Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Biblia ya Bedell—Hatua Mojawapo Katika Kuelewa Vizuri Biblia

Biblia ya Bedell—Hatua Mojawapo Katika Kuelewa Vizuri Biblia

KASISI Mwingereza William Bedell alipoenda Ireland mwaka wa 1627, alishangazwa na hali aliyoikuta. Nchi ya Ireland yenye Wakatoliki wengi ilitawaliwa na Uingereza yenye Waprotestanti. Waprotestanti walikuwa tayari wametafsiri Biblia katika lugha za asili zilizozungumzwa katika bara la Ulaya. Hata hivyo, hakuna mtu aliyekuwa ametafsiri Biblia katika lugha iliyozungumzwa nchini Ireland.

Bedell alihisi kwamba watu wa Ireland “hawapaswi kupuuzwa kwa sababu hawajui Kiingereza.” Hivyo alianzisha mradi wa kutafsiri Biblia katika Kiairishi. Hata hivyo, alikabili upinzani mkali sana, hasa kutoka wa Waprotestanti. Kwa nini?

APINGWA KUTUMIA LUGHA YA WATU WA IRELAND

Bedell aliamua kujifunza Kiairishi. Aliwatia moyo wanafunzi kutumia Kiairishi alipokuwa mkuu wa Chuo cha Trinity huko Dublin na baadaye alipokuwa askofu wa Kilmore. Malkia Elizabeth wa Kwanza wa Uingereza alianzisha Chuo cha Trinity ili kupata makasisi watakaowafundisha raia zake ujumbe wa Biblia katika lugha yao ya asili. Bedell alijitahidi kufanikisha jambo hilo.

Alipokuwa katika dayosisi ya Kilmore, watu wengi walizungumza Kiairishi. Hivyo, Bedell alijitahidi kutafuta makasisi waliozungumza Kiairishi. Alikazia jambo hilo kwa msingi wa maneno ya mtume Paulo yaliyo katika 1 Wakorintho 14:19, yanayosema hivi: “Hata hivyo, katika kutaniko ingekuwa afadhali niseme maneno matano kwa akili yangu, ili pia niwafundishe wengine kwa mdomo, kuliko maneno elfu kumi kwa lugha,” yaani, lugha isiyoeleweka.

Hata hivyo, watu wenye mamlaka walitumia kila njia kupinga jitihada zake. Kulingana wanahistoria, baadhi ya watu walidai kwamba kutumia Kiairishi kulikuwa “hatari kwa Taifa” na wengine walisema kwamba hilo “halikuwa na masilahi kwa Serikali.” Wengine walihisi kwamba Uingereza ingefaidika kwa kutowaelimisha Waairishi. Waingereza walitunga sheria zilizowaamuru Waairishi waache kutumia lugha na tamaduni zao na wajifunze Kiingereza na kufuata tamaduni za Waingereza.

MRADI WA BIBLIA YA BEDELL

Bedell hakuvunjwa moyo na maoni hayo ya kidikteta. Mapema katika miaka ya 1630, alianza kutafsiri toleo la Biblia ya Kiingereza (King James Version ya mwaka 1611) katika Kiairishi. Alitaka kutokeza Biblia ambayo watu wengi wangeelewa. Alihisi kwamba watu wa hali ya chini wasingeweza kuchunguza Maandiko na kuipata njia ya uzima wa milele endapo Biblia ingeendelea kuwa katika lugha wasiyoelewa.—Yohana 17:3.

Bedell hakuwa mtu wa kwanza kuona jambo hilo. Miaka 30 hivi mapema, kasisi mwingine, William Daniel, aliona jinsi ilivyokuwa vigumu kwa mtu yeyote kujifunza mafundisho ya Biblia yanapokuwa katika “lugha isiyoeleweka.” Daniel alitafsiri Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo katika Kiairishi. Bedell akaanza kutafsiri Maandiko ya Kiebrania. Biblia ya Bedell inatia ndani maandiko aliyotafsiri William Daniel. Kama matokeo, Biblia ya Bedell—tafsiri ya Biblia ya kwanza ya Kiairishi—ikawa tafsiri pekee ya Biblia ya Kiairishi iliyotumika kwa miaka 300 iliyofuata.

