Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kitabu Kinachotegemeka​—Sehemu ya 3

Babiloni na Historia ya Biblia

Kitabu Kinachotegemeka​—Sehemu ya 3

Hii ni habari ya tatu kati ya mfululizo wenye habari saba katika matoleo ya “Amkeni!” yenye kufuatana yanayozungumzia serikali saba kuu za ulimwengu zinazotajwa katika historia ya Biblia. Kusudi lake ni kuonyesha kwamba Biblia inategemeka na imeongozwa na roho ya Mungu na ujumbe wake unatoa tumaini kwamba mateso yanayosababishwa na utawala mkatili wa wanadamu yatakwisha.

JIJI la Babiloni ya kale lililokuwa kwenye bonde lenye rutuba kilomita 80 hivi kusini ya jiji la kisasa la Baghdad, lilikuwa lenye kupendeza sana. Likiwa limezungukwa na kuta mbili kubwa na handaki, Babiloni lilionekana kuwa lisiloweza kushindwa. Jiji hilo lilijulikana sana kwa mahekalu yake ya kifahari, bustani zenye kuning’inia, na minara ya hekalu. Kwa kuwa Babiloni lilikuwa moja ya majiji makuu zaidi ya kale, limeitwa jiji la maajabu.

Katika Biblia, linajulikana kama “Bimkubwa wa Falme” na lilikuwa mji mkuu wa serikali kuu ya tatu katika historia ya Biblia. (Isaya 47:5) Kama vile tu milki za Misri na Ashuru zilizokuwepo kabla yake, Milki ya Babiloni pia ilitimiza fungu muhimu katika historia ya Biblia, na hilo linatuwezesha kulinganisha yale ambayo Biblia inasema na yale ambayo vitabu vya historia vinasema.

Historia Inayotegemeka

Kitabu cha Biblia cha Danieli kinatueleza kwamba mwanamume fulani anayeitwa Belshaza alikuwa mtawala wa Babiloni wakati mmoja. (Danieli 5:1) Hata hivyo, vitabu fulani vya kihistoria vinaeleza kwamba ingawa Belshaza alikuwa mwenye mamlaka, hakuwa mfalme hata wakati mmoja. Je, Biblia ilikuwa imekosea? Wachimbuaji wa vitu vya kale wamefukua silinda za udongo katika magofu ya Uru huko Mesopotamia. Silinda moja ilikuwa na bamba lenye maandishi yaliyotia ndani sala iliyotolewa na mfalme wa Babiloni Nabonido kwa niaba ya “Bel-sar-ussur [anayejulikana pia kama Belshaza] mwanangu mkubwa.” Uchunguzi uliofanywa baadaye ulionyesha kwamba Belshaza “alitawala kwa niaba ya baba yake kwa zaidi ya nusu ya kipindi cha utawala wa baba yake, ambapo wakati huo cheo chake kilikuwa sawa na kile cha mfalme” kinaeleza kitabu New Bible Dictionary.

Historia pia inaonyesha kwamba Babiloni la kale lilikuwa jiji lenye dini sana, likiwa limejaa matendo ya unajimu na uaguzi. Kwa mfano, katika Ezekieli 21:21, tunasoma kwamba mfalme wa Babiloni alifanya uaguzi ili ajue ikiwa angelivamia Yerusalemu. Biblia inasema kwamba mfalme huyo ‘alitazama ndani ya ini.’ Kwa nini alifanya hivyo? Wababiloni walitumia kiungo hicho ili kutafuta ishara za bahati. Kitabu Mesopotamian Astrology kinasema kwamba kwenye eneo moja tu la Babiloni la kale, wachimbuaji wa vitu vya kale walipata “sanamu 32 za maini [zilizotengenezwa kwa udongo], zote zikiwa na maandishi” ya ishara za bahati.

Nelson Glueck mchimbuaji maarufu wa vitu vya kale alisema hivi wakati mmoja: “Kwa miaka 30 nimefanya kazi ya kuchimbua nikiwa nimeshika Biblia kwenye mkono mmoja na sepetu kwenye mkono ule mwingine, na nimegundua kwamba Biblia haijawahi kukosea inapozungumzia mambo ya kihistoria.”

“Kwa miaka 30 nimefanya kazi ya kuchimbua . . . , na nimegundua kwamba Biblia haijawahi kukosea inapozungumzia mambo ya kihistoria.”—Nelson Glueck

Unabii Unaotegemeka

Ungesema nini ikiwa mtu angekuambia kwamba mji fulani mkuu—kama vile Dar-es-salaam, Kinshasa, au Nairobi—utaharibiwa na kuachwa ukiwa? Huenda ukawa na shaka. Hivyo ndivyo ilivyokuwa kuhusiana na Babiloni la kale. Miaka 200 hivi mapema, katika mwaka wa 732 K.W.K., Yehova Mungu alimwongoza nabii Mwebrania Isaya kuandika unabii kuhusu kuharibiwa kwa Babiloni. Aliandika hivi: “Babiloni, lile pambo la falme, . . . litakuwa kama wakati Mungu alipoangamiza Sodoma na Gomora. Hatakaliwa kamwe, wala hatakuwa na makao kwa kizazi baada ya kizazi.”—Isaya 13:19, 20.

