Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kitabu Kinachotegemeka—Sehemu ya 2

Ashuru na Historia ya Biblia

Kitabu Kinachotegemeka—Sehemu ya 2

Hii ni habari ya pili kati mfululizo wenye habari saba katika matoleo ya “Amkeni!” yenye kufuatana yanayozungumzia serikali saba kuu za ulimwengu zinazotajwa katika historia ya Biblia. Kusudi lake ni kuonyesha kwamba Biblia inategemeka na imeongozwa na roho ya Mungu na kwamba ujumbe wake unatoa tumaini kwamba mateso yanayosababishwa na utawala mkatili wa wanadamu yatakwisha.

WATU wa Mashariki ya Kati ya kale waliingiwa na baridi waliposikia neno Ashuru. Kulingana na kitabu cha Biblia cha Yona, nabii huyo alipopewa mgawo na Mungu ahubiri ujumbe wa hukumu huko Ninawi, mji mkuu wa Ashuru, alitoroka kuelekea upande mwingine! (Yona 1:1-3) Huenda alifanya hivyo kwa sababu Waashuru waliogopwa sana.

Historia Inayotegemeka

Nabii Nahumu wa Biblia alisema kwamba Ninawi lilikuwa “tundu la simba”na “jiji la umwagaji wa damu.” Aliongezea hivi: “Mawindo hayaondoki! Kuna sauti ya mjeledi na sauti ya mgongano wa gurudumu, na farasi anayetimua mbio na gari linalorukaruka. Mpanda-farasi, na kumetameta kwa upanga, na kumetameta kwa mkuki, na watu wengi waliouawa, na rundo kubwa la mizoga; wala hakuna mwisho wa maiti. Wanaendelea kujikwaa kati ya maiti zao.” (Nahumu 2:11; 3:1-3) Je, vitabu vya historia vinaunga mkono masimulizi hayo ya Biblia kuhusu Ashuru ya kale?

Kitabu Light From the Ancient Past kinasema kwamba Waashuru “walipigana kwa ustadi na ukatili, na waliwashinda adui zao kwa kutumia mbinu ya kuwaogopesha.” Maneno yanayofuata yanaonyesha jinsi mfalme Ashurnasirpal wa Pili wa Ashuru alivyojigamba kuwatendea wote waliompinga:

“Nilijenga nguzo kwenye lango la jiji lake, na kuwachuna ngozi wakuu wote waliokuwa wameasi, na nikafunika mnara huo kwa ngozi; wengine niliwatundika juu ya mnara, wengine nikawatundika juu ya miti kwenye mnara, . . . na nilikata miguu na mikono ya maofisa, wale maofisa wa kifalme waliokuwa wameasi. . . . Nikachoma kwa moto mateka wengi miongoni mwao, nami nikachukua mateka wengi walio hai.” Wachimbuzi wa vitu vya kale walipochimbua majumba ya kifalme ya Ashuru, walipata kuta zilizorembeshwa kwa michoro ya mateka wakitendewa kinyama.

Katika mwaka wa 740 K.W.K., Ashuru ilishinda Samaria, mji mkuu wa ufalme wa kaskazini wa Israeli, na kuwapeleka watu wake uhamishoni. Miaka minane baadaye, Ashuru ilishambulia Yuda. * (2 Wafalme 18:13) Mfalme Senakeribu wa Ashuru alimwagiza Mfalme Hezekia wa Yuda amlipe ushuru wa talanta 30 za dhahabu na 300 za fedha. Masimulizi ya Biblia yanasema kwamba ushuru huo ulilipwa. Hata hivyo, Senakeribu alisisitiza kwamba Yerusalemu, mji mkuu wa Yuda ujisalimishe kwake bila masharti yoyote.—2 Wafalme 18:9-17, 28-31.

Huko Ninawi, wachimbuzi wa vitu vya kale wamepata maandishi ya kihistoria ya Senakeribu yanayosimulia matukio hayohayo. Katika maandishi hayo yaliyoandikwa kwenye mche wa udongo wenye pembe sita, mfalme huyo alijigamba hivi: “Kwa habari ya Hezekia Myahudi, yeye hakujiweka chini ya nira yangu, nilizingira miji 46 kati ya miji yake iliyokuwa imara, ambayo ilikuwa na kuta na ngome, na vijiji vidogo visivyo na hesabu vilivyokuwa karibu, na kushinda (miji na vijiji hivyo) . . . Nilimfanya [Hezekia] awe mfungwa kama ndege kizimbani huko Yerusalemu, makao yake ya kifalme.” Kisha Senakeribu alidai kwamba Hezekia alimpa “talanta 30 za dhahabu, talanta 800 za fedha, mawe yenye thamani, . . . (na) hazina zote zenye thamani,” akitia chumvi idadi ya talanta za fedha alizopokea.

Hata hivyo, ona kwamba Senakeribu hakusema kwamba alilishinda jiji la Yerusalemu. Hataji hata kidogo jinsi Mungu alivyoangamiza jeshi lake. Biblia inasema kwamba malaika wa Mungu aliwaua wanajeshi 185,000 wa Ashuru katika usiku mmoja. (2 Wafalme 19:35, 36) Msomi Jack Finegan anasema: “Tukizingatia majivuno yanayotajwa kwenye maandishi yote ya wafalme Waashuru, ni wazi kwamba Senakeribu hangeandika kamwe kuhusu ushinde kama huo.”

