Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

 HABARI KUU

Je, Wanadamu Wataiharibu Dunia Kabisa?

Je, Wanadamu Wataiharibu Dunia Kabisa?

“Kizazi kinaenda, kizazi kinakuja; lakini dunia inasimama mpaka wakati usio na kipimo.”—MFALME SULEMANI, KARNE YA 11 K.W.K. *

Mwandikaji huyo wa Biblia, alitambua tofauti kubwa kati ya maisha mafupi ya wanadamu na umilele wa dunia. Kwa kweli, kwa maelfu ya miaka, vizazi vimekuja na kwenda, na bado Dunia imedumu na kuendelea kutegemeza uhai—hadi leo.

Watu wameita miaka ya tangu Vita vya Pili vya Ulimwengu kuwa Kipindi cha Maendeleo Makubwa. Katika kipindi cha miaka 70 hivi baada ya vita hivyo, wanadamu wamefanya maendeleo makubwa katika usafiri, mawasiliano, na teknolojia, ambayo yameleta mabadiliko makubwa ya kiuchumi. Watu wengi wanaishi maisha ambayo zamani hayakuwaziwa. Wakati huohuo, idadi ya watu duniani imeongezeka karibu mara tatu.

Ingawa hivyo, maendeleo hayo yametokeza uharibifu. Inasemekana kwamba shughuli za wanadamu zinavuruga mifumo ya asili ya dunia. Kwa kweli, baadhi ya wanasayansi wanasema kwamba tumefikia kipindi ambacho wanadamu wanaharibu dunia kwa kiwango kikubwa sana.

Biblia ilitabiri kipindi ambacho wanadamu ‘wangeiharibu dunia.’ (Ufunuo 11:18) Watu wengine wanajiuliza ikiwa tunaishi katika kipindi hicho. Je, dunia itazidi kuharibiwa? Je, inawezekana kuzuia uharibifu huo? Je, wanadamu wataiharibu dunia kabisa?

 JE, INAWEZEKANA KUZUIA UHARIBIFU?

Je, dunia inaelekea kuharibiwa kabisa? Wanasayansi fulani wanafikiri ni vigumu kutabiri madhara ya uharibifu wa dunia. Kwa hiyo, wanahofu kwamba huenda tukafikia kipindi ambacho mabadiliko makubwa ya hali ya hewa yataleta uharibifu mkubwa.

Kwa mfano, fikiria kuhusu barafu kwenye eneo la magharibi ya Antaktika. Baadhi ya wataalamu wanasema kwamba kuna wakati ambapo haitawezekana kuzuia kuyeyuka kwa barafu katika eneo hilo. Hii ni kwa sababu barafu hiyo husaidia kuakisi miale ya jua. Lakini kadiri barafu inavyozidi kupungua, ndivyo bahari iliyo chini ya barafu ambayo haina uwezo mkubwa wa kuakisi inavyozidi kuonekana. Bahari hufyonza joto na kufanya barafu izidi kuyeyuka. Huenda hali hii ikashindwa kuzuilika. Kuongezeka kwa kiwango cha maji ya bahari kwa sababu ya kuyeyuka kwa barafu kunaweza kuleta maafa kwa watu wengi sana.

UHARIBIFU MKUBWA WA MAZINGIRA

Mipango mingi imefanywa ili kukabiliana na uharibifu wa mazingira. Mpango mmoja wa muda mrefu ni maendeleo-endelevu, yaani, maendeleo yasiyoharibu mazingira. Kumekuwa na matokeo gani?

Kwa kusikitisha, kama matatizo ya kushuka kwa uchumi duniani, matatizo ya mazingira yanazidi kuongezeka. Wanadamu wanaendelea kutumia kwa kasi sana rasilimali za dunia kuliko zinavyoweza kujizalisha. Nini kinachopaswa kufanywa? Mtaalamu mmoja wa mazingira alikiri hivi: “Kwa kweli, tumeshindwa kuitunza dunia yetu.” Maneno hayo yanathibitisha ukweli huu wa Biblia: “Mwanadamu anayetembea hana uwezo wa kuongoza hatua yake.”—Yeremia 10:23.

Kwa upande mwingine, Biblia inatuhakikishia kwamba Mungu, Muumba, hataruhusu wanadamu waangamize dunia. Zaburi 115:16, inasema hivi: “Dunia amewapa wana wa binadamu.” Ndiyo, sayari yetu ni “zawadi njema” kutoka kwa Baba yetu wa mbinguni. (Yakobo 1:17) Je, tunapaswa kufikiri kwamba zawadi kutoka kwa Mungu itakuwa ya muda mfupi tu, kana kwamba ina  tarehe ya mwisho wa matumizi yake? La hasha! Tunasema hivyo kwa sababu ya jinsi sayari yetu ilivyoumbwa kwa ustadi mwingi.

MAKUSUDI YA MUUMBA

Kitabu cha Biblia cha Mwanzo kinatuambia kwa kina jinsi Mungu alivyoitengeneza dunia yetu. Mwanzoni, dunia “ilikuwa bila umbo, na ukiwa, na giza lilikuwa juu ya uso wa kilindi cha maji.” Ona kwamba “maji” yanatajwa kwa sababu ni muhimu kwa uhai duniani. (Mwanzo 1:2) Kisha Mungu akasema: “Kuwe na nuru.” (Mwanzo 1:3) Bila shaka, miale ya jua ilipenya angani, na mwanga ukaanza kuonekana duniani. Baada ya hapo dunia ilitenganishwa na bahari. (Mwanzo 1:9, 10) Baadaye “majani, mimea inayozaa mbegu na miti inayozaa matunda” ikatokea. (Mwanzo 1:12) Hivyo kukawa na mambo yaliyohitajika ili kutegemeza mifumo muhimu kwa uhai kama vile usanidi-mwanga. Kwa nini Mungu alifanya matayarisho hayo yote?

