Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

 MSAADA KWA AJILI YA FAMILIA | VIJANA

Kupokea au Kutuma Ujumbe kwa Adabu

Kupokea au Kutuma Ujumbe kwa Adabu

KIKWAZO

Unazungumza ana kwa ana na rafiki yako, na ghafula unapokea ujumbe wa simu. Unapaswa kufanya nini?

  1. Kuusoma ujumbe huo huku ukizungumza na rafiki yako.

  2. Kumwambia rafiki yako “samahani” kisha usome ujumbe huo.

  3. Kupuuza ujumbe huo na kuendelea kuzungumza na rafiki yako.

Kati ya mambo hayo, je, kuna lolote unalopaswa kufanya? Jibu ni ndiyo!

UNACHOPASWA KUJUA

Kumwandikia rafiki yako ujumbe huku ukizungumza na rafiki mwingine ni kama kucheza mchezo uupendao bila kuzingatia sheria za mchezo huo. ‘Lakini hawa ni rafiki zangu,’ huenda ukajitetea. Na hiyo ndiyo sababu unapaswa kuwa na adabu. Si kwamba uwe mtu asiyependa mzaha wala ucheshi. Lakini huu ndio ukweli wa mambo: Usipokuwa na adabu unapokuwa na rafiki zako, baada ya muda wataacha kuwa rafiki zako.

Kwa nini? Kwa sababu watu hawapendi kudharauliwa. Msichana anayeitwa Beth * anasema, “Mimi huudhika ninapozungumza na rafiki ambaye anatazama simu yake kila mara kana kwamba anatazamia jambo bora zaidi!” Unafikiri Beth ataendelea kumvumilia rafiki huyo kwa muda gani?

Ili kuchunguza unavyotenda unapopokea ujumbe wa simu, fikiria hali iliyotajwa kwenye sehemu ya “Kikwazo.” Ungechagua kutumia dokezo gani? Inaelekea, umetambua kwamba Dokezo la A si la adabu. Lakini vipi kuhusu Dokezo la B na C? Je, ni kukosa adabu kukatisha mazungumzo ili usome ujumbe wa simu? Au je, ni utovu wa nidhamu kupuuza ujumbe wa simu ili uendelee na mazungumzo?

Kama unavyoona, ni rahisi kutokuwa na adabu. Lakini Biblia inaweza kukusaidia. Inasema hivi: “Kama vile mnavyotaka watu wawatendee ninyi, watendeeni wao vivyo hivyo.” (Luka 6:31) Unaweza kutumia ushauri huo kuhusiana na ujumbe wa simu. Jinsi gani?

 UNACHOWEZA KUFANYA

Tuma ujumbe wa simu wakati unaofaa. “Nyakati nyingine mimi hupokea ujumbe wa simu usiku sana,” anasema kijana anayeitwa Richard. “Huenda hata si jambo muhimu, na linanipotezea usingizi!” Jiulize hivi, ‘Je, mimi huwatumia watu ujumbe wa simu wakati ambao huenda wamelala?’—Kanuni ya Biblia: Mhubiri 3:1.

Uwe mwenye adabu. Mawasiliano yanahusisha maneno, sauti, sura, na mwili wako. Lakini unapoandika ujumbe huwezi kutumia mambo hayo yote. Basi, unawezaje kutumia busara? “Tumia maneno yanayoonyesha adabu,” anapendekeza mwanamke anayeitwa Jasmine. “Uliza, ‘Unaendeleaje?’ na utumie maneno kama vile ‘tafadhali’ na ‘asante.’”—Kanuni ya Biblia: Wakolosai 4:6.

Tumia utambuzi. Fikiria tena hali iliyo kwenye sehemu ya “Kikwazo.” Kama unatazamia ujumbe muhimu, huenda ikafaa kuomba radhi na kukatisha mazungumzo. Hata hivyo, huenda si ujumbe wa dharura. “Bado utakuwa na simu yako baada ya kumaliza kuzungumza na rafiki yako,” anasema Amy mwenye umri wa miaka 17, “lakini huenda rafiki yako atakuwa ameondoka utakapomaliza kusoma na kujibu ujumbe wa simu.” Vivyo hivyo, unaweza kutumia utambuzi unapokuwa katika kikundi. “Usitume na kupokea ujumbe muda wote,” anasema Jane mwenye umri wa miaka 18. “Kufanya hivyo ni kama kuwaambia watu, ‘Sitaki kushirikiana nanyi, afadhali ningekuwa mahali pengine.’”

Fikiria kwa makini kabla ya kutuma ujumbe. Je, inawezekana kwamba ujumbe wako utaeleweka vibaya? Je, unaweza kuongeza picha ndogo kuonyesha hisia inayofaa? “Kama unafanya mzaha, weka picha ya mtu anayetabasamu,” anasema Amber mwenye umri wa miaka 21. “Huenda watu wakaumia hisia, na hata kukawa na mgogoro, wasipoelewa kwamba ujumbe uliotuma ni wa mzaha.”—Kanuni ya Biblia: Methali 12:18.

Kwa kweli ni muhimu kuonyesha adabu unapotumia simu!

Jambo la kufikiria: Adabu inategemea upendo. Sifa hiyo huonyeshwaje? Biblia inasema: “Upendo ni wenye ustahimilivu na wenye fadhili. Upendo hauna wivu, haujigambi, haujivuni, haujiendeshi bila adabu, hautafuti faida zake wenyewe, hauchokozeki.” (1 Wakorintho 13:4, 5) Ni jambo gani kuhusiana na upendo ambalo unahitaji kufanyia marekebisho?

^ fu. 11 Baadhi ya majina katika makala hii yamebadilishwa.

Pata msaada zaidi kwa ajili ya familia kwenye www.pr418.com/sw