Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mwenzi wa Ndoa Anapohitaji Kutunzwa kwa Njia ya Pekee

Mwenzi wa Ndoa Anapohitaji Kutunzwa kwa Njia ya Pekee

Siri ya Furaha ya Familia

Mwenzi wa Ndoa Anapohitaji Kutunzwa kwa Njia ya Pekee

Tangu nilipopata ugonjwa wa kuchoka daima (“chronic fatigue syndrome”), imembidi mume wangu afanye kazi akiwa peke yake. Lakini hazungumzi nami kamwe kuhusu matumizi yetu ya pesa. Kwa nini hazungumzi nami kuhusu mambo ya pesa? Inaonekana kwamba tuna tatizo kubwa la kifedha na anajua kuwa nikitambua nitahangaika sana.—Nancy. *

NDOA inaweza kuwa na matatizo, lakini mwenzi mmoja anapopata ugonjwa wa kudumu huku yule mwingine akiwa na afya nzuri, matatizo yanaweza kuongezeka. * Je, unamtunza mwenzi ambaye ana tatizo la kiafya? Ikiwa ndivyo, je, unahangaishwa na moja kati ya maswali haya: ‘Nitafanya nini ikiwa afya ya mwenzi wangu itadhoofika hata zaidi? Ninaweza kuendelea kwa muda gani kumtunza mwenzi wangu na wakati uleule niendelee kupika, kufanya usafi, na kufanya kazi? Kwa nini ninahisi kwamba nina hatia kwa sababu ya kuwa na afya nzuri?’

Kwa upande mwingine, ikiwa wewe ni mwenzi aliye mgonjwa, huenda ukajiuliza: ‘Ninaweza kujiheshimu jinsi gani ikiwa siwezi kutimiza madaraka yangu? Je, mwenzi wangu ananichukia kwa sababu mimi ni mgonjwa? Je, furaha yetu tukiwa wenzi wa ndoa imekwisha?’

Inahuzunisha kwamba ndoa fulani zimevunjika kwa sababu ya mkazo ambao unasababishwa na ugonjwa wa kudumu. Lakini hilo halimaanishi kwamba ndoa yenu haitafanikiwa.

Wenzi wengi wa ndoa wameendelea kuishi pamoja na hata wamefanikiwa ingawa wanakabiliana na ugonjwa wa kudumu. Kwa mfano, fikiria Yoshiaki na Kazuko. Kwa sababu ya kuumia uti wa mgongo, Yoshiaki hawezi kufanya jambo lolote bila kusaidiwa. Kazuko anaeleza hivi: “Mume wangu anahitaji kusaidiwa katika kila jambo. Kwa sababu ya kumtunza, ninaumwa na shingo, mabega, na mikono, na ninaenda kwenye hospitali fulani kutibiwa mifupa. Mara nyingi ninahisi kwamba kazi ya kumtunza ni ngumu sana.” Hata hivyo, ingawa anakabili matatizo hayo, Kazuko anasema: “Uhusiano wetu tukiwa wenzi wa ndoa umekuwa wa karibu zaidi.”

Hivyo basi, ni nini siri ya kupata furaha katika hali hizo? Kwanza, wale ambao wanadumisha uradhi na kutosheka katika ndoa yao wanaona ugonjwa kuwa tatizo lao wawili bali si tatizo la mwenzi aliye mgonjwa. Kwa kweli, mwenzi mmoja anapokuwa mgonjwa, wote wawili wanaumia sana, hata ikiwa ni kwa njia tofauti. Uhusiano huo wa kutegemeana kati ya mume na mke unafafanuliwa hivi kwenye Mwanzo 2:24: “Mwanamume atamwacha baba yake na mama yake naye atashikamana na mke wake nao watakuwa mwili mmoja.” Kwa hiyo, mume au mke anapopata ugonjwa wa kimwili unaoendelea, ni jambo la maana sana kwa wote wawili kushirikiana katika kukabiliana na tatizo hilo.

Kwa kuongezea, uchunguzi unaonyesha kwamba wenzi wa ndoa ambao wanadumisha uhusiano mzuri wanapokabiliana na ugonjwa wa kudumu, wanakubali hali yao na wanajifunza njia nzuri za kushughulika na ugonjwa huo. Njia nyingi ambazo wamejifunza zinapatana na mashauri ya Biblia ambayo bado yana faida leo. Chunguza mapendekezo matatu yanayofuata.

