Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jinsi ya Kushinda Hisia za Kutojiamini

Jinsi ya Kushinda Hisia za Kutojiamini

MTOTO mchanga hawezi kujilinda. Tulipozaliwa tulitegemea ulinzi kutoka kwa wazazi wetu. Tulipojifunza kutembea, tulikutana na watu tusiowafahamu ambao tuliwaona kuwa warefu sana kama majitu makubwa. Tuliwaogopa watu hao wazazi wetu walipokuwa mbali. Lakini tulihisi salama tuliposhika mkono wa mama au baba yetu.

Tulipokuwa watoto, hali yetu njema ilitegemea upendo na kitia moyo cha wazazi wetu. Tulipojua kuwa wazazi wetu wanatupenda, tulihisi tunathaminiwa. Walipotupongeza kwa sababu ya kufanya mambo mazuri, tulijiamini na kufanya vizuri zaidi.

Tulipoendelea kukua, marafiki wa karibu walifanya pia tujiamini. Tulifurahi kushirikiana nao, na walifanya tusiwe na hofu shuleni.

Mawazo hayo yanafafanua malezi yanayofaa ambayo mtoto anapaswa kupewa. Baadhi ya vijana wana marafiki wa karibu wachache sana, na watoto wengi hawapewi malezi yanayofaa na wazazi wao. “Kila mara ninapoona picha za familia ambazo hushirikiana kwa pamoja, huwa ninajiambia, ‘Ninatamani kweli ningefurahia hali hiyo nilipokuwa binti mdogo,’” anasema Melissa. * Huenda wewe pia unahisi hivyo.

MATATIZO YA KULELEWA BILA KUPENDWA

Labda ulikosa kujiamini ulipokuwa mtoto. Huenda haukupendwa au kutiwa moyo. Inawezekana unakumbuka wazazi wako wakigombana mara nyingi na hatimaye ndoa yao ikavunjika—huenda ulijilaumu kimakosa kuwa ulisababisha hali hiyo. Labda mmoja wa wazazi wako alikuwa akikutukana au kukupiga kikatili.

Mtoto aliyetendewa hivyo huenda akatendaje? Baadhi yao hutumia dawa za kulevya au kunywa pombe kupita kiasi wanapokuwa matineja. Wengine hujiunga na makundi ya wahalifu ili wahisi wanakubalika. Vijana hao huenda wakaanzisha uhusiano wa kimapenzi ili kupendwa. Lakini mara nyingi mahusiano hayo hayadumu, na yanapovunjika husababisha kutojiamini zaidi.

Matineja wasiojiamini ambao huepuka matatizo hayo makubwa huenda bado wakawa watu wazima ambao wanajihisi hawafai. Ana anaeleza, “Niliamini kabisa kwamba mimi sifai kitu, kwa kuwa hivyo ndivyo mama yangu alikuwa akiniambia kila wakati. Sikumbuki akinipongeza au kunijali.”

Malezi yetu sio jambo pekee linalofanya tusijiamini. Tunaweza kuhisi hivyo kutokana na talaka, matatizo ya uzee, au hata kuhangaikia mwonekano wetu. Hata sababu iwe nini, inaweza kutukosesha furaha na kuharibu uhusiano wetu na wengine. Tunaweza kufanya nini ili kushinda hisia hizo?

MUNGU ANATUJALI

Tunahitaji kujua kwamba kuna msaada. Mungu anaweza na anataka kutusaidia.

Huu ndio ujumbe ambao Mungu ametoa kupitia nabii wake Isaya: “Usitazame huku na huku, kwa maana mimi ni Mungu wako. Nitakutia nguvu. Nitakusaidia kwelikweli. Nitakushika kwelikweli kwa mkono wangu wa kuume wa uadilifu.” (Isaya 41:10, 13) Inafariji sana kujua kwamba kwa njia ya mfano Mungu anataka kutushika mkono! Hatuna haja ya kuwa na wasiwasi!

Biblia inaeleza kuhusu waabudu wa Mungu ambao walikuwa na wasiwasi lakini walijifunza kuushika mkono wa Mungu. Hana, mama yake Samweli, alihisi hafai kwa kuwa asingeweza kuzaa mtoto. Mara nyingi alidhihakiwa kwa sababu ya kuwa tasa. Mwishowe, Hana alipoteza hamu ya kula na alilia mara nyingi. (1 Samweli 1:6, 8) Hata hivyo, baada ya kummiminia Mungu hisia zake, alianza kuhisi vizuri.—1 Samweli 1:18.

Nyakati nyingine, mtunga-zaburi Daudi aliogopa. Kwa miaka mingi, Mfalme Sauli alijaribu kumwinda. Daudi aliepuka kuuawa mara kadhaa, na alihisi amelemewa na matatizo yake. (Zaburi 55:3-5; 69:1) Licha ya hali hizo, aliandika hivi: “Katika amani nitajilaza na kulala usingizi, kwa maana wewe peke yako, Ee Yehova, hunifanya nikae kwa usalama.”—Zaburi 4:8.

Hana na Daudi walimmiminia Yehova hisia zao, naye aliwategemeza. (Zaburi 55:22) Tunawezaje kuwaiga?

