngumu.” Shangwe hiyo pia hutokana na kujiheshimu kwa sababu ya kufanya kazi kwa unyofu. Na hilo hutuwezesha kutimiza mahitaji ya wengine.—Waefeso 4:28.

Baada ya kuona unyofu wa Joe, “kutanikoni lilimkaribisha, pia walimsaidia kupata nyumba ya kuishi na vitu vingine alivyostahili kuwa navyo,” akasema Cindi. Joe aliendelea kufanya maendeleo na baada ya muda alibatizwa na kuwa Shahidi wa Yehova. Sasa anaweza kueleza kutokana na mambo aliyojionea mwenyewe anapowatia moyo wengine kufuatia hekima ya Mungu, iliyo katika Biblia.—Methali 3:13, 14.

ALIPATA KUSUDI LA MAISHA

Martín alianza kutafuta kusudi la maisha alipokuwa na umri wa miaka 20. Anasema hivi: “Nilichunguza dini, falsafa na kutumia dawa za kulevya nikitumaini kwamba zingetosheleza uhitaji wangu, lakini jitihada hizo ziliambulia patupu.” Aliishi California, Marekani, kwa kipindi fulani na baadaye akahamia Hawaii. “Nilifikiri nimeipata paradiso,” anakumbuka. Lakini mazingira maridadi hayakutosheleza uhitaji wake. “Nilishuka moyo sana,” anakumbuka, “hata nilifikiria kujiua.” Pindi hiyo alilia sana na kumsihi Mungu hivi: “Ikiwa upo, tafadhali nisaidie nikujue.”

Sasa Martín amekuwa na mtazamo mzuri kuhusu uhai

Martín alikumbuka kwamba mapema aliona bango lililosomeka hivi “Jumba la Ufalme la Mashahidi wa Yehova.” Aliamua kwenda hapo ili kuhudhuria mkutano wa Kikristo. Anasema hivi: “Niliingia nikiwa na nywele ndefu na ndevu nyingi, nilivaa nguo ambazo nilikuwa nimezivaa kwa miezi kadhaa, hata hivyo, nilikaribishwa kwa shangwe.” Martín alikubali funzo la Biblia, na alitembea kwa ukawaida kutoka “nyumbani,” yaani, ufuoni mwa bahari hadi mjini ili kujifunza Biblia.

Mwishowe, Martín alianza kupata majibu yenye kuridhisha ya maswali yake. Matokeo ni kwamba, huzuni yake ilikwisha na alianza kupata shangwe aliyotaja Yesu aliposema: “Wenye furaha ni wale wanaotambua uhitaji wao wa kiroho.”—Mathayo 5:3.

“Watu walishangazwa na mabadiliko niliyokuwa nikifanya”

Mtazamo mpya wa maisha wa Martín ulionekana haraka alipotumia kanuni zilezile za Biblia zilizomsaidia Joe, aliyetajwa mapema, kuongoza maisha yake. Martín alianza kurekebisha mwonekano wake, na Mashahidi walimsaidia kupata kazi na mahali pa kuishi. Anasema: “Mwanzoni nilijulikana kuwa mwanaume asiye na makao na anayeishi mitaani, lakini sasa watu walionifahamu walishangazwa na mabadiliko niliyokuwa nikifanya.”

Hatimaye, Martín alirudi Argentina, ambako alibatizwa na kuwa Shahidi wa Yehova. Sasa anafurahia pendeleo la kuwasaidia wengine wenye njaa ya kiroho kupata majibu ya maswali muhimu maishani.

WAKATI AMBAPO KUTOKUWA NA MAKAO NA UMASKINI HAUTAKUWAPO TENA

Yeremia mtumishi wa kale wa Mungu, aliishi katika kipindi kilichokuwa na matatizo makubwa. Maadui walishambulia jiji lao na kuwachukua watu wengi kuwa mateka na watumwa. (Maombolezo 1:3) Ingawa aliokoka, Yeremia alipoteza kila kitu alichokuwa nacho. Akiwa na huzuni, alisali hivi: “Ukumbuke mateso yangu na hali yangu ya kukosa makao.”—Maombolezo 3:19.

Licha ya mateso aliyokabili, Yeremia hakukata tamaa. Kwa nini? Alijua kwamba Yehova hangemwacha. (Yeremia 1:8) Pia, alijifunza Maandiko, yanayotaja wakati ambapo umaskini na kuteseka hakutakuwapo, badala yake kutakuwa na amani na usalama wa kweli.—Zaburi 37:10, 11.

Mabadiliko hayo yataletwa si kutokana na jitihada za wanadamu bali kupitia serikali kamilifu inayoitwa Ufalme wa Mungu. (Danieli 7:13, 14) Mfalme wa Ufalme huo si mwingine ila Yesu Kristo, ambaye alipokuwa mwanadamu duniani, aliwahurumia sana maskini. (Luka 7:22; 14:13) Chini ya utawala wake, “mwadilifu atachipuka, na wingi wa amani . . . Atamkomboa maskini anayelilia msaada, pia mwenye kuteseka na yeyote ambaye hana msaidizi. Ataikomboa nafsi yao kutoka katika ukandamizaji na katika jeuri.”—Zaburi 72:7, 12, 14.

“Watajenga nyumba na kukaa ndani yake.”—Isaya 65:21

Ufalme wa Mungu ulikuwa jambo kuu katika mafundisho ya Yesu. (Luka 4:43) Hata aliwafundisha watu kusali hivi: “Ufalme wako na uje. Mapenzi yako na yatendeke duniani kama ilivyo mbinguni.” (Mathayo 6:9, 10) Maisha yatakuwaje Ufalme wa Mungu utakapoitawala dunia? Biblia hutueleza mambo yenye kupendeza. Kwa mfano, inasema hivi kuhusu raia wa Ufalme wa Mungu:

  • “Na hakika wao watajenga nyumba na kukaa ndani yake; na hakika wao watapanda mashamba ya mizabibu na kula matunda yake. Hawatajenga na mtu mwingine akae ndani yake; hawatapanda na mtu mwingine ale. . . . Watu wangu waliochaguliwa wataitumia kazi ya mikono yao wenyewe kikamilifu.”—Isaya 65:21, 22.

  • “Nao wataketi, kila mtu chini ya mzabibu wake na chini ya mtini wake, wala hakutakuwa na mtu yeyote anayewatetemesha; kwa maana kinywa cha Yehova wa majeshi kimesema hivyo.” —Mika 4:4.

Tumaini hilo hutuimarisha tunapokabili majaribu. Wakati huohuo, kanuni za Biblia zinaweza kutusaidia kuishi maisha yenye kusudi na yenye kuridhisha hata sasa, kama ambavyo Joe, Martín, na wengine wengi walivyojionea. Kwa kweli, Muumba wetu, Yehova Mungu, anatuhakikishia hivi: “Mtu anayenisikiliza, yeye atakaa salama wala hatasumbuliwa na hofu ya msiba.” (Methali 1:33) Na maneno hayo yawe kweli maishani mwako!

^ fu. 6 Kwa sababu ya migogoro, jeuri au mateso, mamilioni ya watu wamelazimika kukimbia makazi yao na kuwa wakimbizi au kuwa bila makao nchini mwao. Tatizo hilo limezungumziwa katika gazeti la Amkeni! la Januari 22, 2002.

^ fu. 11 Baadhi ya watu wanaotaka kufanya kazi hawawezi kwa sababu ya ulemavu, afya mbaya, au uzee. Mungu hapendezwi na mtu ambaye “hataki kufanya kazi.” —2 Wathesalonike 3:10.