Onyesheni Kwamba Mnahangaikiana

Andiko la Mhubiri 4:9 linasema kwamba “wawili ni afadhali kuliko mmoja.” Kwa nini? Kwa sababu mstari wa 10 unaeleza kuwa “mmoja wao akianguka, yule mwingine anaweza kumwinua mwenzake.” Je, ‘unamwinua mwenzako’ kwa kumwonyesha kwamba unamthamini?

Je, mnaweza kutafuta njia za kusaidiana? Yong, ambaye mke wake amepooza kwa kadiri fulani anasema: “Ninajitahidi kumhangaikia mke wangu katika kila pindi. Kila mara ninapokuwa na kiu, ninafikiria kwamba huenda yeye pia ana kiu. Ninapotaka kwenda nje kuona mandhari yenye kupendeza, ninamuuliza ikiwa angependa kwenda pamoja nami. Sote tunahisi uchungu na kuvumilia ugonjwa huo pamoja.”

Kwa upande mwingine, ikiwa unatunzwa na mwenzi wako, je, kuna mambo fulani ambayo unaweza kujifanyia bila kuhatarisha afya yako? Ikiwa ndivyo, hilo linaweza kukufanya uhisi kwamba unathaminiwa zaidi na huenda likamsaidia mwenzi wako aendelee kukutunza.

Badala ya kufikiri tu kwamba unajua njia bora ya kumwonyesha mwenzi wako kuwa unamjali, kwa nini usimuulize mambo ambayo angethamini zaidi? Mwishowe, Nancy ambaye alitajwa mwanzoni mwa habari hii alimwambia mume wake jinsi alivyohisi kwa sababu ya kutojua hali ya kifedha ya familia. Sasa, mume wake anajitahidi kuzungumza naye zaidi kuhusu jambo hilo.

JARIBU KUFANYA HIVI: Orodhesha mambo ambayo unahisi kwamba mwenzi wako anaweza kufanya ili hali yako ya sasa iwe rahisi zaidi, na umwombe mwenzi wako afanye hivyo pia. Kisha mbadilishane orodha hizo. Kila mmoja wenu anapaswa kuchagua pendekezo moja au mawili ambayo mnaweza kutumia kihalisi.

Muwe na Ratiba Iliyosawazika

Mfalme Sulemani mwenye hekima aliandika hivi: “Kuna wakati uliowekwa wa kila kitu.” (Mhubiri 3:1) Hata hivyo, huenda ikaonekana kwamba hamwezi kudumisha ratiba iliyosawazika, kwa sababu ugonjwa wenye kuendelea unaweza kuvuruga utendaji wa kawaida wa familia. Mnaweza kufanya nini ili muwe na usawaziko kwa kadiri fulani?

Mkiwa pamoja mnaweza kuacha mara kwa mara kuhangaikia sana mambo ya kitiba. Je, mnaweza kufurahia mambo fulani ambayo mlifanya pamoja kabla ya ugonjwa kutokea? Ikiwa haiwezekani, ni mambo gani mapya ambayo mnaweza kujaribu kufanya? Unaweza kufanya jambo rahisi kama vile kumsomea mwenzi wako habari fulani kwa sauti au kufanya jambo gumu kama vile kujifunza pamoja lugha mpya. Kufanya pamoja mambo ambayo ugonjwa hauwazuii kufanya kutaimarisha kifungo chenu cha “mwili mmoja” na kuzidisha furaha yenu.

Jambo lingine ambalo litawasaidia kudumisha usawaziko ni kushirikiana na watu wengine. Biblia inasema hivi kwenye Methali 18:1: “Mtu anayejitenga na wengine atatafuta mapendezi yake mwenyewe; atashindana na hekima yote inayotumika.” Je, umeona katika mstari huo kwamba kujitenga kunaweza kuwa na matokeo mabaya kwa akili? Kwa upande mwingine, kushirikiana na wengine mara kwa mara kunaweza kuwafanya mchangamke na kuwasaidia muwe tena na mtazamo mzuri wa akili. Kwa nini msimwalike mtu fulani awatembelee?

