Kulingana na Marko 4:1-41

  • MIFANO KUHUSU UFALME (1-34)

    • Mpandaji (1-9)

    • Kwa nini Yesu alitumia mifano? (10-12)

    • Mfano wa mpandaji wafafanuliwa (13-20)

    • Taa haiwekwi chini ya kikapu (21-23)

    • Kipimo unachopima (24, 25)

    • Mpandaji anayelala (26-29)

    • Mbegu ya haradali (30-32)

    • Kutumia mifano (33, 34)

  • Yesu atuliza dhoruba (35-41)

4  Yesu akaanza tena kufundisha kando ya bahari, na umati mkubwa sana ukakusanyika karibu naye. Basi akapanda ndani ya mashua na kuketi humo mbali kidogo na ufuo, lakini umati wote ulikuwa kando ya bahari, ufuoni.+  Naye akaanza kuwafundisha mambo mengi kwa mifano,+ na alipokuwa akifundisha akasema:+  “Sikilizeni. Tazama! Mpandaji alienda kupanda mbegu.+  Alipokuwa akipanda, mbegu fulani zikaanguka kando ya barabara, ndege wakaja na kuzila.  Nyingine zikaanguka kwenye miamba, mahali pasipo na udongo mwingi, na mara moja zikachipuka kwa sababu udongo haukuwa na kina.+  Lakini jua lilipochomoza, ziliungua na kunyauka kwa sababu hazikuwa na mizizi.  Mbegu nyingine zikaanguka kwenye miiba, nayo miiba ikakua na kuzisonga, nazo hazikuzaa matunda.+  Lakini nyingine zikaanguka kwenye udongo mzuri, nazo zikakua na kuongezeka, zikaanza kuzaa matunda, mara 30, 60, na 100 zaidi.”+  Kisha akaongezea kusema: “Yule aliye na masikio ya kusikiliza, na asikilize.”+ 10  Alipokuwa peke yake, wale waliokuwa karibu naye pamoja na wale 12 wakaanza kumuuliza kuhusu mifano hiyo.+ 11  Akawaambia: “Ninyi mmepewa siri takatifu+ ya Ufalme wa Mungu, lakini kwa wale walio nje mambo yote yako katika mifano,+ 12  ili, ingawa wanatazama, watazame lakini wasione, na ingawa wanasikia, wasikie lakini wasielewe; wala wasigeuke na kusamehewa.”+ 13  Tena akawaambia: “Ikiwa hamwelewi mfano huo, basi mtaelewaje mifano mingine yote? 14  “Mpandaji hupanda neno.+ 15  Basi, hawa ndio wale walio kando ya barabara ambapo neno hupandwa; lakini mara tu wanapolisikia, Shetani huja+ na kuliondoa neno lililopandwa ndani yao.+ 16  Vivyo hivyo, hawa ndio wale waliopandwa kwenye miamba; mara tu wanapolisikia neno, wanalikubali kwa shangwe.+ 17  Hata hivyo, hawana mizizi ndani yao, bali wanaendelea kwa muda fulani; kisha mara tu wanapopata taabu au mateso kwa sababu ya lile neno, wanakwazika. 18  Bado kuna wengine ambao wamepandwa kwenye miiba. Hawa ndio wale wanaolisikia neno,+ 19  lakini mahangaiko+ ya mfumo huu wa mambo* na nguvu za udanganyifu za utajiri+ na tamaa+ za mambo mengine yote huingia na kulisonga neno, nalo halizai matunda. 20  Mwishowe, wale waliopandwa kwenye udongo mzuri ni wale wanaolisikiliza neno na kulipokea vizuri na kuzaa matunda—mara 30, 60, au 100 zaidi.”+ 21  Akaendelea kuwaambia: “Je, taa huletwa na kuwekwa chini ya kikapu* au chini ya kitanda? Je, hailetwi na kuwekwa juu ya kinara cha taa?+ 22  Kwa maana hakuna jambo lolote lililofichwa ambalo halitafichuliwa; hakuna jambo lolote lililofunikwa kwa uangalifu ambalo halitafunuliwa.+ 23  Yeyote aliye na masikio ya kusikiliza, na asikilize.”+ 24  Tena akawaambia: “Sikilizeni kwa makini mambo mnayosikia.+ Kwa kipimo mnachopima, ndicho mtakachopimiwa, ndiyo, mtaongezewa hata zaidi. 25  Kwa maana aliye na kitu ataongezewa,+ lakini yule asiye na kitu, hata kile alicho nacho kitachukuliwa.”+ 26  Basi akaendelea kusema: “Kwa hiyo Ufalme wa Mungu ni kama vile mtu anapopanda mbegu kwenye udongo. 27  Yeye hulala usiku na kuamka mchana, nazo mbegu huota na kuwa ndefu—naye hajui jinsi zinavyokua. 28  Udongo wenyewe hutokeza mazao hatua kwa hatua, kwanza jani, kisha suke, mwishowe nafaka iliyokomaa ndani ya suke. 29  Lakini mimea inapokuwa tayari, yeye hutumia mundu, kwa sababu wakati wa kuvuna umefika.” 30  Akaendelea kusema: “Tutaufananisha Ufalme wa Mungu na nini, au tutatumia mfano gani kuufafanua? 31  Ni kama mbegu ya haradali, ambayo ilipopandwa katika udongo ilikuwa ndogo kuliko mbegu zote duniani.+ 32  Lakini baada ya kupandwa, humea na kuwa kubwa kuliko mboga nyingine zote na kutokeza matawi makubwa, hivi kwamba ndege wa angani hupata makao chini ya kivuli chake.” 33  Akitumia mifano+ mingi kama hiyo, aliwafundisha neno kwa kadiri walivyoweza kusikiliza. 34  Kwa kweli, hakuwa akizungumza nao bila mfano, lakini alipokuwa na wanafunzi wake faraghani aliwafafanulia mambo yote.+ 35  Ilipofika jioni siku hiyo, akawaambia wanafunzi wake: “Tuvuke twende ng’ambo ya bahari.”+ 36  Baada ya kuuaga umati, wakaenda pamoja na Yesu katika mashua, kama alivyokuwa, na kulikuwa na mashua nyinginezo pamoja naye.+ 37  Dhoruba kali ya upepo ikaanza kuvuma, mawimbi yakaipiga mashua, hivi kwamba ikakaribia kuzama.+ 38  Lakini Yesu alikuwa kwenye tezi, akiwa amelalia mto. Basi wakamwamsha na kumwambia: “Mwalimu, je, hujali kwamba tunakaribia kuangamia?” 39  Ndipo akasimama, akaukemea upepo na kuiambia bahari: “Nyamaza! Tulia!”+ Upepo ukakoma, kukawa shwari kabisa. 40  Basi akawauliza: “Kwa nini mnaogopa sana?* Je, bado hamna imani?” 41  Lakini wakaogopa sana, nao wakaulizana: “Kwa kweli, mtu huyu ni nani, hivi kwamba upepo na bahari vinamtii?”+

Maelezo ya Chini

Angalia Kamusi, “Mfumo wa mambo.”
Au “kikapu cha kupimia.”
Au “kwa nini mna hofu?”