Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kutangaza Neno la Mungu Katika Hispania ya Enzi za Kati

Kutangaza Neno la Mungu Katika Hispania ya Enzi za Kati

“Nitakapokuwa nimeenda Uhispania, natumaini, zaidi ya yote, nitakapokuwa safarini kwenda huko, niwaangalie ninyi kidogo nanyi mnisindikize kidogo kwenda huko baada ya mimi kutosheka kwa kiasi fulani na ushirika wenu.”Waroma 15:24.

MTUME Paulo aliwaandikia Wakristo wenzake huko Roma maneno hayo karibu mwaka wa 56 W.K. Haijulikani ikiwa hatimaye Paulo alisafiri kwenda Hispania kwa sababu Biblia haisemi. Vyovyote vile, kupitia jitihada za Paulo na wamishonari wengine Wakristo, habari njema za Neno la Mungu, Biblia, zilifika Hispania kufikia karne ya pili W.K.

Punde si punde, vikundi vya Wakristo vilianza kusitawi huko Hispania. Hilo likafanya kuwe na uhitaji wa kutafsiri Biblia katika Kilatini kwa ajili ya wakaaji wa Hispania. Hii ni kwa sababu kufikia karne ya pili, Hispania ilikuwa imetawaliwa na Waroma kwa muda mrefu na Kilatini kilizungumzwa kotekote katika Milki kubwa ya Roma.

BIBLIA YATAFSIRIWA KATIKA KILATINI

Wakristo wa mapema huko Hispania walitokeza tafsiri kadhaa za Kilatini ambazo kwa ujumla zilijulikana kama Vetus Latina Hispana. Biblia hizo za Kilatini zilisambazwa huko Hispania kwa miaka mingi kabla ya Jerome kukamilisha tafsiri yake ya Kilatini inayojulikana kama Vulgate, mapema katika karne ya tano W.K.

Tafsiri ya Jerome, ambayo aliikamilishia huko Bethlehem, Palestine, ilifika Hispania haraka sana. Wakati Lucinius, mwanafunzi stadi wa Biblia, aliposikia kwamba Jerome alikuwa akitafsiri Biblia katika Kilatini, alitaka kupata nakala ya tafsiri hiyo mara moja. Aliwatuma waandishi sita kwenda Bethlehem kunakili maandishi hayo na kuyaleta Hispania. Katika karne zilizofuata, pole kwa pole tafsiri ya Vulgate ikachukua mahali pa Vetus Latina Hispana. Tafsiri hizi za Kilatini ziliwawezesha watu wa Hispania kusoma Biblia na kuelewa ujumbe wake. Lakini Milki ya Roma ilipoanguka, kukawa na uhitaji wa kutafsiri Biblia katika lugha nyingine.

BIBLIA ZILIZOANDIKWA KWENYE MABAMBA

Katika karne ya tano, Wavisigoth na makabila mengine ya Wajerumani yalivamia Hispania, na lugha mpya, Kigothi, ikafika Hispania. Wavamizi hao walikuwa wafuasi wa Arius, Wakristo ambao walipinga fundisho la Utatu. Pia, walikuja na tafsiri yao iliyoitwa Ulfilas, yaani, Biblia ya Kigothi. Biblia hiyo ilisomwa huko Hispania mpaka mwishoni mwa karne ya sita, wakati Reccared, mfalme wa Wavisigoth, alipoacha kuwa mfuasi wa Arius na kuwa Mkatoliki. Mfalme huyo aliagiza vitabu vyote ya wafuasi wa Arius vikusanywe na kuharibiwa, kutia ndani Biblia ya Ulfilas. Hivyo, maandishi yote ya Kigothi yakatoweka huko Hispania.

Bamba lenye maandishi ya Biblia katika lahaja ya Kilatini, karne ya sita W.K.

Hata hivyo, Neno la Mungu liliendelea kusambazwa huko Hispania. Mbali na Kigothi, kulikuwa na lahaja ya Kilatini iliyozungumzwa huko Hispania, ambayo baadaye ilitokeza lugha za Kiroma zilizozungumzwa kwenye Rasi ya Iberia. * Maandishi  ya kale zaidi ya lahaja hiyo ya Kilatini yanajulikana kama mabamba ya Wavisigoth, kwa sababu yaliandikwa kwenye mabamba. Yaliandikwa mnamo karne ya sita na ya saba, na baadhi yake yana sehemu za kitabu cha Zaburi na Vitabu vya Injili. Bamba moja lina sura nzima ya Zaburi 16.

