Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

HABARI KUU | MUNGU ANA MAONI GANI KUHUSU VITA?

Maoni ya Mungu Kuhusu Vita Leo

Maoni ya Mungu Kuhusu Vita Leo

Watu wengi leo wanakandamizwa. Wengi wao wanamwomba Mungu kila siku awasaidie na wanajiuliza ikiwa kweli atawasaidia. Je, Mungu anasikia vilio vyao vya kuomba msaada? Vipi kuhusu wale wanaopigana vita ili kuondoa ukandamizaji? Je, Mungu anaunga mkono jitihada zao na kuona vita vyao kuwa halali?

Har–Magedoni itakomesha vita vyote

Kwanza kabisa, utafarijika ukijua ukweli huu: Mungu anayaona mateso yote wanayokabili watu ulimwenguni na anapanga kuchukua hatua. (Zaburi 72:13, 14) Katika Neno lake, Biblia, Mungu ametoa ahadi kwamba wale wote ‘wanaopata dhiki, watapata kitulizo.’ Wakati gani? “Wakati wa ufunuo wa Bwana Yesu kutoka mbinguni pamoja na malaika zake wenye nguvu . . . anapoleta kisasi juu ya wale wasiomjua Mungu na wale wasiotii habari njema juu ya Bwana wetu Yesu.” (2 Wathesalonike 1:7, 8) Ufunuo huo wa Yesu utatimizwa wakati ujao unaoitwa na Biblia kuwa “vita vya ile siku kuu ya Mungu Mweza-Yote,” au Har–Magedoni.—Ufunuo 16:14, 16.

Katika vita hivyo vya wakati ujao, Mungu hatatumia wanadamu kupigana vita na waovu bali atamtumia Mwana wake, Yesu Kristo, pamoja na viumbe wa roho wenye nguvu. Jeshi hilo la mbinguni litakomesha ukandamizaji wote.—Isaya 11:4; Ufunuo 19:11-16.

Mpaka sasa, maoni ya Mungu kuhusu vita hayajabadilika. Bado anaona vita kuwa njia halali ya kukomesha ukandamizaji na uovu. Hata hivyo, kama historia inavyoonyesha, Mungu pekee ndiye mwenye haki ya kuamua wakati na wale watakaopigana vita. Kama tulivyoona, Mungu amepanga kwamba vita vya kukomesha uovu na kulipiza kisasi kwa wapinzani wake vipiganwe wakati ujao na Mwana wake, Yesu Kristo. Hilo linamaanisha kwamba Mungu haungi mkono vita vinavyoendelea duniani leo hata kama kuna sababu nzuri ya kupigana.

Kwa mfano: Fikiria watoto wawili wanaoanza kupigana baada ya baba yao kuondoka nyumbani. Wanaacha kupigana kwa muda mfupi na kumpigia simu baba yao. Mtoto mmoja analalamika kuwa mwenzake ndiye chanzo cha ugomvi na yule mwingine anadai kwamba ameonewa. Wote wawili wanapeleka malalamiko kwa baba yao na kila mmoja anatumaini ataungwa mkono. Hata hivyo, baada ya kuwasikiliza, baba yao anawaambia waache kupigana na wamsubiri arudi ili atatue tatizo hilo. Watoto hao wanasubiri kwa muda fulani. Lakini baada ya muda mfupi wanaanza kupigana tena. Baba yao anaporudi anawaadhibu wote wawili kwa sababu hawakutii.

Mara nyingi mataifa yanapopigana humwomba Mungu awasaidie. Lakini Mungu haungi mkono upande wowote wa mapigano hayo. Badala yake, katika Neno lake, Biblia, anaeleza waziwazi kwamba: “Msimlipe yeyote uovu kwa uovu,” na “Msijilipizie kisasi wenyewe.” (Waroma 12:17, 19) Zaidi ya hayo, ameonyesha kwamba wanadamu wanapaswa “kumngojea kwa kutamani” ili achukue hatua, naye atafanya hivyo katika vita vya Har–Magedoni. (Zaburi 37:7) Mungu hukasirika sana mataifa yanaposhindwa kumngojea na kuonyesha kimbelembele kwa kuamua kupigana. Hivyo, katika Har–Magedoni, Mungu ataonyesha hasira yake na kumaliza migogoro yote ya mataifa kwa ‘kukomesha vita mpaka kwenye mwisho wa dunia.’ (Zaburi 46:9; Isaya 34:2) Kwa kweli, vita vya Har–Magedoni vitakomesha vita vyote.

Kukomeshwa kwa vita ni mojawapo ya baraka nyingi za Ufalme wa Mungu. Alipokuwa akizungumzia serikali hiyo katika sala hii inayojulikana sana, Yesu alisema hivi: “Ufalme wako na uje. Mapenzi yako na yatendeke duniani kama ilivyo mbinguni.” (Mathayo 6:10) Ufalme wa Mungu hautakomesha vita tu, bali pia utakomesha chanzo cha vita yaani uovu. * (Zaburi 37:9, 10, 14, 15) Ndiyo sababu wafuasi wa Yesu walitazamia kwa hamu baraka za Ufalme wa Mungu.—2 Petro 3:13.

Hata hivyo, tutasubiri Ufalme wa Mungu kwa muda gani hadi utakapokuja kukomesha mateso, ukandamizaji, na uovu? Utimizo wa unabii mwingi wa Biblia unaonyesha kwamba tunaishi katika “siku za mwisho” za mfumo huu wa mambo. (2 Timotheo 3:1-5) * Hivi karibuni, Ufalme wa Mungu utakomesha siku hizi za mwisho kwa vita vya Har–Magedoni.

Kama ilivyotajwa mwanzoni, wale “wasiotii habari njema juu ya Bwana wetu Yesu” wataangamizwa katika vita hiyo ya mwisho. (2 Wathesalonike 1:8) Lakini kumbuka, Mungu hapendezwi na kifo cha mtu yeyote, kutia ndani waovu. (Ezekieli 33:11) Kwa kuwa “hataki yeyote aangamizwe” katika vita hiyo ya mwisho, anahakikisha kwamba habari njema kumhusu Bwana wetu Yesu ‘inahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa ili kuwa ushahidi kwa mataifa yote’ kabla ya mwisho kuja. (2 Petro 3:8, 9; Mathayo 24:14; 1 Timotheo 2:3, 4) Naam, kupitia kazi ya kuhubiri inayofanywa ulimwenguni pote na Mashahidi wa Yehova, watu wanapata fursa ya kumjua Mungu, kutii habari njema kumhusu Yesu, na kutarajia kuishi wakati ambapo vita havitakuwapo tena.

^ fu. 9 Ufalme wa Mungu utakomesha kifo ambacho ni adui ya wanadamu. Kama ilivyoelezwa katika makala “Majibu ya Maswali ya Biblia” ya toleo hili, Mungu atawafufua watu wengi, kutia ndani wale waliouawa kwa sababu ya vita.

^ fu. 10 Ili kupata habari zaidi kuhusu siku za mwisho, soma sura ya 9 ya kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.