Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

 SIMULIZI LA MAISHA

Nina Nguvu Ingawa Mimi Ni Dhaifu

Nina Nguvu Ingawa Mimi Ni Dhaifu

Nikiwa nimekaa kwenye kiti cha magurudumu, mtu anayeona mwili wangu dhaifu wenye kilo 29 tu, hawezi kufikiri nina nguvu. Lakini kadiri mwili wangu unavyozidi kuwa dhaifu ndivyo ninavyopata nguvu za kuvumilia. Ngoja nieleze jinsi nilivyo na nguvu ingawa mimi ni dhaifu.

Akiwa na umri wa miaka minne

Niliishi na wazazi wangu kwenye nyumba ndogo kusini mwa Ufaransa na maisha yangu ya utotoni yalikuwa yenye furaha. Baba yangu alinitengenezea bembea ya kuchezea na pia nilipenda sana kukimbia-kimbia kwenye bustani. Mashahidi wa Yehova walitutembelea mnamo mwaka 1966, na walizungumza kwa muda mrefu pamoja na baba yangu. Miezi saba baadaye baba aliamua kuwa Shahidi wa Yehova. Mama yangu naye akawa Shahidi wa Yehova muda mfupi baadaye, hivyo nililelewa kwenye familia yenye furaha.

Matatizo yangu yalianza mara tu familia yetu iliporudi Hispania ambako wazazi wangu walikuwa wametoka. Nilianza kuhisi maumivu makali kwenye mikono na kwenye vifundo vya miguu. Baada ya kutembelea madaktari wengi kwa miaka miwili, hatimaye tulimpata daktari bingwa ambaye alisema kwa huzuni: “Hakuna tunachoweza kufanya.” Mama yangu alilia sana aliposikia maneno hayo. Siku hiyo nilisikia maneno ya ajabu kama vile “hitilafu ya kudumu ya kinga” na “baridi-yabisi ya utotoni.” * Nilikuwa na miaka kumi tu kwa hiyo sikuelewa vizuri maana ya maneno hayo, lakini nilitambua kwamba kilichokuwa kinazungumziwa hakikuwa kizuri.

Daktari alishauri nipate matibabu kwenye hospitali ya watoto. Nilifadhaika nilipofika hospitalini. Kulikuwa na sheria kali, watawa waliofanya kazi hapo walikata nywele zangu na kunivisha sare za wagonjwa. Nilijiuliza hivi kwa huzuni: ‘Nitaishije hapa?’

YEHOVA AANZA KUWA HALISI KWANGU

Wazazi wangu walinifundisha kumtumikia Yehova, kwa hiyo nilikataa kushiriki ibada ya Kikatoliki hospitalini. Lakini watawa hawakuelewa imani yangu. Nilimwomba Yehova asiniache, kisha nikahisi ananilinda na kunifariji, kama vile baba anavyomkumbatia mtoto wake kwa shauku.

Wazazi wangu waliruhusiwa kunitembelea siku  za Jumamosi. Waliniletea machapisho ya Biblia niyasome ili nijenge imani yangu. Watoto hawakuruhusiwa kuwa na vitabu, lakini watawa waliniruhusu kuwa navyo pamoja na Biblia ambayo niliisoma kila siku. Niliongea na wasichana wenzangu kuhusu tumaini la kuishi milele katika Paradiso duniani wakati ambapo hakutakuwa na magonjwa. (Ufunuo 21:3, 4) Ingawa nyakati nyingine nilihisi huzuni na upweke, nilifurahi kwamba imani yangu ilizidi kuimarika na niliendelea kumtegemea Yehova.

Baada ya miezi sita, madaktari waliniruhusu kurudi nyumbani. Ingawa bado nilikuwa mgonjwa nilifurahi kuwa pamoja na wazazi wangu. Viungio vyangu vilizidi kulemaa na nikawa na maumivu zaidi. Nilikuwa mnyonge sana nilipoanza kuvunja ungo. Hata hivyo nilibatizwa nikiwa na umri wa miaka 14, na nikaazimia kumtumikia Baba yangu wa mbinguni kwa uwezo wangu wote. Lakini mara nyingi nilivunjika moyo. Nilisali hivi: “Mungu, kwa nini mimi? Tafadhali niponye, huoni ninavyoteseka?”

Miaka ya kubalehe ilikuwa migumu sana kwangu. Ilibidi nikubali kwamba sitapona. Nilijilinganisha na rafiki zangu ambao walikuwa na afya nzuri na walionekana kuwa na furaha. Nilijihisi kuwa duni, na nikaacha kushirikiana na wengine. Hata hivyo familia na rafiki zangu waliendelea kunitegemeza. Ninamkumbuka vizuri Alicia aliyekuwa amenizidi miaka 20 na ambaye alikuwa rafiki wa kweli. Alinisaidia kuzingatia mambo mengine badala ya ugonjwa wangu na kushirikiana na watu badala ya kuwazia tu matatizo yangu.