Kuwepo kwa Maandiko kwenye mabamba kunaonyesha kwamba wakati huo watu wa kawaida walisoma na kunakili Neno la Mungu. Inaonekana kwamba walimu walitumia maandishi hayo ya Biblia kuwafundisha watoto kusoma na kuandika. Mabamba hayo yalikuwa ya bei ya chini yakilinganishwa na vitabu vya ngozi vilivyotumiwa kwenye makao ya watawa kunakili Biblia zenye michoro.

Kisehemu cha maandishi ya Biblia ya León yenye madoido mengi. Ingawa ni zenye thamani, Biblia kama hizo hazikusaidia sana katika kueneza Neno la Mungu

Biblia moja yenye michoro inapatikana kwenye kanisa la San Isidoro huko León, Hispania. Iliandikwa mwaka wa 960 W.K., ina vipande vya ngozi 516 na urefu wa sentimita 47, upana wa sentimita 34 na uzani wa kilogramu 18. Nakala nyingine ambayo inapatikana kwenye Maktaba ya Vatikani, ni Biblia ya Ripoll, iliyoandikwa mwaka wa 1020 W.K. Ni mojawapo ya Biblia zenye madoido mengi zilizoandikwa katika Enzi za Kati. Ili kutokeza michoro hiyo, mtawa angehitaji kutumia siku nzima kuandika herufi moja ya kwanza au juma moja kuandika ukurasa wa kwanza. Ingawa ni zenye thamani, Biblia hizo hazikusaidia sana kueneza ujumbe wa Neno la Mungu.

BIBLIA YA KIARABU

Kufikia karne ya nane, lugha nyingine ilianza kutumiwa nchini Hispania kutokana na uvamizi wa Waislamu. Katika maeneo yaliyotawaliwa na Waislamu, Kiarabu kilizungumzwa badala ya Kilatini na hivyo kukawa na uhitaji wa kutafsiri Biblia katika lugha hiyo mpya.

Bila shaka, tafsiri nyingi za Biblia ya Kiarabu, hasa Vitabu vya Injili, zilisambazwa huko Hispania katika enzi za kati. Inaonekana kwamba katika karne ya nane, John aliyekuwa askofu wa Seville, alitafsiri Biblia nzima katika Kiarabu. Inasikitisha kwamba Biblia nyingi za Kiarabu zimetoweka. Tafsiri moja ya Kiarabu ya vitabu vya Injili  iliyoandikwa katika karne ya kumi imehifadhiwa katika kanisa la León, huko Hispania.

Tafsiri ya Kiarabu ya Vitabu vya Injili, karne ya kumi W.K.

TAFSIRI ZA KIHISPANIA

Mwishoni mwa Enzi za Kati, lugha ya Castilian, au Kihispania, ilianza kuenea kwenye Rasi ya Iberia. Lugha hiyo ilitumiwa sana katika kueneza Neno la Mungu. * Tafsiri ya kale zaidi ya Biblia ya Kihispania ilipatikana katika maandishi ya La Fazienda de Ultra Mar (Matukio Kutoka Maeneo ya Mbali), yaliyoandikwa mwanzoni mwa karne ya 13. Maandishi hayo yana simulizi la safari ya kwenda Israel, na yanatia ndani maandishi ya Pentateuki na vitabu vingine vya Maandiko ya Kiebrania na vilevile Vitabu vya Injili na barua za mitume.

Mfalme Alfonso wa Kumi aliunga mkono kazi ya kutafsiri Biblia katika Kihispania

Viongozi wa kidini hawakufurahishwa na tafsiri hiyo. Mwaka wa 1234, Baraza la Tarragona liliagiza vitabu vyote vya Biblia za lugha za kienyeji vipelekwe kwa makasisi ili vichomwe. Hata hivyo, agizo hilo halikukomesha kazi ya kutafsiri Biblia. Mfalme Alfonso wa Kumi (1252 hadi 1284), anayeaminika kuwa mwanzilishi wa maandishi ya Kihispania, alitaka Biblia itafsiriwe katika lugha hiyo mpya na akaunga mkono kazi hiyo. Kuanzia wakati huo, tafsiri za Kihispania zilitia ndani Biblia ya Kabla ya Alfonsina na Biblia ya Alfonsina iliyotokezwa muda mfupi baadaye, ambayo ilikuwa tafsiri kubwa zaidi ya maandishi ya Kihispania kufikia wakati huo.

