Hamia kwenye habari

MSAADA KWA AJILI YA FAMILIA | KULEA WATOTO

Mtoto Anapotaka Kujiua

Mtoto Anapotaka Kujiua

 Katika miaka ya hivi karibuni, idadi ya vijana wanaojiua imeongezeka sana katika nchi mbalimbali. Kwa nini hali imekuwa hivyo? Je, mtoto wako ana mawazo ya kujiua?

Katika makala hii

 Kwa nini ni muhimu kwa wazazi kuwa makini kuhusu suala la watoto kujiua?

 Kutoka mwaka wa 2009 hadi mwaka wa 2019, kulikuwa na ongezeko la asilimia 40 katika idadi ya wanafunzi wa sekondari waliokuwa na dalili za kushuka moyo (sonona), nchini Marekani. Katika kipindi hicho hicho idadi ya watu waliojiua iliongezeka pia. a

 “Changamoto ambazo vijana wa kizazi hiki wanakabili hazina kifani . . . Changamoto hizo zimesababisha madhara makubwa kwa afya yao ya kiakili.”​—Vivek H. Murthy, U.S. Surgeon General.

 Kanuni ya Biblia: “Roho iliyopondeka humfyonza mtu nguvu.”​—Methali 17:22.

 Unawezaje kujua ikiwa mtoto wako anafikiria kujiua?

 Fikiria mambo yafuatayo.

  •   Matukio. Je, mtoto wako amekabiliana na jambo fulani lenye kuhuzunisha kama vile kukataliwa, urafiki kuvunjika, kushindwa kutimiza jambo fulani, au kifo cha mpendwa? Ikiwa ndivyo, je, huenda jambo hilo linamwathiri b kwa njia kubwa zaidi kuliko unavyofikiri?

  •   Tabia. Je, mtoto wako ameacha kushirikiana na marafiki na watu wa familia au je, amepoteza hamu ya kufanya mambo ambayo alifurahia kufanya? Je, amegawa vitu ambavyo alivipenda sana?

  •   Maneno. Je, mtoto wako huzungumza kuhusu kifo au kusema mambo kama vile, “Afadhali ningekuwa nimekufa”? Je, yeye husema kwamba hangependa kuwa mzigo kwako?

     Ni kweli huenda mambo mengine ambayo mtoto anasema yakawa tu “mazungumzo ya ovyoovyo.” (Ayubu 6:3) Hata hivyo, huenda mambo mengine yakawa kilio cha kuomba msaada. Kwa hiyo, usipuuze jambo lolote ambalo mtoto wako anasema kuhusu kutamani kufa.

 Ikiwa mtoto wako anakwambia kwamba amewahi kufikiria kujiua, unaweza kumuuliza, “Ulifikiria ungejiua lini na ungetumia njia gani?” Jibu atakalokupa litakusaidia kupima hali ni mbaya kadiri gani.

 “Tukiwa wazazi, wakati mwingine tunasita kuwauliza watoto wetu maswali kwa sababu tunaogopa majibu ambayo watatupa. Hata hivyo, ikiwa mambo wanayosema ni yaleyale wanayohisi, basi si ni afadhali tuyajue?”​—Sandra.

 Kanuni ya Biblia: “Mashauri ya moyoni ni kama kilindi; lakini mtu mwenye ufahamu atayateka.”​—Mithali 20:5, Union Version.

 Utafanyaje ikiwa mtoto wako anafikiria kujiua?

  •   Kwa subira jitahidi kujua mawazo na hisia za mtoto wako. Kwanza kabisa, mshukuru kwa kukueleza mambo kwa unyoofu. Kisha unaweza kumwambia: “Ningependa kuelewa mambo ambayo umekuwa ukipitia na jinsi ambavyo umekuwa ukihisi. Niambie mambo yanaendaje? Vilevile unaweza kusema, “Unaweza kunieleza unavyohisi na jinsi hali inavyokuwa unapopata mawazo hayo?”

     Sikiliza kwa makini mtoto wako anapojibu. Usiseme jambo lolote ambalo linaweza kutoa wazo la kwamba unapuuza hisia au mahangaiko yake wala usimpe “suluhisho” haraka-haraka.

     Kanuni ya Biblia: “[Uwe] mwepesi wa kusikia, si mwepesi wa kusema, si mwepesi wa hasira.”​—Yakobo 1:19.

  •   Fanya mipango ya kulinda usalama wa mtoto wako. Msaidie mtoto wako kutambua mambo yafuatayo na kuyaandika:

     Dalili za kuzingatia. Kabla ya kupata mawazo ya kujiua, kwa kawaida mtoto wako anakuwa akifanya mambo gani au kufikiria kuhusu nini?

     Mambo yanayosaidia. Ni mambo gani anayofanya yanayomsaidia kupunguza mkazo na kubadili fikira?

     Watu wanaoweza kusaidia. Je, mtoto wako ana watu wanaoweza kumsaidia anapohitaji msaada? Watu hao wanatia ndani wewe, mtu mwingine ambaye mnamwamini, mtaalamu wa afya ya akili, au shirika lenye uzoefu wa kuwasaidia watu walio na mawazo ya kujiua.

    Fanya mipango ya kulinda usalama wa mtoto wako

     Kanuni ya Biblia: “Mipango ya wenye bidii hakika huleta mafanikio.”​—Methali 21:5.

  •   Endelea kuwa makini. Endelea kupima hali na kuwa mwangalifu hata mtoto wako anapoonekana kwamba anaendelea vizuri.

     “Mwanangu aliponiambia kwamba hakuwa tena na mawazo ya kujiua, nilifikiri kwamba tatizo lake lilikuwa limekwisha. Nilikuwa nimekosea sana. Mtu anaweza kukabili tatizo fulani ghafula na akaanza tena kuwa na mawazo ya kujiua.”​—Daniel.

     Msaidie tineja wako aelewe jambo fulani muhimu kuhusu hisia: Ni za muda tu, zinabadilika-badilika. Kitabu The Whole-Brain Child, kinasema hivi: “Hisia ni kama hali ya hewa. Kihalisi mvua hunyesha, na lingekuwa jambo la kipumbavu kusimama kwenye mvua na kujidanganya haipo. Lakini lingekuwa jambo la kipumbavu pia kufikiri kwamba jua halitawahi kuwaka tena.”

  •   Mhakikishie mtoto wako kwamba unampenda: Mwambie mtoto wako kwamba unampenda na anaweza kuwa na uhakika kwamba utakuwa pamoja naye na utamsaidia. Unaweza pia kumwambia, “Nitafanya kila kitu ninachoweza ili kukusaidia kuvumilia hali hii.”

     Kanuni ya Biblia: “Rafiki wa kweli hupenda nyakati zote naye ni ndugu ambaye amezaliwa kwa ajili ya nyakati za taabu.”​—Methali 17:17.

a Watu wengi ambao wana ugonjwa wa kushuka moyo au sonona hawajiui. Hata hivyo, idadi kubwa ya watu waliojiua walikuwa na ugonjwa huo walipojiua.

b Kanuni ambazo zimezungumziwa katika makala hii zinaweza kuwasaidia watoto wa kike na wa kiume pia.