Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAONI YA BIBLIA

Uzinzi

Uzinzi

Ingawa uaminifu katika ndoa ni jambo linaloonwa kuwa muhimu, bado uzinzi unaendelea kuharibu familia nyingi.

Uzinzi ni nini?

WATU HUSEMA NINI?

Baadhi ya watu hawaoni kwamba ni kosa kufanya ngono nje ya ndoa, hasa kwa waume. Na wengine hawaoni ndoa kuwa muungano wa kudumu.

BIBLIA INASEMA NINI?

Katika Biblia, kwa kawaida uzinzi unatia ndani uhusiano wa kingono kati ya mtu aliyefunga ndoa yaani mume au mke na mtu mwingine ambaye si mwenzi wake wa ndoa. (Ayubu 24:15; Methali 30:20) Uzinzi ni chukizo machoni pa Mungu. Katika Israeli la kale adhabu ya kosa hilo ilikuwa kifo. (Mambo ya Walawi 18:20, 22, 29) Yesu alifundisha kwamba wafuasi wake ni lazima wajiepushe na uzinzi.— Mathayo 5:27, 28; Luka 18:18-20.

KWA NINI JAMBO HILO NI MUHIMU?

Wazinzi huvunja nadhiri waliyoweka kwa wenzi wao siku walipofunga ndoa. Hilo pia ni ‘kumtendea Mungu dhambi.’ (Mwanzo 39:7-9) Uzinzi unaweza kuwatenganisha kikatili watoto na wazazi. Zaidi ya hayo, Biblia huonya kwamba “Mungu atawahukumu . . . wazinzi.”— Waebrania 13:4.

“Ndoa na iheshimiwe kati ya wote, na kitanda cha ndoa kiwe bila unajisi.”Waebrania 13:4.

Je, uzinzi unavunja ndoa?

BIBLIA INASEMA NINI?

Biblia inamruhusu mtu aliyefunga ndoa kumtaliki mwenzi wake ikiwa tu mwenzi huyo amefanya uasherati. (Mathayo 19:9) Hilo humaanisha kwamba baada ya tendo la kukosa uaminifu katika ndoa, mwenzi asiye na hatia ana haki ya kuamua iwapo ataendelea kuishi na mwenzi asiye mwaminifu au kumpa talaka. Huu ni uamuzi wa mtu binafsi.—Wagalatia 6:5.

Kwa upande mwingine, Mungu anaona ndoa kuwa muungano wa kudumu. (1 Wakorintho 7:39) Mungu huchukia talaka, mtu anapodai talaka kwa sababu ndogo-ndogo, kama vile kutoridhishwa na mwenzi wake. Kwa hiyo, uamuzi kuhusu talaka haupaswi kuchukuliwa kwa urahisi.—Malaki 2:16; Mathayo 19:3-6.

“Mimi ninawaambia ninyi kwamba kila mtu anayemtaliki mke wake, isipokuwa kwa sababu ya uasherati, anamweka katika hali ya kuweza kufanya uzinzi.”Mathayo 5:32.

Je, uzinzi ni dhambi isiyosameheka?

BIBLIA INASEMA NINI?

Hapana. Biblia husema kwamba Mungu huwaonyesha rehema wale wote wanaotubu na kuacha dhambi—kutia ndani uzinzi. (Matendo 3:19; Wagalatia 5:19-21) Biblia inasimulia kuhusu wanaume na wanawake ambao waliacha kufanya uzinzi na baadaye wakawa rafiki za Mungu.—1 Wakorintho 6:9-11.

Rehema za Mungu zilionyeshwa katika kisa cha Mfalme Daudi wa Israeli la kale. Daudi alifanya uzinzi na mke wa mmoja wa maofisa wake wa jeshi. (2 Samweli 11:2-4) Biblia inaeleza wazi kwamba “jambo ambalo Daudi alikuwa amefanya likawa baya machoni” pa Mungu. (2 Samweli 11:27) Baada ya kupewa karipio, Daudi alitubu na Mungu akamsamehe. Hata hivyo, Daudi angeteseka kwa sababu ya matokeo ya matendo yake. (2 Samweli 12:13, 14) Mfalme mwenye hekima Sulemani baadaye aliandika hivi: “yeyote anayefanya uzinzi na mwanamke amepungukiwa moyoni.”—Methali 6:32.

MAMBO UNAYOWEZA KUFANYA

Ikiwa umefanya uzinzi, unahitaji kuomba msamaha kwa Mungu na mwenzi wako. (Zaburi 51:1-5) Jifunze kuchukia uzinzi kama Mungu. (Zaburi 97:10) Azimia kuepuka kutazama ponografia, kuwazia-wazia kuhusu ngono, kuchezea wengine kimahaba, au jambo lingine lolote linaloweza kufanya usitawishe upendo wa kimahaba kwa mtu mwingine ambaye si mwenzi wako wa ndoa.—Mathayo 5:27, 28; Yakobo 1:14, 15.

Ikiwa unaumia kwa sababu mwenzi wako amefanya uzinzi, uwe na uhakika kwamba Mungu anaelewa hisia zako. (Malaki 2:13, 14) Sali akupe faraja nyororo na mwongozo wake, naye “mwenyewe atakutegemeza.” (Zaburi 55:22) Ikiwa umeamua kumsamehe mwenzi wako na kuendeleza ndoa yenu, wote mnahitaji kujitahidi kujenga upya ndoa yenu.—Waefeso 4:32.

Nabii Nathani alimwambia hivi Daudi aliyetubu baada ya kufanya uzinzi: “Yehova naye ameacha dhambi yako ipite.”2 Samweli 12:13.