Nabii Isaya alimfafanua Mungu kuwa “Mfanyizaji wa dunia na Mtengenezaji wake, Yeye aliyeifanya imara, ambaye hakuiumba tu bila sababu, ambaye aliiumba ili ikaliwe na watu.” (Isaya 45:18) Kwa kweli, Mungu anakusudia wanadamu waishi duniani milele.

Kwa kusikitisha, wanadamu wametumia vibaya zawadi kutoka kwa Mungu. Hata hivyo, kusudi la Mungu halijabadilika. Mtu mmoja aliyeishi zamani alisema: “Mungu si mwanadamu kwamba aseme uwongo, wala si mwana wa binadamu kwamba ajute. Je, yeye mwenyewe amelisema naye hatalitenda?” (Hesabu 23:19) Mungu hataacha dunia iharibiwe kabisa, hivi karibuni ‘atawaharibu wale wanaoiharibu dunia.’—Ufunuo 11:18.

DUNIA MAKAO YETU YA MILELE

Katika Mahubiri ya Mlimani, Yesu Kristo alisema hivi: “Wenye furaha ni wale walio na tabia-pole, kwa kuwa watairithi dunia.” (Mathayo 5:5) Baadaye katika mahubiri hayohayo, Yesu alieleza jinsi dunia itakavyokombolewa ili isiharibiwe. Aliwaambia wafuasi wake wasali hivi: “Ufalme wako na uje. Mapenzi yako na yatendeke duniani  kama ilivyo mbinguni.” Naam, Ufalme au serikali ya Mungu, itatimiza kusudi la Mungu kwa ajili ya dunia.—Mathayo 6:10.

Kuhusu mabadiliko makubwa yatakayoletwa na Ufalme, Mungu anasema hivi: “Tazama! Ninafanya vitu vyote kuwa vipya.” (Ufunuo 21:5) Je, inamaanisha kwamba Mungu ataumba dunia nyingine mpya? Hapana, kwa sababu tatizo si dunia yenyewe. Badala yake, Mungu atawaondoa wale wanaoleta matatizo duniani, “wale wanaoiharibu dunia,” yaani, mifumo na serikali za wanadamu wanaotawala leo. Mahali pake patachukuliwa na “mbingu mpya na dunia mpya”—serikali mpya ya mbinguni, Ufalme wa Mungu, utakaotawala wanadamu watakaoishi duniani.—Ufunuo 21:1.

Mungu atarekebisha uharibifu uliosababishwa na wanadamu, ataondoa madhara ya kimazingira. Kuhusu yale atakayofanya Mungu, mtunga-zaburi aliandika hivi: “Umeielekezea dunia fikira zako, ili uipatie wingi; unaitajirisha sana.” Kwa vile kutakuwa na hali nzuri ya hewa, na jambo muhimu zaidi baraka za Mungu, dunia itakuwa paradiso yenye kuzaa chakula kingi.—Zaburi 65:9-13.

Pyarelal aliyekuwa mwandishi wa Mohandas Gandhi, kiongozi wa zamani wa India, aliandika kwamba kiongozi huyo alisema: “Dunia ina vitu vingi vya kumtosha kila mtu lakini si kumtosha kila mwenye pupa.” Ufalme wa Mungu utaondoa chanzo cha matatizo mengi ya dunia kwa kubadili mioyo ya watu. Nabii Isaya alitabiri kwamba chini ya utawala wa Ufalme, watu “hawatasababisha madhara yoyote wala kusababisha uharibifu wowote” kwa mmoja na mwenzake na kwa dunia. (Isaya 11:9) Kwa kweli, mamilioni ya watu leo wenye utamaduni mbalimbali wanajifunza kuhusu viwango vya Mungu. Wanafundishwa kumpenda Mungu na jirani, kuwa wenye shukrani, kutunza mazingira, kutumia rasilimali vizuri, na kuishi kupatana na kusudi la Muumba. Wanatayarishwa kuishi katika dunia itakayokuwa paradiso.—Mhubiri 12:13; Mathayo 22:37-39; Wakolosai 3:15.

Kwa kweli, Mungu hataruhusu dunia hii nzuri iangamizwe

Simulizi la uumbaji katika kitabu cha Mwanzo linakamilika kwa maneno haya: “Mungu akaona kila kitu alichokuwa amefanya na, tazama! kilikuwa chema sana.” (Mwanzo 1:31) Kwa kweli, Mungu hataruhusu dunia hii nzuri iangamizwe. Tunafarijika kujua kwamba wakati ujao wa sayari yetu uko salama mikononi mwa Muumba mwenye upendo, Yehova Mungu. Anaahidi hivi: “Waadilifu wenyewe wataimiliki dunia, nao watakaa milele juu yake.” (Zaburi 37:29) Na uwe miongoni mwa “waadilifu,” watakaokaa duniani milele.

^ fu. 3 Andiko la Mhubiri 1:4 katika Biblia.