Nyakati nyingine, inakuwa vigumu kwa yule anayemtunza mwenzi wake wa ndoa kuwa na usawaziko. Wengine wao wanafanya kazi nyingi sana na hivyo wanadhoofika polepole na kuhatarisha afya yao wenyewe. Mwishowe, huenda hata wakashindwa kabisa kuendelea kumtunza mwenzi wao mpendwa. Hivyo, ikiwa unamtunza mwenzi wako wa ndoa ambaye ana ugonjwa wa kudumu, usipuuze mahitaji yako mwenyewe. Tenga wakati wa kuwa peke yako kwa ukawaida ili upumzike. * Wengine wameona kwamba wamefaidika kiafya kwa kuzungumzia mahangaiko yao mara kwa mara pamoja na rafiki wa jinsia yao ambaye wanamwamini.

JARIBU KUFANYA HIVI: Andika kwenye karatasi vizuizi unavyokabili unapomtunza mwenzi wako wa ndoa. Kisha uandike mambo ambayo unaweza kufanya ili kushinda au kukabiliana na vizuizi hivyo kwa njia nzuri zaidi. Badala ya kuchanganua vizuizi hivyo kupita kiasi, jiulize hivi, ‘Ni njia gani rahisi zaidi na nzuri ya kuboresha hali hii?’

Jitahidi Kudumisha Mtazamo Unaofaa

Biblia inaonya hivi: “Usiseme: ‘Kwa nini siku za zamani zilikuwa bora kuliko hizi?’” (Mhubiri 7:10) Kwa hiyo, epuka kufikiria sana jinsi ambavyo hali zingekuwa ikiwa ugonjwa haungekuwapo. Kumbuka kwamba katika ulimwengu huu, huwezi kuwa na furaha kamili. Siri ni kukubali hali yako na kujitahidi kadiri unavyoweza.

Ni nini kinachoweza kukusaidia kufanya hivyo pamoja na mwenzi wako? Zungumzeni pamoja kuhusu baraka zenu. Uwe mwenye furaha wakati afya yako inapoboreka hata kwa kiwango kidogo. Mfikirie mambo ambayo mnaweza kutazamia wakati ujao, na mjiwekee miradi ambayo mnaweza kutimiza pamoja.

Shoji na Akiko, ambao ni wenzi wa ndoa wamefuata mashauri yaliyotolewa hapo juu, na wamepata matokeo mazuri. Muda fulani baada ya Akiko kupatikana na ugonjwa wa misuli, iliwalazimu waache mgawo fulani wa pekee katika huduma ya Kikristo ya wakati wote. Je, walivunjika moyo? Ndiyo. Hata hivyo, Shoji anawashauri hivi wale ambao wanakabili hali kama hiyo: “Msijivunje moyo kwa kufikiria mambo ambayo hamwezi tena kufanya. Endeleeni kuwa na mtazamo unaofaa. Hata ingawa nyote wawili mnatumaini kwamba siku moja mtarudia utendaji wenu wa kawaida, kwa sasa kazieni fikira jinsi maisha yenu yalivyo. Kwangu, hilo linamaanisha kumkazia fikira mke wangu na kumsaidia.” Shauri hilo linalofaa linaweza kukusaidia ikiwa mwenzi wako anahitaji kutunzwa kwa njia ya pekee.

[Maelezo ya chini]

^ fu. 3 Baadhi ya majina yamebadilishwa.

^ fu. 4 Katika habari hii tutazungumzia wakati ambapo mwenzi wa ndoa ana ugonjwa wa kimwili wa kudumu. Hata hivyo, wenzi wa ndoa ambao wanakabiliana na matatizo ya kimwili kwa sababu ya aksidenti au wanakabiliana na matatizo ya kihisia kama vile kushuka moyo wanaweza pia kufaidika kwa kutumia habari inayofuata.

^ fu. 20 Ikitegemea hali zako, huenda ikafaa kutafuta msaada mara kwa mara kutoka kwa wataalamu wa mambo ya afya au mashirika ya kijamii ya kuwatunza wagonjwa, ikiwa yanapatikana katika eneo lenu.

JIULIZE . . .

Kwa sasa, ni nini ambacho mimi na mwenzi wangu tunahitaji sana kufanya?

▪ Kuzungumza zaidi kuhusu ugonjwa huo

▪ Kutozungumza sana kuhusu ugonjwa huo

▪ Kupunguza mahangaiko

▪ Kuhangaikiana zaidi

▪ Kufanya pamoja jambo fulani ambalo halihusiani na ugonjwa huo

▪ Kushirikiana zaidi na watu wengine

▪ Kuwa na miradi ileile

[Picha katika ukurasa wa 12]

Ili kupata usawaziko maishani, je, mnaweza kushiriki katika utendaji fulani pamoja?