Hamia kwenye habari

BIBLIA INABADILI MAISHA

“Nilikuwa Nikijichimbia Kaburi”

“Nilikuwa Nikijichimbia Kaburi”
  • Alizaliwa: 1978

  • Nchi: El Salvador

  • Historia: Mshiriki wa Genge Lenye Ukatili

MAISHA YANGU YA ZAMANI

 Nilishangaa mtu aliponiambia: “Ikiwa kweli unataka kujifunza kumhusu Mungu, shikamana na Mashahidi wa Yehova.” Wakati huo nilikuwa nimejifunza na Mashahidi wa Yehova kwa muda mfupi tu. Lakini ili uelewe kwa nini nilishangaa, acha nikueleze kifupi kuhusu maisha yangu.

 Nilizaliwa Quezaltepeque, mji fulani nchini El Salvador. Nilizaliwa nikiwa mtoto wa 6 katika familia yenye watoto 15. Wazazi walijaribu kunilea niwe mtu mnyoofu anayetii sheria. Pia, Leonardo na Mashahidi wengine wa Yehova walikuja mara kwa mara kutufundisha Biblia. Lakini nilipuuza mambo niliyofundishwa na kufanya uamuzi mmoja mbaya baada ya mwingine. Nilipokuwa na umri wa miaka 14, nilianza kunywa kileo na kutumia dawa za kulevya nikiwa na marafiki wangu shuleni. Marafiki hao waliacha shule mmoja baada ya mwingine na kujiunga na genge, nami nikafuata mfano wao mbaya. Tuliishi mitaani, tukiwalazimisha watu watupe pesa na kuiba ili kuendeleza mazoea yetu mabaya.

 Genge likawa familia yangu. Niliamini kwamba nilipaswa kuwa mshikamanifu kwao. Kwa mfano, siku moja mwanagenge akiwa amelewa dawa za kulevya alimshambulia jirani yangu. Jirani yangu alifaulu kumdhibiti na kuwaita polisi. Nikiwa nimekasirika, nilianza kuvunja-vunja gari lake ili kumshinikiza amwachilie rafiki yangu. Jirani yangu alinisihi niache kufanya hivyo, lakini sikumsikiliza, badala yake, nilivunja dirisha moja baada ya lingine, na kuharibu gari lake.

 Nilipokuwa na umri wa miaka 18, washiriki wa genge langu walipigana na polisi. Nilipotaka kuwarushia bomu lililotengenezwa nyumbani, lililipuka likiwa mkononi mwangu kwa njia ambayo sijawahi kuelewa. Nakumbuka tu nikiona mkono wangu ukiwa umevunjika​—kisha nikapoteza fahamu. Nilipopata fahamu nilikuwa hospitalini, na nikagundua kwamba nilikuwa nimepoteza mkono wangu wa kulia, sikio langu la kulia halingeweza kusikia, na jicho la kulia lilikuwa karibu kupofuka.

 Hata hivyo, licha ya majeraha yangu, nilirudi kwenye genge baada ya kutoka hospitalini. Lakini muda mfupi baadaye polisi walinikamata na nikafungwa gerezani. Nikiwa huko, uhusiano wangu na washiriki wengine wa genge uliimarika. Tulishinda pamoja tukifanya mambo yote pamoja​—kuanzia wakati wa kiamsha-kinywa tulipovuta msokoto wa kwanza wa bangi, hadi tulipolala.

JINSI BIBLIA ILIVYOBADILI MAISHA YANGU

 Nilipokuwa gerezani, Leonardo alinitembelea. Tulipokuwa tukizungumza, alielekeza kidole kwenye chale iliyokuwa imechanjwa kwenye mkono wangu wa kulia. Akaniuliza, “Je, unajua alama hizo tatu zinamaanisha nini?” Nikamwambia, “Bila shaka, zinamaanisha ngono, dawa za kulevya, na muziki wa rock and roll.” Lakini Leonardo alijibu hivi: “Kwa maoni yangu zinamaanisha hospitali, gereza, na kifo. Umekuwa hospitalini, na sasa uko gerezani. Unajua kinachofuata.”

 Maneno ya Leonardo yalinishtua. Hakuwa amekosea. Nilikuwa nikijichimbia kaburi kupitia mtindo wangu wa maisha. Leonardo alinialika nijifunze naye Biblia, nami nikakubali. Mambo niliyojifunza katika Biblia yalinichochea kubadili maisha yangu. Kwa mfano, Biblia inasema kwamba “kushirikiana na watu wabaya hupotosha maadili.” (1 Wakorintho 15:33, maelezo ya chini) Hivyo, jambo la kwanza nililohitaji kufanya ni kutafuta marafiki wapya. Ili kufanya hivyo, niliacha kuhudhuria mikutano ya genge na nikaanza kuhudhuria mikutano ya Mashahidi wa Yehova iliyofanyiwa hapo gerezani. Kwenye mkutano wa Mashahidi, nilikutana na mfungwa anayeitwa Andrés, ambaye alibatizwa na kuwa Shahidi wa Yehova hapo gerezani. Alinialika kunywa kiamsha-kinywa pamoja naye. Baada ya hapo, sikuanza tena siku kwa kuvuta bangi. Badala yake, mimi na Andrés tulizungumzia mstari wa Biblia kila asubuhi.

