Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

 MSAADA KWA AJILI YA FAMILIA | KULEA WATOTO

Jinsi ya Kuwasaidia Vijana Waepuke Hatari Kwenye Intaneti

Jinsi ya Kuwasaidia Vijana Waepuke Hatari Kwenye Intaneti

KIKWAZO

Ripoti zinaonyesha kwamba Intaneti imejaa watu wanaotumia mtandao kuwachokoza wengine, watu wanaowavizia wengine ili wafanye ngono nao, na wezi wa utambulisho. Hivyo una sababu nzuri ya kuhangaika: Hasa ikiwa kijana wako hutumia Intaneti mara nyingi na inaelekea haelewi hatari za Intaneti.

Unaweza kumfundisha kijana wako jinsi ya kuepuka hatari kwenye Intaneti. Hata hivyo, kwanza, fikiria mambo unayohitaji kujua kuhusu Intaneti.

MAMBO UNAYOPASWA KUJUA

Vijana wanaweza kupata Intaneti kwenye vifaa vya kielektroniki vinavyobebwa. Ni vizuri kuweka kompyuta mahali palipo wazi nyumbani. Hata hivyo, akiwa na kompyuta ya kisasa ya mkononi (tablet) au simu ya hali ya juu (smartphone) kijana wako anaweza kutumia Intaneti akiwa peke yake.

Kwa kuwa madereva wengi wamewahi kupata aksidenti, haimaanishi kwamba haifai kuendesha gari. Ndivyo ilivyo na matumizi ya Intaneti. Kijana wako anahitaji kujifunza kuitumia vizuri.

Vijana fulani hutumia muda mwingi kwenye Intaneti. Msichana fulani mwenye umri wa miaka 19 anakiri hivi: “Mimi hufungua kompyuta ili nisome barua-pepe kwa dakika tano lakini ninapata nimetazama video kwa saa nyingi. Ninahitaji kujizuia sana.”

Vijana wanaweza kuweka habari nyingi za kibinafsi kwenye Intaneti. Watu walio na nia mbaya wanaweza kutumia maelezo na picha za kijana kwenye Intaneti kujua mahali anapoishi, shule anayosoma, na anapokuwa peke yake nyumbani.

Vijana wengi hawajui matokeo ya habari wanazoweka kwenye Intaneti. Mambo yanayowekwa kwenye Intaneti hubaki humo. Mara nyingine picha na maelezo yenye kuaibisha hupatikana baadaye—kwa mfano, na mwajiri anapofanya uchunguzi kumhusu mtu anayeomba kazi.

Licha ya mambo hayo, kumbuka kwamba: Intaneti si adui yako. Badala yake, tatizo ni kutumia vibaya Intaneti.

 MAMBO UNAYOWEZA KUFANYA

Mfundishe kijana kutanguliza mambo muhimu na kutumia wakati vizuri. Kuwa mtu mzima mwenye kutegemeka kunatia ndani kujifunza kutanguliza mambo muhimu. Mazungumzo katika familia, kazi za shuleni na za nyumbani ni muhimu kuliko kutumia tu Intaneti. Ikiwa kijana wako anatumia muda mwingi kwenye Intaneti, weka mipaka na ikilazimu mpangie muda hususa.—Kanuni ya Biblia: Wafilipi 1:10.

Mfundishe kijana kuwa mwangalifu anapoandika habari kwenye Intaneti. Msaidie kijana wako ajiulize maswali kama haya: Je, maelezo nitakayoandika yanaweza kumuumiza mtu? Picha hii itaathirije jinsi wengine wanavyoniona? Je, nitaaibika ikiwa wazazi wangu au watu wengine wazima wataona picha au maelezo haya? Watasema nini kunihusu ikiwa wataona habari hizo? Mimi ningemwonaje mtu ambaye angeandika maelezo kama haya au kuweka picha kama hii?—Kanuni ya Biblia: Methali 10:23.

Mfundishe kijana ajiwekee viwango bali si kufuata sheria tu. Huwezi kusimamia kila kitu anachofanya kijana wako. Isitoshe, lengo lako ukiwa mzazi si kuwadhibiti watoto wako bali ni kuwasaidia ili “nguvu zao za ufahamu [zizoezwe] kutofautisha yaliyo sawa na yaliyo makosa pia.” (Waebrania 5:14) Hivyo, badala ya kukazia sheria na adhabu kuwa mambo ya msingi, mhimize kijana wako atumie uwezo wake wa kupambanua mema na mabaya. Anataka watu wawe na maoni gani kumhusu? Anataka ajulikane kwa sifa gani? Lengo lako ni kumsaidia kijana wako afanye maamuzi yanayofaa popote alipo.—Kanuni ya Biblia: Methali 3:21.

“Watoto wanajua mengi kuhusu teknolojia. Nao wazazi wanajua mengi kuhusu maisha”

Kutumia intaneti, sawa na kuendesha gari, kunahitaji maamuzi mazuri—si kujua tu kuitumia. Kwa hiyo, mwongozo wako ukiwa mzazi ni muhimu. Kwa kweli, ni kama anavyosema Parry Aftab, mtaalamu wa usalama kwenye Intaneti, “Watoto wanajua mengi kuhusu teknolojia. Nao wazazi wanajua mengi kuhusu maisha.”