NJIA TATU ZA KUKUFANYA UJIAMINI ZAIDI

1. Jifunze kumtegemea Yehova akiwa Baba.

Yesu alitusihi tumjue Baba yake, “Mungu wa pekee wa kweli.” (Yohana 17:3) Mtume Paulo alituhakikishia kuwa Mungu “hayuko mbali sana na kila mmoja wetu.” (Matendo 17:27) Yakobo alisema, “Mkaribieni Mungu, naye atawakaribia ninyi.”—Yakobo 4:8.

Kujua kwamba tuna Baba wa mbinguni anayetupenda na kutujali ni hatua muhimu ya kushinda wasiwasi. Ni kweli kwamba huenda ikachukua muda mrefu kumtumaini kiasi hicho, lakini wengi wameona kwamba kufanya hivyo husaidia sana. Caroline anasema hivi: “Yehova alipokuwa Baba yangu, nilipata mtu wa kumweleza hisia zangu za ndani. Jambo hilo lilifanya nipate nafuu kubwa!”

Rachel anasema hivi: “Yehova ndiye aliyenifanya nihisi napendwa wakati nilipoachwa peke yangu bila wazazi. Ningeweza kuongea naye na kumwomba anisaidie kupambana na matatizo yangu. Na alinisaidia.” *

2. Tafuta familia ya kiroho.

Yesu aliwafundisha wanafunzi wake kuonana kama ndugu na dada. Aliwaambia, “Ninyi nyote ni ndugu.” (Mathayo 23:8) Alitaka wanafunzi wake wa kweli wapendane na wawe familia kubwa ya kiroho.—Mathayo 12:48-50; Yohana 13:35.

Makutaniko ya Mashahidi wa Yehova hujaribu kwa unyoofu kuwa na uchangamfu na kutoa faraja. (Waebrania 10:24, 25) Wengi wameona kwamba mikutano ya kutaniko ni kama dawa inayotuliza ambayo huponya majeraha na mikwaruzo ya kihisia.

“Nilikuwa na rafiki wa pekee katika kutaniko letu, ambaye alielewa maumivu yangu,” anakumbuka Eva. “Alinisikiliza, alinisomea Biblia, na alisali pamoja nami. Alihakikisha siko peke yangu. Alinisaidia nijieleze na kupunguza mahangaiko yangu. Kwa sababu ya msaada wake, nilianza kujiamini zaidi.” Rachel anaongezea hivi: “Nilipata ‘mama na baba’ katika kutaniko. Walinifanya nihisi napendwa na niko salama.”

3. Waonyeshe wengine upendo na wema.

Kuwaonyesha wengine upendo na wema kunajenga urafiki wa kudumu. Yesu alisema hivi: “Kuna furaha zaidi katika kutoa kuliko ilivyo katika kupokea.” (Matendo 20:35) Bila shaka tutagundua kwamba kadiri tunavyowapenda wengine, ndivyo nao watakavyotupenda. Yesu aliwaambia wafuasi wake hivi: “Muwe na mazoea ya kuwapa watu, na watu watawapa ninyi.”—Luka 6:38.

Tutajiamini zaidi ikiwa tutapendwa na kuwapenda wengine. Kama Biblia inavyosema, “upendo haushindwi kamwe.” (1 Wakorintho 13:8) María anasema, “Ninajua kwamba baadhi ya maoni mabaya niliyo nayo kuhusu jinsi nilivyo si ya kweli. Ninashinda fikira hizo mbaya kwa kuwasaidia wengine na kusahau mambo yangu. Sikuzote ninaridhika ninapofanya jambo fulani kwa ajili ya wengine.”

KILA MTU ANAWEZA KUJIAMINI

Mambo yaliyotajwa hapo juu hayamfanyi mtu apate ahueni mara moja. Lakini yanaweza kubadili hali. Caroline anakiri hivi: “Bado sijiamini. Lakini sasa ninahisi nina thamani. Ninajua kuwa Mungu ananijali, na nina marafiki wengi wa karibu ambao pia hunifanya nijiamini.” Rachel anahisi hivyo pia. Anasema, “Pindi fulani ninalemewa na huzuni. Lakini nina ndugu na dada ambao ninaweza kuwaendea ili nipate ushauri, ambao hunisaidia nione mambo kwa njia nzuri. Na zaidi ya yote, nina Baba wa mbinguni ambaye ninazungumza naye kila siku. Mambo hayo yamefanya hali iwe nzuri.”

Biblia inaeleza kuhusu ulimwengu mpya unaokuja ambapo kila mtu atajiamini

Pia kuna suluhisho la kudumu. Biblia inaeleza kuhusu ulimwengu mpya unaokuja ambapo kila mtu atajiamini. Neno la Mungu linaahidi hivi: “Wataketi, kila mtu chini ya mzabibu wake na chini ya mtini wake, wala hakutakuwa na mtu yeyote anayewatetemesha.” (Mika 4:4) Wakati huo, hakuna mtu atakayetufanya tuhisi hatuko salama, wala hakuna mtu yeyote atakayetudhuru. Hata matukio yenye kuumiza sana ya wakati uliopita “hayatakumbukwa akilini.” (Isaya 65:17, 25) Mungu na mwana wake, Yesu Kristo, wataleta “uadilifu wa kweli.” Hatimaye kutakuwa na “utulivu na usalama.”—Isaya 32:17.

^ fu. 5 Majina yote yamebadilishwa.

^ fu. 21 Mashahidi wa Yehova huwafundisha Biblia bila malipo wale wanaotaka kumkaribia Mungu zaidi.