Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

 SIRI YA FURAHA YA FAMILIA

Ikiwa Mtoto Wako Ni Mlemavu

Ikiwa Mtoto Wako Ni Mlemavu

CARLO: * “Mwana wetu, Angelo, ana ugonjwa wa Down syndrome. Ugonjwa wake hutuchosha kimwili, kiakili, na kihisia. Nguvu unazohitaji kumtunza mtoto mlemavu ni mara mia moja zaidi ya nguvu unazohitaji kumtunza mtoto asiye mlemavu. Wakati mwingine ndoa yetu huathirika.”

MIA: “Inahitaji uvumilivu na subira nyingi kumfundisha Angelo hata mambo rahisi zaidi. Ninapokuwa nimechoka sana, ninakosa subira na kumkasirikia mume wangu, Carlo. Wakati mwingine hatukubaliani kuhusu mambo fulani, na tunaanza kubishana.”

Je, unakumbuka siku ambayo mtoto wenu alizaliwa? Bila shaka, mlifurahia kumbeba. Hata hivyo, kwa wazazi kama Carlo na Mia, shangwe yao hugubikwa na wasiwasi wanapoambiwa kwamba mtoto wao ni mgonjwa au ni mlemavu.

Je, una mtoto mlemavu? Ikiwa ndivyo, huenda ukajiuliza ikiwa utafanikiwa kumlea. Hata hivyo, usikate tamaa. Wazazi walio na matatizo kama yako wamefanikiwa kukabiliana nayo. Fikiria matatizo matatu ambayo huenda ukakabili na jinsi hekima inayopatikana katika Biblia inavyoweza kukusaidia.

TATIZO LA 1: HUAMINI KWAMBA MTOTO WAKO NI MLEMAVU.

Wazazi wengi huumia sana wanapotambua kwamba mtoto wao ni mgonjwa. Juliana, mama kutoka Mexico anasema: “Sikuamini madaktari waliponiambia  kuwa mwana wetu, Santiago, alikuwa amepooza ubongo. Nilifadhaika sana.” Wengine wanaweza kuhisi kama Villana, mama kutoka Italia. “Nilitaka kuwa na mtoto ijapokuwa ni hatari kwa wanawake wenye umri kama wangu,” anasema. “Sasa, mwanangu anaposumbuliwa na ugonjwa wa Down syndrome, ninajihisi mwenye hatia.”

Ikiwa unapambana na hisia za kuvunjika moyo au hatia, tambua kwamba ni hali ya kawaida. Mungu hakukusudia wanadamu wawe wagonjwa. (Mwanzo 1:27, 28) Hakuwaumba wazazi wakiwa na uwezo wa kukabiliana na ulemavu. Kwa njia ya mfano, huenda ukahitaji “kuombolezea” kile ulichopoteza, yaani, afya ya mtoto wako. Itachukua muda kukabiliana na hisia zako na kuzoea hali hiyo.

Vipi ikiwa unajilaumu kwa sababu ya ulemavu wa mtoto wako? Kumbuka kwamba hakuna anayejua kikamili jinsi chembe za urithi, mazingira, na hali nyingine zinavyoathiri afya ya mtoto. Kwa upande mwingine, huenda ukataka kumlaumu mwenzi wako. Hata hivyo, usimlaumu. Ni vema kushirikiana na mwenzi wako na kukazia fikira kumlea mtoto wenu.—Mhubiri 4:9, 10.

PENDEKEZO: Jifunze mengi kuhusu hali ya mtoto wenu. Biblia husema, “Hekima inahitajika ili kuwa na familia nzuri, na utambuzi unahitajika ili kuifanya imara.”—Methali 24:3, New Century Version.

Unaweza kujifunza mengi kutoka kwa wataalamu wa kitiba na machapisho yanayotegemeka. Kujifunza kuhusu hali ya mtoto wenu ni kama kujifunza lugha mpya. Mwanzoni itakuwa vigumu, lakini unaweza kufaulu.

