Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

BIBLIA INABADILI MAISHA

Nilivutiwa na Majibu ya Biblia Yaliyo Wazi na Yanayoeleweka

Nilivutiwa na Majibu ya Biblia Yaliyo Wazi na Yanayoeleweka
  • ALIZALIWA: 1948

  • NCHI: HUNGARIA

  • HISTORIA: NILITAMANI KUPATA MAJIBU YA MASWALI MUHIMU MAISHANI

MAISHA YANGU YA ZAMANI:

Nilizaliwa Székesfehérvár, nchini Hungaria, jiji la kihistoria ambalo limekuwepo kwa zaidi ya miaka 1,000. Lakini kwa kusikitisha, bado ninakumbuka madhara yaliyosababishwa na vita ya pili ya ulimwengu katika jiji hilo.

Nililelewa na babu na nyanya (bibi) yangu. Ninawakumbuka sana—hasa nyanya yangu Elisabeth. Alinisaidia kuwa na imani yenye nguvu katika Mungu. Tangu nilipokuwa na umri wa miaka mitatu, kila jioni tulisali pamoja ile Sala ya Bwana. Hata hivyo, sikuelewa maana ya sala hiyo hadi nilipofikisha umri wa zaidi ya miaka 20.

Babu na nyanya yangu walinitunza tangu nilipokuwa mchanga kwa sababu wazazi wangu walifanya kazi mchana na usiku, ili wapate pesa za kutosha kununua nyumba nzuri. Hata hivyo, kila Jumamosi ya pili ya mwezi familia nzima ilikutana ili kula pamoja. Nilifurahia sana pindi hizo za kuwa pamoja.

Mwaka 1958, tamaa ya wazazi wangu ilitimia; walinunua nyumba na tukaanza kuishi pamoja. Nilifurahi sana kuishi na wazazi wangu! Hata hivyo, miezi sita baadaye furaha yangu ilipotea ghafla. Baba yangu alikufa baada ya kuugua kansa.

Nilikata tamaa. Ninakumbuka sala niliyotoa: “Mungu, nilikuomba umwokoe baba yangu. Bado ninamhitaji. Kwa nini hukujibu sala zangu?” Nilitaka sana kujua baba yangu yuko wapi. Nilijiuliza hivi: ‘Je, ameenda mbinguni? Au ametoweka milele?’ Niliwaonea wivu watoto wengine waliokuwa na baba zao.

Kwa miaka mingi, nilienda makaburini karibu kila siku. Nilipiga magoti kando ya kaburi la baba yangu na kusali hivi: “Tafadhali, Mungu, nataka kujua mahali alipo baba yangu.” Pia nilimwomba anisaidie kujua kusudi la maisha.

Nilipokuwa na umri wa miaka 13, niliamua kujifunza Kijerumani. Nilifikiri kwamba kusoma vitabu vingi vya lugha hiyo, huenda kungenisaidia kupata majibu ya maswali yangu. Mwaka wa 1967, nilianza kujifunza lugha hiyo katika mji wa Jena, ambao ulikuwa sehemu ya Ujerumani Mashariki. Nilisoma kwa makini vitabu vya wanafalsafa wa Ujerumani, hasa vile vilivyoeleza kusudi la maisha ya mwanadamu. Ingawa nilipata hoja zenye kupendeza, lakini hakuna hata moja iliyoniridhisha. Niliendelea kusali ili nipate majibu.

JINSI BIBLIA ILIVYOBADILI MAISHA YANGU:

Mwaka wa 1970, nilirudi Hungaria ambako nilikutana na Rose ambaye baadaye tulioana. Wakati huo Hungaria ilikuwa chini ya utawala wa Wakomunisti. Muda mfupi baada ya kufunga ndoa tukakimbilia nchini Austria. Lengo letu lilikuwa kuhamia Sydney, nchini Australia ambako mjomba wangu aliishi.

Muda mfupi baadaye nikapata kazi nchini Austria. Siku moja, mfanyakazi mwenzangu aliniambia kwamba ningepata majibu ya maswali yangu yote katika Biblia. Alinipa vitabu kadhaa vilivyozungumzia Biblia. Nilivisoma vitabu hivyo haraka na nilikuwa na hamu ya kujua mengi zaidi. Kwa hiyo, niliwaandikia Mashahidi wa Yehova, wachapishaji wa vitabu hivyo ili kuomba machapisho zaidi.

Mwaka mmoja baada ya kufunga ndoa, tulitembelewa na Shahidi wa Yehova kijana mwenyeji wa Austria. Aliniletea machapisho niliyokuwa nimeomba na akajitolea kunifundisha Biblia, nami nikakubali. Kwa sababu nilikuwa na hamu ya kujifunza, tulijifunza mara mbili kwa juma—na tulitumia muda wa karibu saa nne kila wakati tulipojifunza!

Nilifurahia sana mambo niliyojifunza kutoka kwenye Biblia. Nilishangaa sana Mashahidi waliponionyesha jina la Mungu, Yehova, katika Biblia yangu ya Kihungaria. Kwa miaka 27 ambayo nilikuwa nikienda kanisani, sikuwahi kusikia jina la Mungu likitajwa hata siku moja! Nilivutiwa sana na jinsi Biblia ilivyojibu maswali yangu kwa njia iliyo wazi na inayoeleweka. Kwa mfano, nilijifunza kwamba wafu hawajui lolote, ni kana kwamba wako katika usingizi mzito. (Mhubiri 9:5, 10; Yohana 11:11-15) Pia nilijifunza kuhusu ahadi ya Biblia ya ulimwengu mpya ambao “kifo hakitakuwapo tena.” (Ufunuo 21:3, 4) Natumaini kumwona baba yangu tena, kwa sababu “kutakuwa na ufufuo” katika ulimwengu mpya.—Matendo 24:15.

Mke wangu Rose alijiunga nami katika kujifunza Biblia. Tulifanya maendeleo haraka, na tukamaliza kujifunza baada ya miezi miwili tu! Tulihudhuria mikutano yote ya Mashahidi wa Yehova. Tulivutiwa sana na upendo, ushirikiano, na umoja miongoni mwao.—Yohana 13:34, 35.

Mwaka wa 1976, mimi na Rose tuliruhusiwa kuingia nchini Australia. Mara moja tukawapata Mashahidi wa Yehova huko. Nao wakatukaribisha vizuri. Mwaka wa 1978, tulibatizwa na kuwa Mashahidi wa Yehova.

JINSI AMBAVYO NIMEFAIDIKA:

Hatimaye, nimepata majibu ya maswali yaliyonisumbua kwa muda mrefu sana. Kwa kumkaribia Yehova Mungu, pia nimempata Baba bora sana. (Yakobo 4:8) Ninatamani sana kumwona tena baba yangu mzazi katika ulimwengu mpya unaokuja.—Yohana 5:28, 29.

Mwaka wa 1989, tuliamua kurudi Hungaria ili tuwaeleze watu wa familia yetu, rafiki zetu, na wengine kuhusu imani yetu. Tumefurahia sana kuwafundisha Biblia watu wengi. Watu zaidi ya 70 kati yao, kutia ndani mama yangu mpendwa, wamejiunga nasi katika kumtumikia Yehova.

Nilisali kwa miaka 17 ili nipate majibu ya maswali yangu. Miaka mingine 39 imepita na bado ninasali, lakini sasa ninaweza kusema, “Asante, Baba yangu mpendwa wa mbinguni, kwa kujibu sala zangu za utotoni.”