Hamia kwenye habari

BIBLIA INABADILI MAISHA

“Nilikuwa Mwenye Hasira na Jeuri”

“Nilikuwa Mwenye Hasira na Jeuri”
  • Alizaliwa: 1975

  • Nchi: Mexico

  • Historia: Hasira na jeuri; mfungwa

MAISHA YANGU YA ZAMANI

 Nilizaliwa San Juan Chancalaito, mji mdogo katika jimbo la Chiapas, Mexico. Familia yangu ilitokana na kikundi cha Wamaya kinachoitwa Chol. Wazazi wangu walikuwa na watoto 12, nami nilikuwa wa tano. Nilipokuwa mtoto, mimi na ndugu zangu tulijifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova. Inasikitisha kwamba sikutumia ushauri wa Biblia nilipokuwa mdogo.

 Kufikia wakati nilipokuwa na umri wa miaka 13, nilikuwa nikitumia dawa za kulevya na kuiba. Nilitoka nyumbani wakati huo na nikaanza kurandaranda. Nilipokuwa na umri wa miaka 16, nilianza kufanya kazi katika shamba la bangi. Nilifanya kazi hapo kwa mwaka mmoja hivi kisha usiku mmoja tulipokuwa tukisafirisha bangi nyingi sana, watu wa kikundi pinzani cha kusafirisha dawa za kulevya waliokuwa na silaha nyingi walitushambulia. Niliokoka kupigwa risasi kwa kupiga mbizi mtoni na kutokea eneo la mbali kwenye mto huo. Baada ya hapo, nilitorokea nchi ya Marekani.

 Huko Marekani, niliendelea kuwa mlanguzi wa dawa za kulevya na nikaingia mashakani. Nilipokuwa na umri wa miaka 19, nilikamatwa na kufungwa gerezani kwa sababu ya wizi na kujaribu kuua. Nikiwa gerezani, nilijiunga na genge na nikahusika katika matendo mengine ya jeuri. Kwa sababu hiyo, wenye mamlaka walinihamishia kwenye gereza lenye ulinzi mkali la Lewisburg, Pennsylvania.

 Kwenye gereza la Lewisburg, mwenendo wangu ukawa mbaya hata zaidi. Kwa kuwa nilikuwa na alama za chale za genge, nilijiunga na genge hilohilo kwenye gereza hilo jipya. Nikawa mkatili hata zaidi, kila wakati nilikuwa nikipigana. Pindi moja nilihusika katika vita kati yetu na genge lingine kwenye uwanja wa gereza. Tulipigana vikali tukitumia magongo ya besiboli na vyuma vya kutanua misuli. Ili kututenganisha, walinzi walitumia gesi za kutoa machozi. Baada ya hapo, niliwekwa kwenye kitengo cha usimamizi wa pekee cha wafungwa hatari. Nilikuwa na hasira kali na niliwatukana watu. Ilikuwa rahisi kwangu kuwapiga watu. Kwa kweli, nilifurahia kuwapiga wengine. Sikujutia hata kidogo mwenendo wangu.

JINSI BIBLIA ILIVYOBADILI MAISHA YANGU

 Katika kitengo hicho cha usimamizi wa pekee, niliruhusiwa kutoka nje kwa muda mfupi tu kila siku, hivyo nikaanza kusoma Biblia ili kupitisha muda. Baadaye, mlinzi alinipa kitabu Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani. a Niliposoma kitabu hicho cha kujifunzia Biblia, nilikumbuka mambo mengi niliyojifunza nilipokuwa mtoto nilipojifunza Biblia na Mashahidi. Baada ya hapo, nilianza kufikiria jinsi maisha yangu yalivyokuwa yameharibika kwa sababu ya utu wangu wenye jeuri. Pia, niliifikiria familia yetu. Kwa kuwa dada zangu wawili walikuwa Mashahidi wa Yehova, nilijiambia, ‘Wao wataishi milele.’ Kisha nikajiuliza, ‘Kwa nini mimi pia nisiweze kuishi milele?’ Hapo ndipo nilipoazimia kabisa kubadilika.

