Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

NJIA YA MAISHA INAYOLETA FURAHA

Afya Nzuri na Ustahimilivu

Afya Nzuri na Ustahimilivu

UGONJWA WA KUDUMU AU ULEMAVU UNAWEZA KUATHIRI SANA MAISHA YA MTU. Mwanamume anayeitwa Ulf ambaye mwanzoni alikuwa mwenye afya nzuri, alisema hivi baada ya kupooza: “Nilishuka moyo sana. Niliishiwa nguvu na kupoteza ujasiri . . . Nilihisi maisha yangu yamefika mwisho.”

Kisa cha Ulf kinatukumbusha kwamba hakuna yeyote anayeweza kuilinda kikamili afya yake. Hata hivyo, kwa kiasi fulani tunaweza kuchukua hatua ili kujitunza. Lakini namna gani afya yetu ikizorota? Je, hilo linamaanisha hatuwezi kabisa kuwa na furaha? Kama tutakavyoona, sivyo hata kidogo. Acheni kwanza tuchunguze kanuni tunazoweza kufuata ili kuwa na afya nzuri.

UWE “MWENYE KIASI KATIKA MAZOEA.” (1 Timotheo 3:2, 11) Kuwa na zoea la kula au kunywa kupita kiasi kunadhuru afya yetu na pia kunaathiri hali yetu ya kiuchumi. “Usiwe miongoni mwa watu wanaokunywa divai nyingi mno, miongoni mwa wale wanaokula nyama kwa pupa, kwa maana mlevi na mlafi watakuwa maskini.”—Methali 23:20, 21.

USIUCHAFUE MWILI WAKO. “Acheni tujisafishe kila unajisi wa mwili na roho.” (2 Wakorintho 7:1) Watu huchafua miili yao kwa kutafuna au kuvuta tumbaku, au kwa kutumia vibaya kileo au dawa. Kwa mfano, Taasisi ya Kudhibiti na Kuzuia Magonjwa Nchini Marekani (CDC), inasema kwamba kuvuta sigara “husababisha magonjwa na ulemavu na kudhuru kila kiungo cha mwili.”

UONE MWILI NA UHAI WAKO KUWA ZAWADI ZENYE THAMANI. “Kupitia kwake [Mungu] tuko hai, tunatembea, na tunaishi.” (Matendo 17:28) Kutambua jambo hilo hutuchochea kuepuka kujihatarisha isivyo lazima iwe tuko kazini, tunaendesha chombo cha usafiri, au tunapokuwa katika burudani. Kwa nini ujisababishie ulemavu wa kudumu kwa sababu ya msisimko wa muda mfupi?

DHIBITI HISIA ZENYE MADHARA. Mwili na akili yako hufanya kazi kwa pamoja. Hivyo, jitahidi kuepuka mahangaiko yasiyo ya lazima, hasira isiyodhibitiwa, wivu, na hisia nyingine zenye madhara. Zaburi 37:8 inasema: “Acha hasira na uache ghadhabu.” Pia, Biblia inasema: “Msihangaike kamwe kuhusu kesho, kwa maana kesho itakuwa na mahangaiko yake yenyewe.”—Mathayo 6:34.

JITAHIDI KUDUMISHA MAWAZO CHANYA. Andiko la Methali 14:30 linasema: “Moyo mtulivu huupa mwili uzima.” Pia, Biblia inasema: “Moyo wenye shangwe ni dawa nzuri.” (Methali 17:22) Hilo ni jambo lililothibitishwa kisayansi. Daktari mmoja nchini Scotland alisema: “Ukiwa mwenye furaha, una uwezekano mdogo wa kupata magonjwa wakati ujao kwa kulinganisha na mtu asiye na furaha.”

UWE MWENYE USTAHIMILIVU. Kama Ulf aliyetajwa mwanzoni, huenda usiwe na la kufanya zaidi ya kuvumilia hali ngumu uliyo nayo. Lakini bado unaweza kupata mbinu za kukabiliana nayo. Baadhi ya watu huvunjika moyo kabisa, na hilo husababisha hali iwe mbaya zaidi. Andiko la Methali 24:10 linasema: “Ukivunjika moyo siku ya taabu, nguvu zako zitakuwa chache.”

Wengine huinuka tena baada ya kuwa wamevunjika moyo. Wanagundua njia za kukabiliana na hali yao. Hivyo ndivyo ilivyokuwa katika kisa cha Ulf. Alisema kwamba baada ya kusali sana na kutafakari ujumbe wenye kufariji wa Biblia, “alianza kuona mambo anayoweza kufanya badala ya vipingamizi.” Vilevile, kama ilivyo kwa wengi ambao hukabili hali ngumu, alijifunza kuwa mwenye huruma na kuelewa hisia za wengine, na hilo lilimchochea kuwaeleza wengine ujumbe wa Biblia unaofariji.

Steve, ni mtu mwingine ambaye alikabili hali ngumu sana. Alipokuwa na umri wa miaka 15, alianguka vibaya na akapooza kutoka shingoni hadi chini. Kufikia umri wa miaka 18, alikuwa ameanza kutumia mikono yake. Baadaye alienda chuo kikuu, na akiwa huko alianza kutumia dawa za kulevya na pombe na kujihusisha katika upotovu wa maadili. Hakuwa na tumaini lolote hadi alipoanza kujifunza Biblia, ambayo ilimsaidia kuwa na mtazamo mpya wa maisha na kumwezesha kushinda mazoea yake mabaya. Alisema: “Hali ya kujihisi sifai niliyokuwa nayo kwa muda mrefu sana iliisha. Sasa nina amani, furaha, na nimeridhika.”

Maelezo ya Steve na Ulf yanatukumbusha maneno ya Zaburi 19:7, 8: “Sheria ya Yehova ni kamilifu, hurudisha nguvu. . . . Maagizo kutoka kwa Yehova ni ya uadilifu, huufanya moyo ushangilie; amri ya Yehova ni safi, huyafanya macho yang’ae.”