Hamia kwenye habari

Je, Mungu Atanisamehe?

Je, Mungu Atanisamehe?

Jibu la Biblia

 Ndiyo, Mungu atakusamehe dhambi zako ikiwa utachukua hatua zinazofaa. Biblia inasema kwamba Mungu yuko “tayari kusamehe” na kwamba “atasamehe kwa njia kubwa.” (Nehemia 9:​17; Zaburi 86:5; Isaya 55:7) Anapotusamehe yeye hufanya hivyo kikamili. Dhambi zetu ‘hufutwa.’ (Matendo 3:​19) Pia, Mungu husamehe kabisa, kwa kuwa anasema hivi: “Dhambi yao sitaikumbuka tena.” (Yeremia 31:34) Anaposamehe, hakumbuki dhambi zetu ili atushtaki au kutuadhibu tena na tena.

 Hata hivyo, msamaha wa Mungu si udhaifu wala hauongozwi na hisia tu. Hapuuzi kamwe viwango vyake vya uadilifu. Kwa sababu hiyo, yeye hukataa kusamehe dhambi fulani.​—Yoshua 24:19, 20.

Hatua za kupata msamaha wa Mungu

  1.   Kubali kwamba dhambi yako imevunja viwango vya Mungu. Ingawa wengine wanaweza kuwa wameumizwa na jambo ulilofanya, unapaswa kwanza kutambua kwamba dhambi yako ni kosa dhidi ya Mungu.​—Zaburi 51:​1, 4; Matendo 24:16.

  2.   Ungama kwa Mungu kwa kutoa sala.​—Zaburi 32:5; 1 Yohana 1:9.

  3.   Onyesha kwamba unahuzunika kikweli kwa sababu ya dhambi yako. Kuonyesha “huzuni kwa njia ya kimungu” hutokeza toba, au kunamfanya mtu abadili mawazo yake. (2 Wakorintho 7:10) Kunatia ndani kujuta kwa sababu ya kuchukua hatua zilizomwongoza mtu kufanya dhambi.​—Mathayo 5:​27, 28.

  4.   Badili mwenendo wako, yaani, ‘geuka.’ (Matendo 3:​19) Hilo linamaanisha kwamba usirudie tendo ulilofanya au zoea ulilokuwa nalo, au linaweza kumaanisha kwamba ubadili njia yako ya kufikiri na kutenda.​—Waefeso 4:​23, 24.

  5.   Chukua hatua za kurekebisha ubaya au kurekebisha madhara yaliyofanywa. (Mathayo 5:​23, 24; 2 Wakorintho 7:​11) Waombe msamaha watu walioumizwa kwa sababu ya jambo ulilofanya au ulilokosa kufanya, na ujaribu kulipa fidia kwa kadiri unayoweza.​—Luka 19:​7-​10.

  6.   Toa sala umwombe Mungu msamaha kwa msingi wa dhabihu ya fidia ya Yesu. (Waefeso 1:7) Ili sala yako ijibiwe, unapaswa kuwasamehe wale ambao wamekutendea dhambi.​—Mathayo 6:​14, 15.

  7.   Ikiwa umetenda dhambi nzito, zungumza na mtu ambaye anastahili kukupa msaada wa kiroho unaohitaji na ambaye anaweza kusali kwa niaba yako.​—Yakobo 5:​14-​16.

Maoni yasiyofaa kuhusu kupata msamaha wa Mungu

 “Nimefanya dhambi nyingi sana siwezi kusamehewa.”

Mungu alimsamehe Daudi alipofanya uzinzi na kuua

 Maadamu tunachukua hatua ambazo Mungu ameonyesha katika Biblia, tutasamehewa, kwa kuwa uwezo wake wa kusamehe ni mkubwa kuliko dhambi zetu. Anaweza kusamehe dhambi nzito sana kutia ndani zile ambazo zimerudiwa mara nyingi sana.​—Isaya 1:​18.

 Kwa mfano, Mfalme Daudi wa Israeli alisamehewa alipofanya uzinzi na kuua. (2 Samweli 12:​7-​13) Mtume Paulo, ambaye alihisi kuwa yeye ndiye mtenda-dhambi mbaya zaidi, alisamehewa pia. (1 Timotheo 1:​15, 16) Hata Wayahudi wa karne ya kwanza ambao Mungu aliwashutumu kwa kumuua Yesu, aliyekuwa Masihi, wangeweza kusamehewa ikiwa wangebadili njia zao.​—Matendo 3:​15, 19.

 “Nikiungama mbele ya kasisi au kiongozi wa dini, dhambi zangu zitafutwa.”

 Hakuna mwanadamu leo aliye na mamlaka ya kumsamehe mtu ambaye amemtendea Mungu dhambi. Ingawa kuungama mbele ya mtu mwingine kunaweza kumsaidia mtenda-dhambi ajihisi vizuri, ni Mungu tu anayeweza kusamehe dhambi.​—Waefeso 4:​32; 1 Yohana 1:​7, 9.

 Ikiwa ndivyo, Yesu alimaanisha nini alipowaambia mitume wake hivi: “Mkisamehe dhambi za watu wowote, watakuwa wamesamehewa; msiposamehe zile za watu wowote, watakuwa hawajasamehewa”? (Yohana 20:23) Alikuwa akifafanua mamlaka ya pekee ambayo angewapa mitume baada ya wao kupokea roho takatifu.​—Yohana 20:22.

 Kama ilivyoahidiwa, mitume walipokea zawadi hiyo wakati ambapo roho takatifu ilimiminwa juu yao katika 33 W.K. (Matendo 2:​1-4) Mtume Petro alitumia mamlaka hiyo alipowahukumu Anania na Safira. Petro alijua kimuujiza kuhusu njama yao ya uwongo, na hukumu yake ilionyesha kwamba dhambi yao haingesamehewa.​—Matendo 5:​1-​11.

 Zawadi hiyo waliyopata kimuujiza kupitia roho takatifu, ilikoma baada ya kifo cha mitume, kama tu ilivyokuwa kwa zawadi nyingine kama vile uwezo wa kuponya na kusema kwa lugha. (1 Wakorintho 13:8-10) Kwa hiyo, leo hakuna mwanadamu anayeweza kufuta dhambi ya mwingine.