 Hata hivyo, nilijua kwamba nilihitaji kupata msaada ili nibadilike. Kwa hiyo, kwanza, nilimsihi Yehova Mungu anisaidie. Kisha, nikaiandikia barua ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova nchini Marekani na kuomba funzo la Biblia. Ofisi ya tawi ilifanya mipango ili kutaniko la karibu liwasiliane nami. Wakati huo sikuruhusiwa kutembelewa na wageni ambao si washiriki wa familia, hivyo Shahidi kutoka kutaniko hilo alianza kuniandikia barua zenye kutia moyo na machapisho ya Biblia, jambo ambalo liliongeza tamaa yangu ya kubadilika.

 Nilipiga hatua kubwa nilipoamua kutoka kwenye genge nililoshirikiana nalo kwa miaka mingi. Kiongozi wa genge hilo pia alikuwa kwenye kitengo hicho cha usimamizi wa pekee, hivyo siku moja wakati wa mapumziko nilimfikia na kumwambia kwamba nilitaka kuwa Shahidi wa Yehova. Nilishangaa aliponiambia: “Ikiwa umeazimia kufanya hivyo, ni sawa. Siwezi kupingana na Mungu. Lakini ikiwa unajaribu tu kutoka kwenye genge, unajua matokeo.”

 Kwa miaka miwili iliyofuata, wafanyakazi wa gereza waliona jinsi utu wangu ulivyobadilika. Kwa sababu hiyo, walinitendea kwa fadhili zaidi. Kwa mfano, waliacha kunifunga pingu waliponisindikiza kwenda kuoga. Mlinzi mmoja alinifikia na kunitia moyo niendelee kufanya mabadiliko. Wenye mamlaka hata walinihamisha kwenye gereza lisilo na ulinzi mkali lililokuwa karibu na gereza kuu nilipotumikia mwaka wangu wa mwisho gerezani. Mwaka wa 2004, baada ya kufungwa kwa miaka kumi, niliachiliwa na kurudishwa Mexico kwa basi la gereza.

 Muda mfupi baada ya kufika Mexico, nilitafuta Jumba la Ufalme la Mashahidi wa Yehova. Nilihudhuria mkutano wa kwanza nikiwa na nguo za gerezani, hizo ndizo nguo nzuri peke yake nilizokuwa nazo. Licha ya jinsi nilivyoonekana, Mashahidi walinikaribisha kwa uchangamfu. Nilipoona jinsi walivyonitendea kwa fadhili, nilihisi kwamba nilikuwa kati ya Wakristo wa kweli. (Yoh 13:35) Baada ya mkutano, wazee wa kutaniko walipanga nianze kujifunza Biblia rasmi. Nilibatizwa na kuwa Shahidi wa Yehova mwaka mmoja baadaye, Septemba 3, 2005.

 Januari 2007, nilianza kutumika nikiwa mhudumu wa wakati wote, nikitumia saa 70 kila mwezi kuwafundisha wengine Biblia. Mnamo 2011, nilihitimu kutoka Shule ya Biblia ya Ndugu Waseja (sasa inaitwa Shule ya Waeneza-Injili wa Ufalme). Shule hiyo imenisaidia sana kutimiza majukumu yangu kutanikoni.

Sasa ninafurahia kuwafundisha wengine wafanye amani

 Mwaka wa 2013, nilifunga ndoa na mke wangu mpendwa, Pilar. Anasema kwamba haamini mambo ninayomwambia kuhusu maisha yangu ya zamani. Sijawahi kurudia mazoea yangu ya zamani. Mimi na mke wangu tunaamini kwamba utu wangu wa sasa umetokezwa na nguvu za Biblia za kubadili maisha.​—Waroma 12:2.

JINSI AMBAVYO NIMEFAIDIKA

 Ninahisi kwamba maneno ya Yesu katika Luka 19:10 yananihusu. Alisema hivi: “[Nilikuja] kutafuta na kuokoa kilichopotea.” Sasa sijihisi tena kama mtu aliyepotea, wala siwaumizi watu tena. Kwa sababu ya Biblia, sasa ninafurahia kuwa na kusudi bora maishani, kushughulika na wengine kwa amani na jambo muhimu hata zaidi, nina uhusiano mzuri na Muumba wangu, Yehova.

[MAELEZO YA CHINI]

a Kitabu hicho kilichapishwa na Mashahidi wa Yehova lakini sasa hakichapishwi tena. Sasa kitabu kikuu kinachotumiwa kujifunzia Biblia ni Biblia Inatufundisha Nini?