Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

BIBLIA INABADILI MAISHA

Nilitembea na Bunduki Kila Wakati

Nilitembea na Bunduki Kila Wakati
  • ALIZALIWA: 1958

  • NCHI: ITALY

  • HISTORIA: MSHIRIKI WA GENGE HATARI LA WAHALIFU

MAISHA YANGU YA ZAMANI:

Nilizaliwa na kulelewa katika jiji la Roma, katika eneo la wafanyakazi maskini. Maisha yalikuwa magumu. Sikumjua mama yangu, na sikuwa na uhusiano mzuri na baba yangu. Tangu utotoni nilijifunza kuishi katika mazingira magumu.

Nilipokuwa na umri wa miaka kumi tu, tayari nilikuwa nimeanza kuiba. Nikiwa na umri wa miaka 12, nilitoroka nyumbani kwa mara ya kwanza. Zaidi ya mara moja, baba yangu alilazimika kuja kunichukua kwenye makao makuu ya polisi ili kunirudisha nyumbani. Nilibishana na watu mara nyingi—nilikuwa mjeuri na mwenye hasira kali. Nilipokuwa na umri wa miaka 14, nilitoroka nyumbani kabisa. Nilianza kutumia dawa za kulevya na kuishi mtaani. Sikuwa na mahali pa kulala, mara nyingine niliingia ndani ya gari la mtu na kukaa ndani hadi alfajiri. Kisha ningetafuta mahali penye maji ili nioge.

Nilikuwa mwizi hodari—niliiba mikoba ya watu na pia kwenye nyumba za watu usiku. Nikawa na sifa mbaya na punde nikaalikwa kujiunga na genge hatari, ambalo lilinipa “fursa” ya kuiba kwenye benki. Kwa sababu ya ujeuri wangu, niliheshimiwa sana na washiriki wengine wa kundi hilo. Nilitembea na bunduki kila wakati, hata nililala nayo. Jeuri, madawa ya kulevya, wizi, matusi, na maadili mapotovu yalikuwa mambo ya kawaida kwangu. Nilitafutwa na polisi kila mara. Nilikamatwa na kufungwa mara nyingi.

JINSI BIBLIA ILIVYOBADILI MAISHA YANGU:

Pindi moja baada ya kutoka gerezani, niliamua kumtembelea dadake mama. Nilishangaa kwamba mama mdogo na watoto wake wawili walikuwa Mashahidi wa Yehova. Walinialika kuhudhuria mkutano wa Mashahidi. Kwa sababu nilitaka kuchunguza, niliandamana pamoja nao. Tulipofika kwenye Jumba la Ufalme, nilisisitiza nikae karibu na mlango ili nione wanaoingia na kutoka. Kama kawaida, nilikuwa na bunduki.

Mkutano huo ulibadili maisha yangu. Nilifikiri nilikuwa kwenye sayari nyingine. Nilisalimiwa na watu wenye uchangamfu na waliotabasamu kwa urafiki. Bado nakumbuka vizuri jinsi Mashahidi walivyoonekana kuwa wenye fadhili na unyoofu. Hali hiyo ilikuwa tofauti kabisa na maisha niliyozoea!

Nikaanza kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi. Kadiri nilivyozidi kujifunza, ndivyo nilivyotambua kwamba nilihitaji kubadili kabisa maisha yangu. Nilifuata ushauri wa maneno ya Methali 13:20: “Anayetembea na watu wenye hekima atakuwa na hekima, lakini anayeshirikiana na wajinga atapatwa na mabaya.” Niliona kwamba nilihitaji kujitenga na lile genge la wahalifu. Haikuwa rahisi kufanya hivyo, lakini kwa msaada wa Yehova, nilifanikiwa.

Kwa mara ya kwanza nikaanza kudhibiti matendo yangu

Pia, nilihitaji kufanya mabadiliko ya kimwili. Kwa jitihada nyingi nilifanikiwa kuacha kuvuta sigara na kutumia dawa za kulevya. Nilinyoa nywele zangu ndefu, nikaacha kuvaa hereni, na kuacha matusi. Kwa mara ya kwanza maishani nikaanza kudhibiti matendo yangu.

Sikupenda kusoma wala kujifunza, kwa hiyo ilikuwa vigumu kwangu kukaza fikira wakati wa kujifunza Biblia. Hata hivyo, nilipoendelea kujitahidi, nilianza kumpenda Yehova, na nikahisi mabadiliko fulani—dhamiri yangu ilianza kunichoma. Mara kwa mara nilijihisi vibaya na kudhani kwamba Yehova hangenisamehe kwa sababu ya maovu niliyofanya. Katika hali hiyo nilipata faraja kwa kusoma jinsi Yehova alivyomsamehe Mfalme Daudi baada ya kufanya dhambi nzito.—2 Samweli 11:1–12:13.

Changamoto nyingine ilikuwa kwenda kuhubiri nyumba kwa nyumba. (Mathayo 28:19, 20) Niliogopa kukutana na watu ambao huenda niliwaibia au kuwaumiza wakati uliopita! Lakini hatua kwa hatua nilishinda hofu yangu. Nilianza kupata furaha kwa kuwasaidia watu wajifunze kumhusu Baba yetu wa mbinguni, ambaye husamehe kwa njia kubwa.

JINSI AMBAVYO NIMEFAIDIKA:

Kujifunza kumhusu Yehova kuliokoa maisha yangu! Wengi kati ya rafiki zangu wa zamani wamekufa au wako gerezani, lakini mimi nina maisha yenye kuridhisha na tumaini zuri la wakati ujao. Nimejifunza kuwa mnyenyekevu na mtiifu na pia kudhibiti hasira yangu kali. Hivyo, ninafurahia uhusiano mzuri na watu. Sasa nimefunga ndoa, na mke wangu mrembo anaitwa Carmen. Mimi na mke wangu, tunapata shangwe kwa kuwasaidia watu wajifunze Biblia.

Jamani, sasa nafanya kazi ili nipate riziki—wakati mwingine mimi huenda kwenye benki kufanya kazi ya usafi, bali si kuiba!