Bedell alifanya kazi na watu wawili waliozungumza Kiairishi ili wamsaidie kutafsiri Biblia katika lugha ya Kiairishi. Walipokuwa wakiendelea na kazi yao, Bedell na msaidizi wake mmoja au wawili wenye kutegemeka, walifanya kazi nzito ya kuchunguza na kurekebisha kila mstari. Walitumia tafsiri ya Kiitaliano ya mwanatheolojia Mswisi aliyeitwa Giovanni Diodati, Septuajinti ya Kigiriki, na hati ya awali yenye thamani ya Maandiko ya Kiebrania.

Pia, walifuata kile ambacho watafsiri wa Biblia ya King James Version (Bedell aliwafahamu vizuri wengi wao) walifanya kwa kutumia jina la Mungu katika mistari kadhaa ya Biblia yao. Kwa mfano, katika Kutoka 6:3, walitumia jina la Mungu, “Iehovah.” Hati ya awali ya Bedell imehifadhiwa katika Maktaba ya Marsh, Dublin, nchini Ireland.—Ona sanduku “Kumkumbuka Bedell na Kutambua Mchango wake.”

HATIMAYE YACHAPISHWA

Bedell alikamilisha mradi wake mwaka wa 1640 hivi. Hata hivyo, hakuchapisha kazi yake mara moja. Kwa nini? Sababu moja ni upinzani mkali aliokuwa akikabili. Wapinzani wake walimdhihaki mtafsiri mkuu wa Bedell wakiwa na lengo la kuishushia hadhi tafsiri hiyo. Hata walimkamata na kumfunga gerezani. Pia, mwaka wa 1641 kulitokea uasi dhidi ya Uingereza uliosababisha umwagaji wa damu. Licha ya kwamba alikuwa na asili ya Uingereza, Bedell alilindwa kwa muda na watu wa Ireland wakati wa uasi huo, kwa kuwa walijua kwamba aliwahangaikia sana. Hata hivyo, baadaye wanajeshi waasi walimfunga katika gereza lililokuwa na hali mbaya sana. Huenda hali hizo zilichangia kifo chake katika mwaka wa 1642. Alikufa kabla kazi yake haijachapishwa.

Ukurasa wa kwanza wa hati ya awali ya Bedell, karibu mwaka wa 1640, na Biblia iliyochapishwa, mwaka wa 1685

Kazi ya Bedell ilikuwa karibu kupotea kabisa nyumba yake ilipovamiwa na kuharibiwa. Hata hivyo, rafiki yake wa karibu alifanikiwa kuokoa nyaraka zote zilizotafsiriwa. Baadaye, Narcissus Marsh, aliyekuja kuwa askofu mkuu wa Armagh na mkuu wa Kanisa la Ireland, alizipata nyaraka hizo. Alifadhiliwa na mwanasayansi Robert Boyle na kwa ujasiri alichapisha Biblia ya Bedell mwaka wa 1685.

HATUA MUHIMU

Biblia ya Bedell haikupokewa vizuri na watu wengi. Hata hivyo, ilikuwa hatua mojawapo muhimu katika kuielewa vizuri Biblia, hasa kwa watu waliozungumza Kiairishi—kuanzia Ireland, Scotland na maeneo mengine mengi. Waliweza kutosheleza uhitaji wao wa kiroho kwa kusoma Neno la Mungu katika lugha yao ya asili.—Mathayo 5:3, 6.

“Tuliposoma Biblia ya Bedell tulisikia Neno la Mungu katika lugha yetu ya asili. Jambo hilo muhimu liliniwezesha mimi na familia yangu kujifunza kweli nzuri zilizo katika Maandiko.”

Biblia ya Bedell inawasaidia wale wanaopenda kweli leo kutosheleza uhitaji wao wa kiroho. Mtu mmoja anayezungumza Kiairishi, ambaye katika miaka ya karibuni amejifunza mambo ambayo Biblia inafundisha, alisema hivi: “Tuliposoma Biblia ya Bedell tulisikia Neno la Mungu katika lugha yetu ya asili. Jambo hilo muhimu liliniwezesha mimi na familia yangu kujifunza kweli nzuri zilizo katika Maandiko.”