Kurasa za Biblia ya Kabla ya Alfonsina (kushoto) na Biblia ya Alfonsina (kulia) zilizoandikwa karne ya 13

Tafsiri hizo mbili zilisaidia sana kuboresha lugha mpya ya Kihispania. Msomi Thomas Montgomery anasema hivi kuhusu Biblia ya Kabla ya Alfonsina: “Mtafsiri wa Biblia hiyo alitokeza tafsiri sahihi na yenye lugha bora. . . . Lugha hiyo ni rahisi na yenye kueleweka kwa watu wasiojua Kilatini.”

Hata hivyo, Biblia hizo za kale za Kihispania zilitafsiriwa kutokana na Vulgate ya Kilatini badala ya lugha za awali. Kuanzia karne ya 14 wasomi wa Kiyahudi walianza kutokeza tafsiri za Kihispania za Maandiko ya Kiebrania (yanayoitwa Agano la Kale) moja kwa moja kutoka kwenye maandishi ya Kiebrania. Wakati huo, Hispania ilikuwa na wakaaji wengi zaidi Wayahudi barani Ulaya, na watafsiri wa Kiyahudi wangeweza kupata maandishi bora ya Kiebrania kwa ajili ya kutafsiri. *

Mfano mmoja ni Biblia ya Alba, iliyokamilishwa katika karne ya 15. Mhispania mashuhuri, Luis de Guzmán, alimwagiza Rabbi Moisés Arragel aitafsiri Biblia katika lugha ya castizo (Kihispania sanifu). Alitoa sababu mbili za kutafsiri Biblia hiyo mpya. Kwanza, “Biblia zinazopatikana leo katika lugha za Kiroma si sahihi,” na pili, “Watu kama sisi tunahitaji sana maandishi ya pambizoni kuhusu masimulizi yasiyoeleweka.” Ombi lake linaonyesha kwamba wakati huo watu walitamani sana kusoma na kuielewa Biblia. Pia, linaonyesha kwamba tayari Biblia za lugha za kienyeji zilikuwa zimesambazwa sana huko Hispania.

Jitihada za watafsiri na waandishi ziliwasaidia  watu wenye elimu huko Hispania kusoma Biblia katika lugha yao bila kizuizi. Hiyo ndiyo sababu mwanahistoria Juan Orts González alisema: “Wahispania waliijua Biblia vizuri kuliko Wajerumani na Waingereza walioishi kabla ya Luther.”

“Wahispania waliijua Biblia vizuri kuliko Wajerumani na Waingereza walioishi kabla ya Luther.”—Mwanahistoria Juan Orts González

Hata hivyo, kufikia mwisho wa karne ya 15, Baraza la Kuhukumu Waasi wa Kidini la Hispania lilipiga marufuku kutafsiri na kumiliki Biblia za lugha za kienyeji. Kisha, Biblia ikapigwa marufuku nchini Hispania kwa miaka mingi. Miaka mia tatu ilipita kabla ya marufuku kuondolewa. Katika kipindi hicho kigumu, wasomi wachache wenye ujasiri walitafsiri Biblia katika Kihispania wakiwa katika nchi za nje na kuziingiza kisiri nchini Hispania. *

Kama historia hii ya Biblia katika Hispania ya enzi za kati inavyoonyesha, wapinzani wamejaribu njia nyingi ili kukomesha kutafsiriwa kwa Neno la Mungu. Ingawa hivyo, wameshindwa kunyamazisha maneno ya Mweza-Yote.Zaburi 83:1; 94:20.

Kazi ngumu ya wasomi mbalimbali iliwezesha Biblia kusitawi na kuenea katika Hispania ya enzi za kati. Watafsiri wa kisasa wamefuata mfano wa wale waliotafsiri Maandiko katika Kilatini, Kigothi, Kiarabu, na Kihispania. Matokeo ni kwamba mamilioni ya watu wanaozungumza Kihispania leo wanaweza kusoma Neno la Mungu katika lugha wanayoielewa vizuri.

^ fu. 10 Zinatia ndani lugha ya Castilian, Kigalisiani, Kikatalani, na Kireno.

^ fu. 17 Leo, Kihispania kinazungumzwa na watu milioni 540 hivi.

^ fu. 20 See the article “Jina la Mungu na Jitihada za Alfonso de Zamora za Kutokeza Maandishi Sahihi,” katika toleo la gazeti hili la Desemba 1, 2011.

^ fu. 23 See the article “Pambano la Casiodoro de Reina kwa Ajili ya Biblia ya Kihispania,” katika toleo la gazeti hili la Juni 1, 1996.

Kuanzia karne ya tano hadi ya nane W.K., Biblia za Kilatini na Kiarabu zilitumiwa kuwatangazia Wahispania ujumbe wa Mungu