 Mara moja, washiriki wengine wa genge waligundua kwamba nimeanza kubadilika. Kwa sababu hiyo, kiongozi mmoja wa genge letu aliniambia kwamba anahitaji kuongea nami. Niliogopa sana. Sikujua angenifanya nini atakapojua nia yangu, kwa sababu haiwezekani kwa mtu kuacha genge. Aliniambia: “Tumeona kwamba umeacha kuhudhuria mikutano yetu na umeanza kuhudhuria mikutano ya Mashahidi wa Yehova. Unapanga kufanya nini?” Nilimwambia kwamba nilitaka kuendelea kujifunza Biblia na kubadili maisha yangu. Nilishangaa aliponiambia kwamba genge litaniheshimu ikiwa tu nitathibitisha kwamba kweli ninataka kuwa Shahidi wa Yehova. Kisha akasema: “Ikiwa kweli unataka kujifunza kumhusu Mungu, shikamana na Mashahidi wa Yehova. Tunatarajia uache kufanya mambo mabaya. Ninakupongeza sana. Umefanya uamuzi mzuri. Mashahidi wanaweza kweli kukusaidia. Nilijifunza nao nilipokuwa Marekani, na watu fulani katika familia yangu ni Mashahidi wa Yehova. Usiogope. Tia bidii.” Ingawa bado nilikuwa na woga, nilijihisi nikiwa na furaha sana. Nilimshukuru Yehova Mungu moyoni. Nilihisi kama ndege aliyeachiliwa kutoka kwenye mtego wake, na nikaelewa maneno haya ya Yesu: “Mtaijua kweli, nayo kweli itawaweka ninyi huru.”​—Yohana 8:​32.

 Hata hivyo, baadhi ya marafiki wangu wa zamani walinijaribu kwa kunipa dawa za kulevya. Lazima nikiri kwamba pindi fulani, nilishindwa na vishawishi vyao. Lakini baada ya muda, na baada ya kutoa sala nyingi, mwishowe niliacha mazoea yangu mabaya.​—Zaburi 51:10, 11.

 Baada ya kuachiliwa, watu wengi waliamini kwamba ningerudia maisha yangu ya zamani, lakini sikufanya hivyo. Badala yake, nilirudi gerezani mara nyingi ili kuwaonyesha wafungwa wengine mambo niliyojifunza kutoka kwa Biblia. Mwishowe, marafiki wangu wa zamani waliamini kwamba nilikuwa nimebadilika. Lakini inasikitisha kwamba maadui wangu wa zamani hawakujua jambo hilo.

 Siku moja nilipokuwa nikihubiri, mimi na mwandamani wangu tulizingirwa na washiriki wenye silaha wa genge pinzani ambao walitaka kuniua. Mwandamani wangu aliwaeleza kwa upole lakini kwa ujasiri kwamba sikuwa mshiriki wa genge sasa. Mimi nilijitahidi kubaki mtulivu. Baada ya kunipiga na kunionya nisirudi tena katika eneo hilo, wanaume hao walishusha silaha zao na kuturuhusu tuondoke. Kwa kweli Biblia ilikuwa imebadili maisha yangu. Zamani ningejaribu kulipiza kisasi. Lakini sasa ninatii shauri la Biblia katika 1 Wathesalonike 5:​15: “Hakikisheni hakuna yeyote anayelipa ubaya kwa ubaya, bali sikuzote mwendelee kutendeana mema kati yenu na kwa wengine wote.”

 Baada ya kuwa Shahidi wa Yehova, nimejitahidi kuwa mnyoofu. Haijawa rahisi. Lakini kwa msaada wa Yehova Mungu, mashauri ya Biblia, na kuungwa mkono na marafiki wangu wapya, nimefaulu. Sitaki kamwe kurudia mazoea yangu ya zamani.​—2 Petro 2:​22.

JINSI AMBAVYO NIMEFAIDIKA

 Nilikuwa mkatili na mwenye hasira kali. Ninaamini kwamba nisingekuwa hai ikiwa ningeendelea kuishi maisha hayo ya jeuri. Nilichojifunza katika Biblia kilinibadili. Niliacha mazoea yangu mabaya. Nimejifunza kushughulika kwa amani na maadui wangu wa zamani. (Luka 6:​27) Sasa nina marafiki ambao wananisaidia kusitawisha sifa nzuri. (Methali 13:20) Ninaishi maisha yenye furaha na kusudi, nikimtumikia Mungu ambaye yuko tayari kusamehe maovu yote niliyofanya.​—Isaya 1:​18.

 Mwaka wa 2006, nilihudhuria shule ya mazoezi ya pekee kwa ajili ya waeneza-injili waseja. Miaka kadhaa baadaye, nilimwoa mke wangu mrembo, na sasa tunashirikiana kumlea binti yetu. Sasa ninatumia wakati mwingi kuwafundisha wengine kuhusu kanuni za Biblia zilizonisaidia. Pia, ninatumikia nikiwa mzee katika kutaniko letu, na ninajaribu kuwasaidia vijana kuepuka makosa niliyoyafanya nilipokuwa na umri kama wao. Sasa badala ya kujichimbia kaburi, ninajitahidi kupata wakati ujao wa milele ambao Mungu anaahidi katika Biblia.