Hamia kwenye habari

MISTARI YA BIBLIA YAFAFANULIWA

Isaya 26:3—“Utamlinda Yeye Ambaye Moyo Wake Umekutegemea Katika Amani Kamilifu”

Isaya 26:3—“Utamlinda Yeye Ambaye Moyo Wake Umekutegemea Katika Amani Kamilifu”

 “Utawalinda wale wanaokutegemea kikamili; utawapa amani inayodumu, kwa sababu wanakutumaini wewe.”​—Isaya 26:3, Tafsiri ya Ulimwengu Mpya.

 “Utamlinda yeye ambaye moyo wake umekutegemea katika amani kamilifu, kwa kuwa anakutumaini.”​—Isaya 26:3, Union Version.

Maana ya Isaya 26:3

 Nabii Isaya alitumia maneno hayo yenye kutoa uhakikisho kuonyesha kwamba Mungu anawalinda wale wanaomtegemea kikamili. Anafanya hivyo kwa kuwasaidia wajihisi salama na kwamba wana amani.

 “Utawalinda wale wanaokutegemea kikamili.” Sehemu hii ya mstari huo inawafafanua wale ambao wameazimia kabisa akilini mwao kumtegemea Yehova a Mungu nyakati zote. Wale wanaomtumaini Mungu wanatambua kwamba wanahitaji kumtegemea kikamili. Kwa mfano, hawategemei mawazo yao wenyewe wanapofanya maamuzi muhimu. Badala yake, wanazingatia mawazo ya Mungu katika kila jambo wanalofanya. (Methali 3:5, 6) Wanajifunza maoni ya Mungu kuhusu jambo fulani kwa kusoma kwa makini Neno lake, Biblia, na kwa kutafakari kwa undani mambo waliyosoma. (Zaburi 1:2; 119:15) Wanapokabili hali ngumu, wanasali kwa Yehova kwa unyoofu na kumwomba msaada. (Zaburi 37:5; 55:22) Wanapofanya hivyo, wanaonyesha uhakika wao katika Mungu, naye anawapa amani.

 “Utawapa amani inayodumu.” Katika Kiebrania cha awali, neno “amani” limeandikwa mara mbili ili kutia mkazo; hivyo, ili kuwasilisha mkazo huo, neno hilo linaweza kutafsiriwa “amani inayodumu,” “amani kamilifu,” au “amani kamili.” Kwa maneno mengine, wale wanaomtegemea Yehova kikamili wanapata hisi ya amani, amani ya ndani ambayo haitegemei hali wanazokabili. (Zaburi 112:7; 119:165) Amani hii inatokana na kuwa na uhusiano wa karibu na wa kibinafsi pamoja na Yehova na kujitahidi kufanya yaliyo sawa machoni pake.​—Methali 3:32; Isaya 48:18.

 Hiyo “amani inayodumu” haimaanishi Mungu anawazuia waabudu wake wasipatwe na magumu na hivyo kuwaondolea mahangaiko yote. (1 Samweli 1:6, 7; Ayubu 6:1, 2; Zaburi 31:9) Badala yake, anawasaidia kukabiliana na hali ngumu wanazokabili. (Isaya 41:10, 13) Anatenda kupatana na sala zao, akiwapa hekima, nguvu, na faraja. (Zaburi 94:19; Methali 2:6; Isaya 40:29) Kwa sababu hiyo, wanaweza kuendelea kuwa watulivu hata wanapopatwa na hali ngumu.​—Wafilipi 4:6, 7.

Muktadha wa Isaya 26:3

 Nabii Isaya aliishi katika karne ya nane K.W.K. Watu wengi walioishi Yuda wakati huo, na katika miaka iliyofuata, hawakumwabudu Yehova Mungu kwa uaminifu. Kwa sababu hiyo, hatimaye Yehova aliruhusu Yerusalemu, mji wao mkuu, uharibiwe katika mwaka wa 607 K.W.K.

 Hata hivyo, zaidi ya miaka mia moja kabla ya uharibifu huo, Isaya aliandika wimbo wa kinabii wa kumsifu Yehova. Wimbo huo unapatikana katika sura ya 26. (Isaya 26:1-6) Wimbo huo ulionyesha kwamba wakati ujao jiji katika nchi ya Yuda, ambalo inaonekana ni Yerusalemu, lingejengwa upya.

 Yerusalemu lilijengwa upya baada ya mwaka wa 537 K.W.K. Hilo lilipotukia, Wayahudi waaminifu waliokuwa wamerudishwa wangeweza kujihisi salama na kusema: “Tuna jiji imara.” (Isaya 26:1) Hata hivyo, si kuta zilizoimarishwa zilizofanya jiji hilo liwe imara. Badala yake, usalama wa jiji hilo ulitegemea baraka na ulinzi wa Yehova.​—Isaya 26:2.

 Hivyo ndivyo ilivyo leo. Wale wanaomtegemea Yehova kikamili wanajihisi salama kwa sababu wanamwona kuwa “Mwamba” wao, au kimbilio lao.​—Isaya 26:4.

 Tazama video hii fupi ili upate habari zaidi kuhusu kitabu cha Isaya.

a Yehova ni jina la kibinafsi la Mungu. (Zaburi 83:18) Ona makala “Yehova Ni Nani?