NATAFUTA JINSI YA KUFANYA MAISHA YANGU YAWE NA KUSUDI

Nilipokuwa na umri wa miaka 18, afya yangu ilitetereka sana, hata nilihisi uchovu mwingi baada ya kuhudhuria mikutano. Licha ya hilo, nilitumia muda niliokaa nyumbani kusoma Biblia kwa makini. Vitabu vya Ayubu na Zaburi vilinisaidia kuelewa kwamba Yehova Mungu anahangaikia zaidi hali yetu ya kiroho kuliko ya kimwili. Niliposali nilipata “nguvu zinazopita zile za kawaida” na “amani ya Mungu yenye ubora unaozidi fikira zote.”2 Wakorintho 4:7; Wafilipi 4:6, 7.

Nilipokuwa na umri wa miaka 22, ilibidi nikubali kwamba nitatumia kiti cha magurudumu miaka yangu yote. Niliogopa kwamba badala ya kuniona watu wangeona tu kiti cha magurudumu kikiwa kimekaliwa na mwanamke mlemavu. Hata hivyo kiti hicho kilinifanya nijihisi huru zaidi, laana hiyo ikabadilika kuwa baraka. Rafiki yangu mmoja anayeitwa Isabel alinishauri nijiwekee lengo la kuhubiri pamoja naye saa 60 kwa mwezi mmoja.

Mwanzoni nilihisi jambo hilo halingewezekana. Lakini nilifaulu kwa sababu nilisali kwa Yehova na kutegemezwa na marafiki na watu wa familia. Mwezi huo ulipita haraka, na nilishinda woga na haya. Nilifurahia sana hivi kwamba niliamua kuwa painia wa kawaida kuanzia mwaka 1996—nikihubiri kwa saa 70 kila mwezi. Huo ulikuwa uamuzi mzuri sana, nilimkaribia Yehova hata zaidi na nikawa na nguvu zaidi za kimwili. Kazi ya kuhubiri iliniwezesha kuongea na wengine kuhusu imani yangu na hata kusaidia wengine wajenge urafiki na Mungu.

YEHOVA ANAENDELEA KUNITEGEMEZA

Katika mwaka 2001, nilipata aksidenti mbaya ya gari na nikavunjika miguu yote miwili. Nilipokuwa nimelazwa hospitalini nikiwa na maumivu makali sana, nilisali kimya-kimya nikisema: “Yehova, tafadhali usiniache!” Papo hapo, mwanamke aliyekuwa karibu nami aliniuliza: “Wewe ni Shahidi wa Yehova?” Sikuwa na nguvu za kujibu, kwa hiyo niliitikia kwa kichwa tu. Akasema: “Ninawajua ninyi. Mimi husoma magazeti yenu.” Maneno hayo yalinifariji sana. Hata katika hali hiyo ya kuhuzunisha bado nilitoa ushahidi kumhusu Yehova. Lilikuwa pendeleo kubwa!

Nilipopata nafuu kidogo niliamua kuhubiri zaidi. Mama yangu alinisukuma kwenye wodi ya hospitali nikiwa kwenye kiti cha magurudumu, miguu ikiwa imefungwa plasta. Kila siku tulitembelea wagonjwa kadhaa, tukawajulia hali na kuwaachia machapisho ya Biblia. Nilichoka sana, lakini Yehova alinisaidia.

Nikiwa na wazazi wangu, mwaka wa 2003

 Hivi karibuni maumivu yangu yamezidi kuongezeka na kifo cha baba yangu kimenihuzunisha sana. Lakini bado najitahidi kuwa na mtazamo mzuri. Jinsi gani? Najitahidi kuwa pamoja na marafiki na watu wa familia, na hilo hunisaidia kutofikiria matatizo yangu. Ninapokuwa peke yangu huwa nasoma, najifunza Biblia, au kuhubiri kupitia simu.

Mara nyingi najiwazia nikiwa katika ulimwengu mpya ambao Mungu ameahidi

Najitahidi kufurahia mambo ya kawaida kama vile upepo mwanana au manukato ya maua. Vitu hivyo hunipa sababu ya kuwa na shukrani. Ucheshi pia hunisaidia. Siku moja nilikuwa nikihubiri pamoja na rafiki yangu aliyekuwa akinisukuma kwenye kiti cha magurudumu, aliposimama ili aandike kitu fulani. Ghafula kiti kilianza kuteremka kwa kasi na nikagonga gari lililokuwa limesimama. Tulishtuka lakini tulipoona hakuna jambo lolote baya limetokea tulicheka sana.

Kuna vitu vingi ambavyo siwezi kufanya sasa. Ni tamaa nitakazotosheleza wakati ujao. Mara nyingi najiwazia nikiwa katika ulimwengu mpya ambao Mungu ameahidi. (2 Petro 3:13) Najiwazia nikiwa na afya nzuri, nikitembea huku na huku na kufurahia maisha kikamili. Nachochewa na maneno haya ya Mfalme Daudi: “Mtumaini Yehova; uwe hodari na moyo wako uwe na nguvu.” (Zaburi 27:14) Ingawa mwili wangu unazidi kuwa dhaifu, Yehova ananipa nguvu. Naendelea kupata nguvu ingawa mimi ni dhaifu.

^ fu. 6 Baridi yabisi ya utotoni ni ugonjwa wa mifupa na viungio unaoathiri watoto. Badala ya kulinda mwili, mfumo wa kinga unashambulia na kuharibu tishu mwilini, na hivyo kusababisha maumivu na uvimbe kwenye viungio.