Hamia kwenye habari

Biblia Inasema Nini Kuhusu Ista?

Biblia Inasema Nini Kuhusu Ista?

Jibu la Biblia

 Sherehe ya Ista haiungwi mkono na Biblia. Ukichunguza historia, utaona maana halisi ya Ista—ni desturi inayotegemea maadhimisho ya kale ya kusheherekea uwezo wa kuzaa. Fikiria mambo yafuatayo.

  1.   Jina: Kitabu Encyclopædia Britannica kinasema hivi: “Chanzo cha jina la Kiingereza Easter hakijulikani; katika karne ya nane, kasisi Mjerumani, Venerable Bede, alitoa jina hilo kutoka kwa mungu wa kike wa Wajerumani wa majira ya masika aliyeitwa Eostre.” Vitabu vingine vinahusianisha jina hilo na Astarte, mungu wa kike wa uzazi wa Wafoinike ambaye anajulikana kama Ishtari kwa Wababiloni.

  2.   Sungura: Mnyama huyo ni ishara ya uwezo wa kuzaa “iliyokuwa ikitumiwa zamani katika sherehe za wapagani wakati wa majira ya masika huko Ulaya na Mashariki ya Kati.”​—Encyclopædia Britannica.

  3.   Mayai: Kulingana na kamusi Funk & Wagnalls Standard Dictionary of Folklore, Mythology and Legend, kutafuta mayai ya Ista ambayo inasemekana kuwa yaliletwa na sungura wa Ista, “si mchezo wa watoto tu, bali ni masalio ya sherehe za kale za uwezo wa kuzaa.” Watu wa tamaduni fulani huamini kwamba yai la Ista lililopakwa rangi “lina nguvu za kimuujiza za kuleta furaha, ufanisi, afya, na ulinzi.”—Traditional Festivals.

  4.   Mavazi mapya ya Ista: “Ilionwa kuwa kukosa adabu na hivyo bahati mbaya kumsalimu mungu wa kike wa Skandinavia wa Majira ya Masika, au Eastre, ikiwa mtu hakuwa amevalia nguo mpya.”—The Giant Book of Superstitions.

  5.   Maombi ya kucha kwa jua: Yamehusianishwa na sherehe za waabudu wa kale wa jua “zilizofanywa mwanzoni mwa majira ya masika ili kulikaribisha jua na uwezo wake mkubwa wa kuvipa uhai tena vitu vyote vilivyokuwa vikikua.”—Celebrations—The Complete Book of American Holidays.

  Kitabu The American Book of Days kinaeleza vizuri chanzo cha Ista kinaposema: “Hakuna shaka kwamba Kanisa katika siku za mapema lilichukua desturi za zamani za kipagani na kuziingiza katika Ukristo.”

 Biblia inaonya kuhusu kumwabudu Mungu kwa kufuata mapokeo au desturi ambazo zinamchukiza. (Marko 7:6-8) Barua ya Pili kwa Wakorintho 6:17 inasema hivi: “‘Mjitenge,’ asema Yehova, ‘na mwache kugusa kitu kilicho najisi.’” Ista ni sikukuu ya kipagani na wote wanaotaka kumpendeza Mungu wataiepuka.