Hamia kwenye habari

BIBLIA INABADILI MAISHA

“Niliishi Mitaani”

“Niliishi Mitaani”
  • Alizaliwa: 1955

  • Nchi: Hispania

  • Historia: Nilitumia Dawa za Kulevya, Kileo, na Nilikuwa Mkatili

MAISHA YANGU YA ZAMANI

 Ni vigumu kwa watu fulani kujifunza kutokana na makosa waliyofanya maishani. Mimi nilikuwa hivyo. Nilizaliwa na kulelewa jijini Barcelona, jiji la pili kwa ukubwa nchini Hispania. Familia yetu iliishi Somorrostro, eneo ambalo lilikuwa karibu na ufukwe wa bahari. Eneo hilo lilijulikana kwa uhalifu mwingi na uuzaji wa dawa za kulevya.

 Wazazi wangu walikuwa na watoto tisa, nami nilikuwa mtoto wa kwanza kati yao. Kwa kuwa familia yetu ilikuwa maskini sana, baba yangu alinipeleka kwenye klabu ya tenisi na nikaajiriwa kuokota mipira iliyotoka nje ya uwanja wakati wa michezo. Nilikuwa na umri wa miaka kumi na nilifanya kazi kwa saa kumi kila siku. Kwa sababu hiyo sikupata nafasi ya kwenda shuleni kama watoto wengine. Nilipokuwa na umri wa miaka 14 nilianza kufanya kazi kwenye duka la utengenezaji wa vifaa vya chuma.

Katika mwaka wa 1975, nilijiunga na Kikosi cha Kigeni cha Hispania cha Afrika Kaskazini na nilivalia sare ya kikosi hicho

 Katika mwaka wa 1975, niliandikishwa jeshini, kwa kuwa utumishi huo ulikuwa wa lazima nchini Hispania. Nilitaka kufanya jambo lenye kusisimua maishani mwangu hivyo nilijitolea kwenye Kikosi cha Kigeni cha Hispania huko Melilla, eneo la Afrika Kaskazini linalomilikiwa na Hispania. Wakati huo, nilianza kutumia kileo kupita kiasi na dawa za kulevya.

 Nilipotoka jeshini, nilirudi jijini Barcelona na kuunda genge. Tuliiba chochote ambacho tungeweza. Kisha tuliuza vitu hivyo na kununua dawa za kulevya. Nilianza kutumia dawa kali zaidi za kulevya (LSD na amphetamines), na kujiingiza zaidi kwenye matumizi mabaya ya kileo, maisha mapotovu kingono, na kucheza kamari. Maisha hayo mabaya yalinifanya niwe mkatili zaidi. Nilibeba kisu, shoka, au panga, na sikuogopa kuvitumia ilipohitajika.

 Pindi moja, mimi na genge langu tuliiba gari na polisi wakaanza kutukimbiza. Ni kana kwamba tulikuwa tukiigiza sinema. Tuliendesha gari hilo kwa umbali wa kilomita 30 hivi, kisha polisi wakaanza kutufyatulia risasi. Hatimaye, tulipata aksidenti na sote tukakimbia. Baba yangu alipogundua jambo hilo, alinifukuza nyumbani.

 Kwa miaka mitano iliyofuata, niliishi mitaani. Nililala kwenye malori, milangoni, bustanini, na makaburini. Hata kwa muda fulani niliishi pangoni. Maisha yangu hayakuwa na kusudi lolote, sikujali hata ikiwa ningekufa. Hata ninakumbuka pindi fulani nilipokuwa nimetumia dawa za kulevya nilijikata mikono. Bado nina makovu ya pindi hiyo.

JINSI BIBLIA ILIVYOBADILI MAISHA YANGU

 Nilipokuwa na umri wa miaka 28, mama alikuja kunitafuta na kuniambia nirudi nyumbani. Nilikubali na kumwahidi kwamba nitarekebisha maisha yangu, lakini ilinichukua muda mrefu kutimiza ahadi hiyo.

 Siku moja mchana, Mashahidi wawili wa Yehova walibisha mlango wetu. Nilipokuwa nikiwasikiliza, Baba aliniambia kwa sauti nifunge mlango. Kwa kuwa sikupenda kuamrishwa, niliamua kumpuuza. Walinipa vitabu vitatu vidogo, nami nilikubali kuvipokea. Niliwauliza wanafanyia wapi ibada, na siku chache baadaye nilienda kwenye Jumba la Ufalme.

