Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jinsi Biblia Inavyoweza Kuwasaidia Wanaume Kukabiliana na Mahangaiko

Jinsi Biblia Inavyoweza Kuwasaidia Wanaume Kukabiliana na Mahangaiko

 Unapowazia mtu aliye na mahangaiko, a huenda ukafikiria kuhusu mtu mwenye wasiwasi mwingi, ambaye hawezi hata kuamka kutoka kitandani asubuhi, au mtu anayezungumzia sana matatizo anayokabili.

 Baadhi ya watu hutenda kwa njia hiyo wanapokabili mahangaiko. Lakini watafiti wamegundua kwamba watu wengine—hasa wanaume—hutenda kwa njia tofauti. Ripoti moja inasema kwamba kuna uwezekano mkubwa zaidi kwa wanaume “kutumia kileo na dawa za kulevya ili kukabiliana na mahangaiko, kwa hiyo kile ambacho kinaonekana kuwa tatizo la kunywa kupita kiasi kinaweza kuwa ishara ya kulemewa na mahangaiko. Na mara nyingi wanaume huonyesha wana mahangaiko kwa kuzungumza kwa hasira na kukasirika upesi.”

 Ni kweli kwamba wanaume hutenda kwa njia zinazotofautiana. Lakini vyovyote ambavyo mtu atashughulika na mahangaiko, ukweli ni kwamba limekuwa tatizo kubwa katika “nyakati [hizi] za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo.” (2 Timotheo 3:1) Ikiwa unakabiliana na mahangaiko, je, Biblia inaweza kukusaidia?

Ushauri wa Biblia Unaoweza Kukusaidia Kushughulika na Mahangaiko

 Biblia ina ushauri mwingi unaotegemeka ambao unaweza kutusaidia tunapokuwa na mahangaiko. Fikiria mifano mitatu.

  1.  1. “Msihangaike kamwe kuhusu kesho, kwa maana kesho itakuwa na mahangaiko yake yenyewe. Kila siku ina matatizo yake ya kutosha.”—Mathayo 6:34.

     Maana: Ni jambo la hekima kuepuka kuwa na wasiwasi kupita kiasi kuhusu mambo ambayo yanaweza kutokea (au yasitokee) wakati ujao. Mara nyingi, mambo tuliyokuwa na hofu kwamba yatatokea huwa hayatokei. Katika visa fulani, mambo hubadilika bila kutarajia na kuwa mazuri.

     Jaribu kufanya hivi: Jaribu kukumbuka pindi ambazo ulikuwa na uhakika kitu kibaya kingetokea—lakini hakikutokea. Kisha changanua wasiwasi ulio nao sasa hivi na ujaribu kupima kihalisi uwezekano wa mambo hayo kuwa matatizo makubwa.

  2.  2. “Kama chuma kinavyonoa chuma, ndivyo mtu anavyomnoa rafiki yake.”—Methali 27:17.

     Maana: Watu wengine wanaweza kutusaidia kushughulika na mahangaiko yetu—ikiwa tutawaruhusu. Wanaweza kutupa mapendekezo mazuri yanayotegemea hali walizokabiliana nazo maishani. Mbali na hilo, wanaweza kutusaidia kuona jambo linalotuhangaisha kwa njia tofauti.

     Jaribu kufanya hivi: Jiulize ni nani anayeweza kutoa ushauri mzuri, kama vile rafiki ambaye amewahi kukabiliana na tatizo kama unalokabiliana nalo. Muulize ni nini kilichomsaidia na ni nini ambacho hakikumsaidia.

  3.  3. “[Tupeni] mahangaiko yenu yote juu yake, kwa sababu yeye anawajali ninyi.”—1 Petro 5:7.

     Maana: Mungu anawajali sana wale wanaoteseka. Anatukaribisha tusali kwake kuhusu jambo lolote linalotuhangaisha au kutulemea.

     Jaribu kufanya hivi: Andika orodha ya mambo yanayokuhangaisha. Kisha sali kwa Mungu kuhusu mambo hayo, ukimweleza kila tatizo na kumwomba akusaidie kushughulika nalo.

Wakati Ambapo Mahangaiko Hayatakuwapo Tena

 Biblia ina habari nyingi kuliko ushauri tu wa kushughulika na mahangaiko. Inaahidi kwamba hivi karibuni sana wasiwasi tunaokabili leo utaondolewa milele. Hilo litawezekanaje?

 Ufalme wa Mungu utaondoa chanzo cha mahangaiko yetu. (Ufunuo 21:4) Kwa kweli, Ufalme huo utakapotawala, hata hatutakumbuka mahangaiko na mikazo tuliyokuwa nayo.—Isaya 65:17.

 Huo ndio wakati ujao ambao “Mungu anayetoa amani” anataka ufurahie. (Waroma 16:20) Anatuhakikishia hivi: “Ninajua vizuri mawazo ninayofikiria kuwaelekea ninyi, . . . mawazo ya amani, wala si ya msiba, ili niwape ninyi wakati ujao na tumaini.”—Yeremia 29:11.

a Katika makala hii, neno “mahangaiko” halirejelei tatizo kubwa la afya bali linarejelea mikazo na wasiwasi wa kila siku ambao watu hukabiliana nao. Wale ambao wanapambana na tatizo la afya wanaweza kuamua kutafuta msaada wa daktari.—Luka 5:31.