Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Habari Kuu

Je, Yesu Alikuwa Mtu Halisi?

Je, Yesu Alikuwa Mtu Halisi?

HAKUWA mtu tajiri wala mashuhuri. Hakuwa na nyumba yake mwenyewe. Hata hivyo, mafundisho yake yamewachochea mamilioni ya watu. Je, kweli Yesu Kristo alikuwa mtu halisi? Watu mashuhuri walioishi zamani na sasa wanasema nini?

  • Michael Grant, mwanahistoria na mchunguzi wa maendeleo ya jamii za kale, alisema hivi: “Ikiwa tunachunguza maandishi ya Agano Jipya, kwa kutumia kanuni ileile ambayo tunatumia kuchunguza maandishi mengine ya kale ya kihistoria, hatuwezi kupinga kwamba Yesu alikuwa mtu halisi, kama vile tusivyoweza kutilia shaka kuwapo kwa watu wengine mashuhuri.”

  • Rudolf Bultmann, profesa wa masomo ya Agano Jipya, alisema hivi: “Shaka yoyote kwamba Yesu hakuwa mtu halisi haina msingi na haifai. Hakuna anayeweza kutilia shaka kwamba Yesu alikuwa mtu halisi kutokana na ushahidi wa kihistoria unaopatikana katika jamii [ya Wakristo] ya Wapalestina wa kale.”

  • Will Durant, mwanahistoria, mwandishi, na mwanafalsafa, aliandika hivi: “Haingewezekana kwa Wanaume wachache [waandikaji wa Injili] wa kizazi kimoja kuandika habari kuhusu mtu yuleyule mwema, mwenye cheo cha juu, na mwenye uvutano mkubwa katika jamii, huo ungekuwa muujiza mkubwa kuliko miujiza mingine iliyo katika Injili.”

  • Albert Einstein, mwanafizikia mzaliwa wa Ujerumani na Myahudi alieleza hivi: “Mimi ni Myahudi, lakini ninavutiwa sana na mfano mzuri wa Mnazareti.” Alipoulizwa ikiwa anaamini kwamba Yesu alikuwa mtu halisi, alijibu hivi: “Bila shaka! Hakuna mtu anayeweza kusoma Injili na akose kuamini kwamba Yesu alikuwa mtu halisi. Maneno yake yalifunua utu wake. Hakuna simulizi lingine lililo na mambo halisi kama hayo.”

    “Hakuna mtu anayeweza kusoma Injili na akose kuamini kwamba Yesu alikuwa mtu halisi.”—Albert Einstein

HISTORIA INAFUNUA NINI?

Masimulizi kuhusu maisha na huduma ya Yesu yameandikwa katika Biblia, nayo hujulikana kuwa Injili, na yanaitwa kwa majina ya waandikaji wake, yaani, Mathayo, Marko, Luka, na Yohana. Kwa kuongezea, vyanzo vingine vya habari visivyo vya Kikristo vinaeleza kuhusu Yesu.

  • TACITUS

    (c. 56-120 W.K., au Wakati wa Kawaida) Tacitus anajulikana kuwa mmoja kati ya wanahistoria mashuhuri zaidi wa Roma ya kale. Maandishi Yake yanaeleza kuhusu Milki ya Roma kuanzia mwaka wa 14 W.K. hadi 68 W.K. (Yesu alikufa mwaka wa 33 W.K.) Tacitus aliandika kwamba moto mkubwa ulipoharibu Roma mwaka wa 64 W.K., ilidhaniwa kwamba Maliki Nero alihusika. Hata hivyo, Tacitus aliandika kwamba “ili kumaliza uvumi huo,” Nero aliwalaumu Wakristo kuhusika na moto huo. Kisha, Tacitus alisema: “Kristo, ambaye ni chanzo cha jina [Mkristo], alihukumiwa kifo katika utawala wa Tiberio, kupitia hukumu iliyotolewa na mtesaji Pontio Pilato.”—Annals, XV, 44.

  • SUETONIUS

    (c. 69–a. 122 W.K.) Katika kitabu chake Lives of the Caesars, mwanahistoria huyo Mroma alirekodi matukio ya utawala wa maliki wa kwanza wa Roma hadi maliki wa 11. Katika sehemu anayoeleza kuhusu maliki Claudius anataja vurugu iliyotokea miongoni mwa Wayahudi huko Roma, ambayo huenda ilisababishwa na bishano kumhusu Yesu. (Matendo 18:2) Suetonius aliandika hivi: “Kwa kuwa Wayahudi walifanya vurugu mara kwa mara kwa kuchochewa na Kristo, [Claudius] aliwafukuza Roma.” (The Deified Claudius, XXV, 4) Ingawa dai lake kwamba Yesu alianzisha vurugu ni la uwongo, Suetonius aliamini kwamba Yesu alikuwa mtu halisi.

  • PLINI MDOGO

    (c. 61-113 W.K.) Mtungaji huyo Mroma na msimamizi wa Bithynia (sasa Uturuki) alimwandikia Maliki Mroma Trajan jinsi ya kushughulika na Wakristo katika eneo lake. Plini alisema kwamba aliwalazimisha Wakristo wakane imani yao, na aliwaua wote waliokataa kufanya hivyo. Alifafanua hivi: “Wale . . . waliorudia kiapo kwa Miungu [ya kipagani], na kuabudu sanamu yako kwa kufukiza ubani na divai . . . na ambao mwishowe walimlaani Kristo . . . , niliwaachia huru.”—Pliny—Letters, Book X, XCVI.