 Jambo la kwanza nililotambua ni kwamba kila mtu alikuwa nadhifu. Lakini mimi nilikuwa na nywele ndefu, nilikuwa nimevalia ovyoovyo, na sikuwa nimenyoa ndevu kwa muda mrefu. Nilihisi sistahili kuingia, hivyo niliamua kubaki nje ya jumba. Nilishangaa kumwona Juan ambaye zamani tulikuwa katika genge moja la uhalifu akiwa amevalia suti. Nilipomwona nilipata ujasiri wa kuingia ndani na kuhudhuria mkutano. Baadaye niligundua kwamba Juan alianza kuwa Shahidi wa Yehova mwaka mmoja hivi mapema. Maisha yangu yalianza kubadilika tangu wakati huo.

 Nilikubali kujifunza Biblia na upesi nikagundua kuwa ili nipate kibali cha Mungu, ninahitaji kuacha jeuri na mwenendo mpotovu. Haikuwa rahisi kufanya mabadiliko hayo. Ili kumpendeza Yehova Mungu, nilipaswa ‘kugeuzwa kwa kufanya upya akili yangu.’ (Waroma 12:2) Niliguswa sana na rehema za Mungu. Licha ya makosa yangu nilihisi kwamba alikuwa akinipa nafasi ya kubadili maisha yangu. Mambo niliyojifunza kumhusu Yehova Mungu yalipenya ndani kabisa ya moyo wangu. Ilikuwa wazi kwamba kuna Muumba anayenijali.​—1 Petro 5:6, 7.

 Hilo lilinichochea nianze kufanya mabadiliko. Kwa mfano, nilipojifunza kwamba ni kosa kutumia tumbaku, nilijiambia hivi: ‘Ikiwa Yehova Mungu anataka niwe safi na nijisafishe kila unajisi, ninapaswa kuacha kuvuta sigara!’ (2 Wakorintho 7:1) Nilitupa sigara zote.

 Pia, nilihitaji kuacha kuuza na kutumia dawa za kulevya. Muda mwingi na jitihada zilihitajika ili nifanye mabadiliko hayo. Nilijua kwamba ili nifaulu, nilipaswa kuacha kushirikiana na marafiki wangu wa zamani. Uvutano wao ulinizuia nisifanye maendeleo ya kiroho. Hata hivyo, baada ya muda nilianza kumtegemea Mungu zaidi na kutegemea msaada wa marafiki wangu wapya kutanikoni. Walinionyesha upendo mwingi sana. Sikuwa nimewahi kutendewa hivyo maishani mwangu. Kadiri muda ulivyopita, nilifaulu kuacha kutumia dawa za kulevya na ‘nikavaa utu mpya.’ Hilo lilinisaidia kupata kibali cha Mungu. (Waefeso 4:​24) Nilibatizwa Agosti 1985 na kuwa Shahidi wa Yehova.

JINSI AMBAVYO NIMEFAIDIKA

 Biblia ilinisaidia kuwa na maisha bora zaidi. Iliniweka huru kutokana na maisha mabaya yenye kuaibisha na ambayo yalikuwa yakidhuru mwili wangu. Isitoshe, zaidi ya watu 30 ambao nilishirikiana nao mwanzoni walikufa wakiwa na umri mdogo kutokana na ugonjwa wa UKIMWI au matatizo mengine yanayosababishwa na dawa za kulevya. Ninashukuru sana kwamba kwa sababu ya kutumia kanuni za Biblia nilifaulu kuepuka madhara hayo yaliyowapata wenzangu.

 Siku hizi sibebi tena visu na mashoka kama nilivyofanya nilipokuwa kijana. Sikuwahi kuwazia kwamba siku moja nitakuwa nikibeba Biblia na kuitumia kuwasaidia watu. Sasa, mimi na mke wangu tunatumikia tukiwa watumishi wa wakati wote wa Mashahidi wa Yehova.

 Wazazi wangu hawajawahi kuwa Mashahidi wa Yehova lakini wanathamini kwamba kujifunza Biblia kumenifanya niwe na maisha mazuri. Isitoshe, baba yangu aliwatetea Mashahidi mbele ya wafanyakazi wenzake. Ilikuwa wazi kwake kwamba imani yangu mpya ilinisaidia kufanya mabadiliko makubwa maishani. Mara nyingi mama yangu alisema nilipaswa kuanza kujifunza Biblia mapema zaidi. Ninakubaliana naye kabisa!

 Mambo ambayo nimejionea maishani yamenifundisha kwamba kutumia dawa za kulevya au njia nyingine kama hizo hakumfanyi mtu awe na maisha yenye kuridhisha. Ninahisi kwamba nimeridhika kwa sababu ninawasaidia wengine kujifunza Neno la Mungu ambalo liliokoa maisha yangu.