Carlo na Mia walionukuliwa mwanzoni, walitafuta habari kutoka kwa daktari wao na shirika linaloshughulika na ugonjwa wa mtoto wao. Wazazi hao walieleza hivi: “Hilo lilitusaidia kuelewa matatizo tunayoweza kutarajia na pia mambo ‘mazuri’ kuhusu ugonjwa wa Down syndrome. Tuliona kwamba kwa kadiri fulani mtoto wetu angeishi maisha ya kawaida. Hilo lilitufariji sana.”

JARIBUNI KUFANYA HIVI: Kazia fikira mambo ambayo mtoto wenu anaweza kufanya. Pangeni kufanya mambo pamoja mkiwa familia. Mtoto wenu akifanikiwa kutimiza hata jambo dogo, mpongezeni na kushangilia pamoja naye.

TATIZO LA 2: UNAHISI UMECHOKA NA HUNA MTU WA KUZUNGUMZA NAYE.

Huenda ukahisi kwamba unatumia nguvu nyingi kumlea mtoto wenu. Jenney, mama kutoka New Zealand, anasema, “Kwa miaka michache baada ya mwanangu kugunduliwa ana ugonjwa wa spina bifida, nilihisi uchovu na hata kulia nilipojaribu kufanya kazi za nyumbani.”

Tatizo lingine ni kwamba huenda ukahisi umetengwa. Ben ana mtoto mwenye tatizo la misuli na ugonjwa wa Asperger. Anasema hivi: “Watu wengi hawawezi kuelewa kikamili jinsi maisha yetu yalivyo.” Huenda ukataka sana kuzungumza na watu wengine. Lakini, rafiki zako hawana watoto walemavu. Hivyo, unasita kuzungumza nao.

PENDEKEZO: Omba msaada. Na ukubali unaposaidiwa. Juliana, aliyenukuliwa mapema anasema: “Wakati mwingine mimi na mume wangu tunaaibika kuomba msaada.” Hata hivyo, anaongeza kusema, “Tumejifunza kwamba tunahitaji msaada wa wengine. Tunaposaidiwa, hatuhisi upweke.” Rafiki wa karibu au mtu wa ukoo anapojitolea kukaa na mtoto wako kwenye tafrija au mikutano ya Kikristo, kubali kwa uthamini. Methali moja ya Biblia husema, “Rafiki wa kweli anapenda nyakati zote, naye ni ndugu aliyezaliwa kwa ajili ya wakati wa taabu.”—Methali 17:17.

Tunza afya yako. Kama tu gari la wagonjwa linavyopaswa kuwekwa mafuta kwa ukawaida ili kuendelea kuwapeleka wagonjwa hospitalini, unapaswa kudumisha afya yako kwa kupata lishe bora, kufanya mazoezi, na kupumzika ili uendelee kumtunza mtoto wako vizuri. Javier, ambaye ana mtoto mlemavu anasema hivi: “Mvulana wangu hawezi kutembea, hivyo ninajitahidi kula vizuri. Mimi humpeleka kila mahali. Mimi ndiye miguu yake!”

Unawezaje kupata wakati wa kutunza afya yako? Wazazi fulani hupanga zamu za kumtunza mtoto wao. Hivyo, mzazi mmoja anaweza kupumzika au kufanya mambo mengine ya kibinafsi. Unahitaji kununua wakati kutoka kwenye mambo yasiyo muhimu, na inaweza kuwa vigumu kusawazika. Hata hivyo, kama anavyosema Mayuri, mama kutoka India, “Hatimaye utazoea ratiba hiyo.”

 Zungumza na rafiki unayemwamini. Hata rafiki asiye na mtoto mlemavu anaweza kukufariji. Pia, unaweza kusali kwa Yehova Mungu. Je, sala inaweza kukusaidia? Yazmin aliye na watoto wawili wenye ugonjwa wa cystic fibrosis, anasema hivi, “Nyakati fulani nimehisi mkazo sana kana kwamba nilikuwa karibu kufa.” Hata hivyo, anaongezea, “Ninasali kwa Yehova ili kupata kitulizo na nguvu. Kisha, ninahisi kwamba ninaweza kuendelea.”—Zaburi 145:18.