  • FLAVIO YOSEFO

    (c. 37-100 C.E.) Mwanahistoria na kuhani huyo Myahudi alisema kwamba Anasi, kuhani mkuu Myahudi ambaye alikuwa na uvutano mkubwa wa kisiasa, “aliwashawishi mahakimu wa Sanhedrini [mahakama kuu ya Wayahudi] na kumleta mbele yao Yakobo, ndugu ya Yesu aliyeitwa pia Kristo.”—Jewish Antiquities, XX, 200.

  • TALMUD

    Mkusanyo huo wa maandishi ya kirabi ya Kiyahudi ya kuanzia karne ya tatu hadi sita W.K., huonyesha kwamba hata maadui wa Yesu waliamini kwamba alikuwa mtu halisi. Sehemu moja ilisema hivi: “Yesu Mnazareti alitundikwa mtini siku ya Pasaka,” hilo ni sahihi kihistoria. (Babylonian Talmud, Sanhedrin 43a, Munich Codex; soma Yohana 19:14-16) Sehemu nyingine inaeleza hivi: “Tusiwafundishe watoto katika njia itakayowaletea aibu hadharani kama Mnazareti,” jina ambalo nyakati zote lilirejelea Yesu.—Babylonian Talmud, Berakoth 17b, footnote, Munich Codex; soma Luka 18:37.

UTHIBITISHO WA BIBLIA

Vitabu vya Injili vina masimulizi mengi kuhusu maisha na huduma ya Yesu, kutia ndani mambo hususa kuhusu watu, mahali, na nyakati, huo ni uthibitisho mwingi wa kihistoria. Kwa mfano, Luka 3:1, 2 inatusaidia kuelewa wakati hususa ambao Yohana Mbatizaji, mtangulizi wa Yesu, alianza rasmi kazi yake.

“Andiko lote limeongozwa na roho ya Mungu.”—2 Timotheo 3:16

Luka aliandika hivi: “Katika mwaka wa kumi na tano wa kumiliki kwa Kaisari Tiberio, Pontio Pilato alipokuwa gavana wa Yudea, na Herode alipokuwa mtawala wa wilaya ya Galilaya, lakini Filipo ndugu yake alikuwa mtawala wa wilaya wa nchi ya Iturea na Trakoniti, na Lisania alikuwa mtawala wa wilaya ya Abilene, katika siku za mkuu wa makuhani Anasi na za Kayafa, tangazo la Mungu likamjia Yohana mwana wa Zekaria nyikani.” Habari hizo, zinatusaidia kuthibitisha kwamba ‘tangazo la Mungu lilimjia Yohana’ mwaka wa 29 W.K.

Wanahistoria wanawajua vema viongozi hao saba ambao Luka aliwataja. Wakati fulani, kuna watu ambao walitilia shaka iwapo Pontio Pilato na Lisania walikuwa watu halisi. Lakini shaka hiyo haikuwa na msingi wowote. Hati za kale zenye majina ya maofisa hao wawili ziligunduliwa, hivyo kuthibitisha kuwa maandishi ya Luka ni sahihi. *

KWA NINI MAMBO HAYO NI MUHIMU?

Yesu alifundisha watu kuhusu Ufalme wa Mungu, serikali ya ulimwengu

Ni muhimu kutambua kwamba Yesu alikuwa mtu halisi kwa sababu mafundisho yake ni muhimu. Kwa mfano, Yesu aliwafundisha watu jinsi ya kuwa na furaha na kuishi maisha yenye kuridhisha. * Pia, aliahidi wakati ambapo wanadamu wataishi kwa amani ya kweli, usalama na umoja chini ya serikali ya ulimwengu, inayoitwa “Ufalme wa Mungu.”—Luka 4:43.

Jina “Ufalme wa Mungu” linafaa kwa sababu serikali hiyo ya ulimwengu itatimiza enzi ya Mungu duniani. (Ufunuo 11:15) Katika sala ya mfano, Yesu alitaja jambo hilo waziwazi aliposema: “Baba yetu uliye mbinguni, . . . Ufalme wako na uje. Mapenzi yako na yatendeke duniani.” (Mathayo 6:9, 10) Ufalme huo utawafanyia nini wanadamu? Fikiria mambo yafuatayo:

Huenda baadhi ya watu wakafikiri kwamba ahadi hizo ni ndoto tu. Lakini itakuwa ndoto kutumaini jitihada za wanadamu kutimiza mambo hayo! Fikiria jambo hili: Licha ya maendeleo makubwa katika nyanja ya elimu, sayansi, na teknolojia, mamilioni ya watu hawana usalama na wana hofu kuhusu wakati wao ujao. Na kila siku tunashuhudia hali mbaya ya uchumi, siasa, ukatili wa dini, na vilevile pupa na ufisadi. Naam, ukweli ni kwamba serikali za wanadamu zimeshindwa!—Mhubiri 8:9.

Kwa kumalizia, ni muhimu kuchunguza mambo yanayothibitisha kwamba Yesu alikuwa mtu halisi. * Andiko la 2  Wakorintho 1:19, 20 linasema: “Kwa maana hata ahadi za Mungu ziwe nyingi kadiri gani, zimekuwa Ndiyo kwa njia ya [Kristo].”

^ fu. 23 Hati ya kale yenye jina la “mtawala wa wilaya,” aliyeitwa Lisania ilipatikana. (Luka 3:1) Alitawala Abilene katika kipindi kilekile ambacho Luka alitaja.

^ fu. 25 Mfano wa mafundisho bora ya Yesu unapatikana katika Mathayo sura ya 5 hadi 7, ambayo huitwa Mahubiri ya Mlimani.

^ fu. 32 Ili kupata habari zaidi kuhusu Yesu na mafundisho yake, tembelea www.pr418.com/sw na tafuta kwenye MAFUNDISHO YA BIBLIA > MAJIBU YA MASWALI YA BIBLIA.