Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MSAADA KWA AJILI YA FAMILIA | VIJANA

Uchumba Unapovunjika

Uchumba Unapovunjika

KIKWAZO

“Nilifikiri kwamba nimepata mtu anayenifaa. Nilijiambia hivi: ‘Nitaishi naye milele.’ Hata hivyo, baada ya miezi miwili ya kuwa marafiki, nilihitaji kuvunja uhusiano pamoja naye. Sikuamini kwamba uhusiano huo ungevunjika baada ya muda mfupi!”—Anna. *

“Tulipendezwa na mambo yaleyale. Akilini mwangu ni kana kwamba tayari tulikuwa tumefunga ndoa. Hata hivyo, baada ya muda nilianza kugundua kwamba tunatofautiana sana. Nilivunja uhusiano huo nilipogundua kwamba ulikuwa na matatizo.”—Elaine.

Je, umewahi kuwa katika hali kama hiyo? Ikiwa ndivyo, makala hii itakusaidia kukabiliana nayo.

UNACHOPASWA KUJUA

Kuvunjika kwa uhusiano ni jambo linaloumiza hisia za wote hata za yule aliyevunja uhusiano huo. “Nilihisi vibaya sana!” anasema msichana anayeitwa Sarah, aliyevunja uhusiano wake na rafiki yake wa kiume baada ya miezi sita. “Pindi moja alikuwa sehemu ya maisha yangu na mipango yangu ya wakati ujao; baada ya muda mfupi mambo yalibadilika. Niliposikia nyimbo tulizozipenda sana zilinikumbusha pindi nzuri tulipokuwa pamoja. Nilipotembelea sehemu tulizozipenda niliumia kutokana na kumkosa. Nilihisi hivyo hata ingawa mimi ndiye niliyeomba kuvunja uhusiano naye!”

Ingawa kuvunja uhusiano huumiza, kunaweza kuwa jambo linalofaa. Elaine anasema hivi: “Ni kweli kwamba hungependa kuumiza hisia za mwenzako. Hata hivyo, baada ya muda unagundua kwamba hatimaye nyote wawili mtaumizwa kihisia ikiwa mtaendeleza uchumba wenye matatizo.” Sarah anakubaliana na hilo. Anasema hivi: “Nafikiri kwamba ikiwa hufurahii urafiki wenu, huenda hautakuwa na furaha hata baada ya kufunga ndoa naye, hivyo, kuvunja uhusiano ni jambo linalofaa.”

Kuvunja uhusiano hakumaanishi kwamba haufai. Kwa kawaida, lengo la uchumba ni kufikia uamuzi, na si wakati wote uamuzi huo ni ndoa. Ikiwa wewe au rafiki yako mna mashaka fulani ya msingi, huenda ikafaa kuvunja uchumba huo. Ikiwa hilo litatokea, kutofanikiwa kwa uchumba huo hakumaanishi kwamba wewe haufai. Unaweza kuendelea na maisha! Jinsi gani?

MAMBO UNAYOWEZA KUFANYA

Tambua uchungu. Elaine aliyenukuliwa mwanzoni anasema hivi: “Nilimpoteza rafiki yangu wa karibu.” Ni jambo la kawaida kuhuzunika unapovunja uhusiano na rafiki yako wa karibu. Kijana anayeitwa Adam, anasema hivi: “Uhusiano unapovunjika lazima utahisi uchungu kwa kiasi fulani hata kama unajua kwamba uamuzi huo ulikuwa unafaa.” Huenda ukahisi kama Mfalme Daudi anayetajwa katika Biblia. Aliandika hivi alipokuwa na huzuni: “Usiku kucha nafanya kitanda changu kilowane.” (Zaburi 6:6) Nyakati fulani, njia bora ya kushughulika na maumivu ni kukabiliana nayo na wala si kuyakimbia. Kutambua hisia zako kunaweza kuwa hatua ya kwanza ya kupona.—Kanuni ya Biblia: Zaburi 4:4.

Shirikiana na watu wanaokujali. Ni kweli kwamba huenda isiwe rahisi. Anna, aliyetajwa mwanzoni anasema hivi: “Mwanzoni, sikutaka kuonana na watu. Nilihitaji muda wa kutosha ili kupata nafuu na kufikiria kilichonipata.” Hata hivyo, baada ya muda, Anna aliona faida inayotokana na kushirikiana na rafiki wa karibu ambao wangemtia moyo. Anasema hivi: “Nina mtazamo unaofaa, kuvunjika kwa uhusiano hakunivunji moyo sana kama ilivyokuwa mwanzoni.” —Kanuni ya Biblia: Methali 17:17.

Jifunze kutokana na kilichotokea. Jiulize: ‘Je, hali hii niliyopitia imenisaidia kutambua mambo ninayohitaji kuboresha? Nitafanya nini ili kuboresha uhusiano mwingine nitakaoanzisha?’ Msichana anayeitwa Marcia anasema hivi: “Baada ya kipindi fulani cha wakati kupita, niliweza kuchanganua vizuri kilichotokea. Hata hivyo, nilihitaji kusubiri kuanzisha uhusiano mpaka nilipoweza kufanya uamuzi kwa usawaziko badala ya kusukumwa na hisia.” Adam, aliyetajwa mapema anahisi hivyo pia. Anasema hivi: “Ilinichukua mwaka mzima kukabiliana na uchungu unaotokana na kuvunjika kwa uhusiano. Ilichukua muda mrefu zaidi kujifunza kutokana na hali hiyo. Hali niliyopitia ilinifundisha mengi kunihusu, kuhusu wasichana, na mahusiano. Sasa, uchungu unaotokana na kuvunjika kwa uhusiano umepungua kwa kiasi kikubwa.”

Sali kuhusu mahangaiko yako. Biblia inasema kwamba Mungu “anawaponya wenye mioyo iliyovunjika, naye anafunga sehemu zao zenye maumivu.” (Zaburi 147:3) Ijapokuwa Mungu hatuchagulii mwenzi na wala si wa kulaumiwa ikiwa uchumba unavunjika, angependa uwe na hali njema. Mwambie hisia zako kupitia sala.—Kanuni ya Biblia: 1 Petro 5:7.

^ fu. 4 Majina katika makala hii yamebadilishwa.