Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAONI YA BIBLIA

Kazi

Kazi

Ingawa Biblia ni kitabu cha kale, kanuni zake zinafaa leo. Mambo ambayo Biblia ilisema kuhusu kazi yanatufaa leo kama ilivyokuwa wakati ilipoandikwa.

Ni mtazamo gani unaofaa kuhusu kazi?

WATU HUSEMA NINI?

Ili kufanikiwa katika soko la ajira lenye ushindani, lazima mtu atangulize kazi kuliko kitu kingine chochote. Mtazamo huo umewafanya wengine wazingatie sana kazi hivi kwamba wamepuuza familia na afya yao.

BIBLIA INASEMA NINI?

Biblia ina maoni yenye usawaziko kuhusu kazi. Inasifu bidii na kulaumu uvivu. (Methali 6:6-11; 13:4) Wakati huohuo, Biblia haitutii moyo kutumia wakati na nguvu zote katika kazi. Badala yake, inatutia moyo kuwa na pindi fulani za kupumzika. Andiko la Mhubiri 4:6 linasema hivi: “Konzi moja ya pumziko ni afadhali kuliko konzi mbili za kazi ngumu na kufuatilia upepo.” Hivyo, usifanye kazi kupita kiasi hivi kwamba ukapuuza familia au afya yako. Hakuna faida kufanya kazi na kuidhuru afya yako mwenyewe!

“Kwa mwanadamu hakuna jambo bora kuliko kwamba ale, naam, anywe na kuifanya nafsi yake ione mema kwa sababu ya kazi yake ngumu.”Mhubiri 2:24.

Ni kazi gani inayofaa?

WATU HUSEMA NINI?

Kazi nzuri ni ile yenye mshahara mnono. Maoni hayo, na tamaa ya kupata pesa kwa haraka, kumefanya baadhi ya watu wajiunge katika biashara zisizo halali na kufanya kazi zilizo kinyume na sheria.

Wengine wanaofuata falsafa kama vile, ‘fuata ndoto zako’ au ‘fanya kile upendacho’ na hivyo hukubali tu kazi zinazowavutia au kuwasisimua. Ikiwa kazi hiyo “hawaipendi” maishani mwao au haiwafanyi wasisimuke, huiona kuwa inachosha. Matokeo ni kwamba, wanakuwa na maoni yasiyofaa kuhusu kazi yao na hawaifanyi kwa bidii. Hata wanaweza kukataa kufanya kazi nyingine nzuri kwa sababu wanahisi kwamba kazi hiyo inawashushia heshima.

BIBLIA INASEMA NINI?

Biblia haiungi mkono kufanya kazi isiyohalali au inayodhuru wengine kwa njia yoyote. (Mambo ya Walawi 19:11, 13; Waroma 13:10) Kazi nzuri hunufaisha wengine na kutusaidia kudumisha “dhamiri njema.”—1 Petro 3:16.

Biblia hufundisha kwamba kazi inapaswa kutimiza kusudi linalofaa, yaani, si kutufurahisha tu bali kutusaidia kuishi na kutunza familia. Ingawa si vibaya kufurahia kazi yetu ya kuajiriwa, kazi hiyo haipaswi kuwa jambo muhimu sana maishani.

“Baba yangu ana shughuli nyingi. Mbali na kazi yake ya kimwili, ana madaraka mengine katika kutaniko tunalohudhuria tukiwa Mashahidi wa Yehova. Hata hivyo, baba ana sifa nzuri ya kufanya kazi kwa bidii. Hutimiza yote anayopaswa kufanya na bado hutumia wakati pamoja na mimi, dada na mama yangu. Ingawa mara nyingi baba yangu huwa na mambo ya kufanya, hutimiza yote kwa usawaziko.”—Alannah.

Ni kweli kwamba, kuongezeka kwa bei za bidhaa kunaweza kutufanya tuhangaikie jinsi ya kupata riziki, hata hivyo Biblia hututia moyo kuwa na kiasi. Inasema hivi: “Tukiwa na chakula na kitu cha kujifunika, tutaridhika na vitu hivyo.” (1 Timotheo 6:8) Maneno hayo hayamaanishi kwamba tunapaswa kuishi maisha ya kujinyima. Lakini tunahitaji kuona mambo kihalisi kuamua kile tunachoweza kununua na kuwa wenye usawaziko kuhusu vitu tunavyonunua.—Luka 12:15.

UNACHOWEZA KUFANYA

Uwe mwenye bidii katika kazi yako. Pendezwa kikweli na kazi yako. Hata ikiwa kazi unayofanya inaonekana kuwa ya hali ya chini au si kazi uliyopenda kufanya maishani, jitahidi kuboresha ustadi wako katika kazi hiyo. Kufanya kazi kwa bidii kutafanya uhisi kwamba umetimiza jambo fulani, na kuboresha ustadi wako katika kazi yako kunaweza kukuongezea uradhi.

Na wakati huohuo, uwe mwenye usawaziko. Furahia vipindi vya mapumziko na burudani. Pindi hizo hufurahisha hata zaidi baada ya kufanya kazi kwa bidii. Pia, kupata mahitaji ya lazima, hutufanya tujiheshimu na kuheshimiwa na wengine, kutia ndani watu wa familia.—2 Wathesalonike 3:12.

“Msihangaike kamwe na kusema, ‘Tutakula nini?’ au, ‘Tutakunywa nini?’ au, ‘Tutavaa nini?’ . . . Baba yenu wa mbinguni anajua mnahitaji vitu hivi vyote.”Mathayo 6:31, 32.