Lakini kwa nini Mungu alitabiri kuhusu kuharibiwa kwa Babiloni? Katika mwaka wa 607 K.W.K., majeshi ya Babiloni yaliharibu Yerusalemu na kupeleka waokokaji hadi Babiloni, ambako walitendewa kwa ukatili sana. (Zaburi 137:8, 9) Mungu alitabiri kwamba watu wake wangevumilia mateso hayo makali kwa miaka 70 kwa sababu ya matendo yao maovu. Kisha Mungu angewakomboa na kuwarudisha katika nchi yao.—Yeremia 25:11; 29:10.

Kama tu Neno la Mungu la kinabii lilivyosema, katika mwaka wa 539 K.W.K.—kabla tu ya kile kipindi cha miaka 70 cha uhamisho wa Yuda kukamilika—jiji la Babiloni lililoonekana kuwa haliwezi kushindwa lilipinduliwa na majeshi ya Muungano wa Wamedi na Waajemi. Kisha jiji hilo likaja kuwa rundo la mabomoko—kama tu ilivyotabiriwa. Hakuna mwanadamu yeyote ambaye angeweza kutabiri tukio kama hilo la pekee sana. Ni wazi kwamba kutabiri, au kusema mambo kimbele, humtofautisha kabisa Mtungaji wa Biblia—yule Mungu wa kweli, Yehova—na miungu mingine.—Isaya 46:9, 10.

Tumaini Lenye Kutegemeka

Pia kuna unabii mwingine ambao unatimizwa leo. Unabii huo unahusisha Mfalme Nebukadneza wa Babiloni na ndoto aliyoota kuhusu sanamu kubwa sana. Mwili huo ulikuwa umegawanywa katika sehemu tano—kichwa, mikono, viuno, miguu, na nyayo—na kila sehemu ilikuwa imetengenezwa kwa chuma tofauti. (Danieli 2:31-33) Sehemu hizo za chuma ziliwakilisha mfuatano wa serikali au falme kuanzia na ile ya Babiloni na kuendelea hadi kufikia Serikali Kuu ya Ulimwengu ya Uingereza na Marekani, ambayo ndiyo ya saba katika historia ya Biblia.—Danieli 2:36-41.

Danieli anafunua kwamba nyayo za miguu na vidole vya sanamu hiyo vilifanyizwa kwa vifaa tofauti. Vifaa gani? Chuma safi kilibadilishwa na mchanganyiko wa udongo mbichi na chuma. Danieli alimweleza hivi Nebukadneza: “Na kama ulivyoona chuma kimechanganyikana na udongo mbichi, watachanganyikana na uzao wa wanadamu; lakini hawatashikamana pamoja, huyu na yule, kama vile chuma kisivyochanganyikana na udongo uliofinyangwa.” (Danieli 2:43) Ndiyo, chuma na udongo haviwezi ‘kushikamana pamoja.’ Hilo linafafanua kwa usahihi ulimwengu wa kisiasa tunamoishi leo!

Danieli pia anafunua tukio lingine muhimu. Katika ndoto yake, Mfalme Nebukadneza aliona jiwe lililokatwa kutoka kwa mlima mkubwa. Jiwe hilo liliinuliwa, “nalo likaipiga sanamu hiyo juu ya nyayo zake za chuma na za udongo uliofinyangwa, likaziponda.” (Danieli 2:34) Hilo linamaanisha nini? Danieli anajibu hivi: “Katika siku za wafalme hao [wakati wa utawala wa serikali kuu ya mwisho ya ulimwengu], Mungu wa mbinguni atausimamisha ufalme ambao hautaharibiwa kamwe. Na ufalme huo hautapewa watu wengine wowote. Utazivunja na kuzikomesha falme hizi zote, nao utasimama mpaka wakati usio na kipimo.” (Danieli 2:44) Unabii huo ulirejelea Ufalme unaotofautiana kabisa na serikali nyingine za wanadamu. Mfalme wa Ufalme huo ni Yesu Kristo, yule Masihi. Kama ilivyotajwa katika habari zilizotangulia za mfululizo huu, Yesu atamponda Shetani na wafuasi wake wote, wawe wanadamu au malaika waovu, na hivyo kuleta amani na upatano ulimwenguni pote.—1 Wakorintho 15:25.