Unabii Unaotegemeka

Miaka 100 hivi kabla ya kuanguka kwa Milki ya Ashuru, Isaya alitangaza kwamba Yehova Mungu angewatoza hesabu washindi hao wenye kiburi kwa sababu ya kuwatendea watu wake kwa dharau. Yehova alisema hivi: ‘Nitatoza hesabu kwa ajili ya matunda ya dharau la moyo wa mfalme wa Ashuru na kwa ajili ya kujihesabia makuu kwa majivuno ya macho yake.’ (Isaya 10:12) Isitoshe, Nahumu, nabii wa Mungu alitabiri kwamba Ninawi lingeporwa, malango yake yangefunguliwa kwa ajili ya adui zake, na walinzi wake wangekimbia. (Nahumu 2:8, 9; 3:7, 13, 17, 19) Nabii Sefania wa Biblia aliandika kwamba jiji hilo lingekuwa “mahame yenye ukiwa.”—Sefania 2:13-15.

Unabii huo wa maangamizi ulitimia mwaka wa 632 K.W.K. Katika mwaka huo, ushirikiano wa majeshi ya Wababiloni na Wamedi ulishinda mji wa Ninawi na Milki ya Ashuru ikafikia mwisho wenye aibu. Maandishi ya Babiloni ya tukio hilo yanasema kwamba washindi “walibeba nyara nyingi za mji huo na hekalu” na kuacha mji wa Ninawi ukiwa “rundo la magofu.” Leo mahame yenye ukiwa ya Ninawi ni rundo la magofu yaliyo kwenye ukingo wa mashariki wa Mto Tigri, unaoelekeana na jiji la Mosul, huko Iraki.

Kuangamizwa kwa Ashuru pia kulichangia kutimizwa kwa unabii mwingine wa Biblia. Katika mwaka wa 740 K.W.K., Ashuru ilishinda ufalme wa yale makabila kumi na kuwapeleka Waisraeli uhamishoni. Karibu na wakati huo, Isaya, nabii wa Mungu alitabiri kwamba Yehova ‘atamvunja Mwashuru,’ ‘atamkanyagia chini,’ na kuwarudisha Waisraeli katika nchi yao. Isaya aliandika hivi: “Mabaki ya watu wake watakaobaki kutoka Ashuru . . . , [Mungu] atawakusanya pamoja.” Hivyo ndivyo ilivyotukia miaka 200 hivi baadaye!—Isaya 11:11, 12; 14:25.

Ahadi Yenye Kutegemeka

Muda mrefu kabla ya kuanguka kwa Ninawi, wakati ambapo bado wafalme wake waliwatia hofu maadui zao, Isaya alitabiri kuhusu kuja kwa mtawala tofauti kabisa. Aliandika hivi: “Kuna mtoto ambaye amezaliwa kwetu, kuna mwana ambaye tumepewa; na utawala wa ukuu utakuwa juu ya bega lake. Naye ataitwa . . . Mkuu wa Amani. Hakutakuwa na mwisho kwa habari ya wingi wa huo utawala wa kifalme na kwa amani, juu ya kiti cha ufalme cha Daudi na juu ya ufalme wake ili kuufanya imara na kuutegemeza kwa njia ya haki na kwa njia ya uadilifu, kuanzia sasa na kuendelea mpaka wakati usio na kipimo. Bidii ya Yehova wa majeshi itafanya hayo.”—Isaya 9:6, 7.

“Mkuu wa Amani,” Yesu Kristo, atatawala dunia yote. Zaburi 72:7, 8 inasema: “Katika siku zake aliye mwadilifu atachipuka, na wingi wa amani mpaka mwezi utakapokuwa haupo tena. Naye atakuwa na raia kutoka bahari mpaka bahari na kutoka ule Mto [Efrati] mpaka miisho ya dunia.”

Kupitia huyo “Mkuu wa Amani” mwenye nguvu, Yehova Mungu atatimiza ahadi iliyo kwenye Zaburi 46:8, 9: “Njooni, tazameni matendo ya Yehova, jinsi ambavyo ameweka matukio ya kushangaza duniani. Anakomesha vita mpaka kwenye mwisho wa dunia. Upinde anauvunja na kuukata mkuki vipande-vipande; magari ya kukokotwa anayateketeza motoni.”

Kama mwanzo wa utimizo wa unabii huo wa Biblia, Mashahidi wa Yehova wana programu ya elimu ya Biblia ya kuwafundisha watu njia za amani kama Yesu alivyofanya. Kwa kweli, unabii huu ulioandikwa kwenye Isaya 2:4 hautatimizwa na wanadamu bali na Mungu mwenyewe: “Watafua panga zao ziwe majembe na mikuki yao iwe miundu. Taifa halitainua upanga juu ya taifa, wala hawatajifunza vita tena.” Hata hivyo, leo ulimwengu na watawala wake hutumia matrilioni ya dola kila mwaka katika miradi ya kijeshi!

Historia yake na unabii wake sahihi hufanya Biblia iwe kitabu cha pekee, na kuwaonyesha watu wanyoofu wanaotafuta kweli kwamba kwa kweli ni kitabu kinachoweza kutegemeka. Habari inayofuata katika mfululizo huu itazungumzia Babiloni la kale, mji mkuu wa serikali kubwa ya tatu katika historia ya Biblia.

^ fu. 9 Baada ya utawala wa Mfalme Sulemani, taifa la Israeli lenye makabila 12 liligawanyika. Makabila ya Yuda na Benyamini yalifanyiza ufalme wa kusini; na yale makabila mengine kumi yakafanyiza ufalme wa kaskazini. Yerusalemu ulikuwa mji mkuu wa ufalme wa kusini, na Samaria ukawa mji mkuu wa ufalme wa kaskazini.