Hamia kwenye habari

Kwa Nini Yesu Anaitwa Mwana wa Mungu?

Kwa Nini Yesu Anaitwa Mwana wa Mungu?

Jibu la Biblia

 Mara nyingi Biblia inamwita Yesu “Mwana wa Mungu.” (Yohana 1:49) Maneno “Mwana wa Mungu” yanaonyesha kwamba Mungu ndiye Muumba, au Chanzo, cha uhai wote kutia ndani uhai wa Yesu. (Zaburi 36:9; Ufunuo 4:11) Biblia haifundishi kwamba Mungu alimzaa mwana kihalisi kwa njia ileile ambayo wanadamu huzaa watoto.

 Pia, Biblia inawaita malaika “wana wa Mungu wa kweli.” (Ayubu 1:6) Na Biblia inasema kwamba mwanadamu wa kwanza, Adamu, alikuwa “mwana wa Mungu.” (Luka 3:38) Hata hivyo, kwa kuwa Yesu alikuwa uumbaji wa kwanza wa Mungu na yule pekee ambaye aliumbwa moja kwa moja na Mungu, Biblia inamfafanua Yesu kuwa Mwana wa pekee zaidi wa Mungu.

 Je, Yesu aliishi mbinguni kabla ya kuzaliwa duniani?

 Ndiyo. Yesu alikuwa kiumbe wa roho mbinguni kabla ya kuzaliwa akiwa mwanadamu duniani. Yesu mwenyewe alisema hivi: “[Nimeshuka] kutoka mbinguni.”—Yohana 6:38; 8:23.

 Mungu alimuumba Yesu kabla ya kuumba kitu kingine chochote. Biblia inasema hivi kumhusu Yesu:

  •   “Yeye ndiye . . . mzaliwa wa kwanza wa viumbe vyote.”—Wakolosai 1:15.

  •   Yeye ndiye “mwanzo wa uumbaji wa Mungu.”—Ufunuo 3:14.

 Yesu alitimiza unabii kumhusu yule “ambaye asili yake ni ya tangu nyakati za kale, tangu siku za zamani za kale.”—Mika 5:2; Mathayo 2:4-6.

 Yesu alifanya kazi gani kabla ya kuja duniani?

 Alikuwa na cheo cha juu mbinguni. Yesu alizungumzia cheo hicho aliposali hivi: “Sasa Baba, nitukuze . . . kwa utukufu niliokuwa nao kando yako kabla ya ulimwengu kuwako.”—Yohana 17:5.

 Alimsaidia Baba yake kuumba vitu vingine vyote. Yesu alifanya kazi kando ya Mungu akiwa “mfanyakazi stadi.” (Methali 8:30) Kulingana na Yesu, Biblia inasema: “Kwa sababu kupitia kwake vitu vingine vyote viliumbwa mbinguni na duniani.”—Wakolosai 1:16.

 Mungu alimtumia Yesu kutokeza vitu vingine vyote. Uumbaji huo ulitia ndani viumbe wengine wote wa roho, kutia na ulimwengu halisi. (Ufunuo 5:11) Kwa njia fulani, ushirikiano huo kati ya Mungu na Yesu ulikuwa kama wa msanifu-ujenzi anayefanya kazi na mjenzi. Msanifu-ujenzi anabuni kitu; mjenzi anajenga kilichochorwa.

 Alikuwa Neno. Biblia inamwita Yesu “Neno” inapozungumza kuhusu maisha yake kabla ya kuwa mwanadamu. (Yohana 1:1) Ni wazi hilo linamaanisha kwamba Mungu alimtumia Mwana wake kuwajulisha viumbe wengine wa roho habari na maagizo Yake.

 Pia inaonekana kwamba Yesu alikuwa Msemaji wa Mungu kwa wanadamu duniani. Inawezekana kwamba Mungu alizungumza kupitia Yesu akiwa Neno alipowapa Adamu na Hawa maagizo katika bustani ya Edeni. (Mwanzo 2:16, 17) Huenda Yesu ndiye malaika aliyewaongoza Waisraeli wa kale walipokuwa jangwani na ambaye Waisraeli walipaswa kutii sauti yake.—Kutoka 23:20-23. a

a Neno hakuwa malaika pekee ambaye Mungu alimtumia kuwasilisha ujumbe. Kwa mfano, aliwatumia malaika wengine mbali na Mwana wake mzaliwa wa kwanza, kuwapa Waisraeli wa kale Sheria yake.—Matendo 7:53; Wagalatia 3:19; Waebrania 2:2, 3.