JARIBUNI KUFANYA HIVI: Chunguza chakula unachokula, muda unaotumia kufanya mazoezi na kulala. Chunguza jinsi unavyoweza kununua wakati kutoka kwenye mambo yasiyo muhimu ili utunze afya yako. Endelea kurekebisha ratiba yako inapohitajika.

TATIZO LA 3: UNAMKAZIA FIKIRA ZAIDI MTOTO MLEMAVU KULIKO WENGINE KATIKA FAMILIA.

Ugonjwa wa mtoto unaweza kuathiri chakula ambacho familia hula, wanakoenda, na muda ambao wazazi wanatumia pamoja na kila mtoto. Hivyo, huenda watoto wengine wakahisi wanapuuzwa. Pia, wazazi wanaweza kutumia muda mwingi kushughulika na mtoto wao mgonjwa hivi kwamba ndoa yao ikaathiriwa. Lionel, baba kutoka Liberia anasema: “Wakati mwingine mke wangu anasema kwamba anashughulika zaidi kuliko mimi na kwamba simjali mtoto wetu. Ninahisi haniheshimu na wakati mwingine ninamjibu kwa ukali.”

PENDEKEZO: Ili kuwahakikishia watoto wako wote kwamba unawapenda, panga shughuli wanazofurahia. “Wakati mwingine tunamfanyia mwana wetu mkubwa jambo la pekee,” anasema Jenney, aliyenukuliwa mwanzoni, “hata kama ni kula chakula cha mchana kwenye mkahawa anaopenda.”

Pendezwa na watoto wako wote

Ili kulinda ndoa yenu, zungumza na kusali pamoja na mwezi wako. Aseem, baba kutoka India ambaye mtoto wake ana ugonjwa wa kifafa anasema: “Ingawa nyakati nyingine mimi na mke wangu tunahisi uchovu na kuvunjika moyo, tunapanga muda wa kukaa, kuzungumza, na kusali pamoja. Kila asubuhi kabla watoto wetu kuamka, tunatumia wakati pamoja kuzungumzia mistari fulani ya Biblia.” Wenzi wengine wa ndoa huzungumza faraghani kabla ya kulala. Mazungumzo yenu ya ukaribu na sala za kutoka moyoni zinaweza kuimarisha ndoa yenu mnapokabili mkazo. (Methali 15:22) Mwenzi mmoja wa ndoa alisema hivi: “Baadhi ya nyakati nzuri sana katika maisha yetu ni wakati tulipokabili matatizo.”

JARIBUNI KUFANYA HIVI: Wapongeze watoto wenu kwa msaada wowote wanaompa mtoto wenu mgonjwa. Waonyeshe kwa ukawaida watoto wako na mwenzi wako kwamba unawapenda na kuwathamini.

ENDELEA KUWA NA MAONI YANAYOFAA

Biblia inaahidi kwamba hivi karibuni Mungu ataondoa kabisa magonjwa na ulemavu unaowahangaisha watu wote. (Ufunuo 21:3, 4) Siku hiyo, “hakuna mkaaji atakayesema: ‘Mimi ni mgonjwa.’” *Isaya 33:24.

Kwa sasa, unaweza kufanikiwa ukiwa mzazi wa mtoto mlemavu. Carlo na Mia walionukuliwa mwanzoni wanasema hivi: “Usivunjike moyo unapoona kana kwamba kila kitu kinaenda kombo, fikiria mambo mazuri kuhusu mtoto wako kwa sababu ni mengi.”

^ fu. 3 Majina katika makala hii yamebadilishwa.

^ fu. 29 Unaweza kusoma mengi zaidi kuhusu jinsi Biblia inavyoahidi afya kamilifu katika sura ya 3 ya kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

JIULIZE . . .

  • Ninafanya nini ili kuimarisha hali yangu ya kimwili, kihisia, na kiroho?
  • Ni lini mara ya mwisho nilipowapongeza watoto wangu wengine kwa msaada wao?