Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Wajua?

Je, Wajua?

Kwa nini Yosefu alinyoa kabla ya kwenda kwa Farao?

Ukuta wa kale wa Misri ulio na mchoro wa kinyozi akiwa kazini

Kulingana na simulizi la kitabu cha Mwanzo, Farao aliagiza mfungwa Mwebrania aliyeitwa Yosefu apelekwe kwake haraka ili atafsiri ndoto zilizomsumbua sana. Kufikia wakati huo, Yosefu alikuwa amefungwa kwa miaka mingi. Licha ya kuitwa haraka, alitenga wakati wa kunyoa. (Mwanzo 39:20-23; 41:1, 14) Mwandishi wa simulizi hilo anapotaja jambo hili linaloonekana kuwa si muhimu, anaonyesha kwamba Yosefu alijua desturi za Wamisri.

Waebrania pamoja na watu wa mataifa mengine ya kale walikuwa na desturi ya kufuga ndevu. Tofauti na mataifa hayo, “Wamisri wa kale walikuwa watu pekee wa Mashariki waliokuwa na desturi ya kunyoa ndevu,” kinasema kitabu cha McClintock and Strong’s Cyclopedia of Biblical, Theological, and Ecclesiastical Literature.

Je, walinyoa ndevu tu? Gazeti la Biblical Archaeology Review linaeleza kwamba kulingana na desturi fulani za Misri mwanaume alipaswa kujitayarisha kumwona Farao kama ambavyo angejitayarisha kwenda hekaluni. Hivyo, inaonekana kwamba Yosefu alihitaji kunyoa nywele zote kichwani na sehemu nyingine za mwili.

Simulizi la kitabu cha Matendo linasema kwamba baba ya Timotheo alikuwa Mgiriki. Je, hilo linamaanisha alizaliwa Ugiriki?

Si lazima iwe hivyo. Katika maandishi yake yaliyoongozwa na roho ya Mungu, mara kadhaa mtume Paulo amewatofautisha Wayahudi na watu wa mataifa kwa kuwaita Wagiriki. (Waroma 1:16; 10:12) Sababu moja ya kuwaita hivyo ni kwamba lugha na utamaduni wa Wagiriki ulienea katika maeneo yote ambayo Paulo alihubiri.

Ni mambo gani yaliyomtambulisha mtu kuwa Mgiriki? Katika karne ya nne K.W.K., Isocrates, msemaji mwenye ufasaha kutoka Athene, alieleza kwa majivuno jinsi utamaduni wa Ugiriki ulivyosambaa duniani kote. Akitaja matokeo ya kusambaa huko alisema hivi: “Watu wameitwa Wagiriki kwa kuwa wamenufaika na elimu yetu, na si kwa sababu wamezaliwa Ugiriki.” Huenda Paulo alimwita hivyo baba ya Timotheo ambaye hakuwa Myahudi na watu wengine kwa kuwa walifuata utamaduni wa Wagiriki wala si kwa sababu walizaliwa Ugiriki.Matendo 16:1.