Hamia kwenye habari

MISTARI YA BIBLIA YAFAFANULIWA

Yohana 16:33​—“Mimi Nimeushinda Ulimwengu”

Yohana 16:33​—“Mimi Nimeushinda Ulimwengu”

 “Nimewaambia mambo haya ili kupitia kwangu muwe na amani. Ulimwenguni mtapata dhiki, lakini jipeni moyo! Mimi nimeushinda ulimwengu.”—Yohana 16:33, Tafsiri ya Ulimwengu Mpya.

 “Hayo nimewaambieni mpate kuwa na amani ndani yangu. Ulimwenguni mnayo dhiki; lakini jipeni moyo; mimi nimeushinda ulimwengu.”—Yohana 16:33, Union Version.

Maana ya Yohana 16:33

 Kupitia maneno hayo, Yesu anawahakikishia wafuasi wake kwamba wanaweza kufanikiwa kumpendeza Mungu licha ya majaribu na upinzani wanaokabili.

 “Nimewaambia mambo haya ili kupitia kwangu a muwe na amani.” Sehemu inayofuata ya mstari huo inaonyesha kwamba kuwa na amani hiyo hakumaanishi mtu hatapatwa na matatizo. Badala yake ni amani ya moyoni na ya akilini. Amani hiyo ya ndani inawezekana “kupitia” kwa Yesu, aliyeahidi kutuma roho takatifu. “Msaidizi” huyo mwenye nguvu angewawezesha wanafunzi wa Yesu kufanikiwa licha ya hali zozote ngumu.—Yohana 14:16, 26, 27.

 “Ulimwenguni mtapata dhiki, lakini jipeni moyo!” Yesu alionyesha wazi kwamba wanafunzi wake wangekabili majaribu, kama vile ukosefu wa haki na mateso. (Mathayo 24:9; 2 Timotheo 3:12) Licha ya hayo, walikuwa na sababu ya ‘kujipa moyo.’—Yohana 16:33.

 “Mimi nimeushinda ulimwengu.” Hapa neno “ulimwengu” linarejelea jamii ya wanadamu wasio waadilifu waliotenganishwa na Mungu. b 1 Yohana 5:19 inasema: “Ulimwengu mzima unakaa katika nguvu za yule mwovu,” yaani, Shetani. Hivyo, watu katika “ulimwengu” huu, wanafikiri na kutenda kinyume na mapenzi ya Mungu.—1 Yohana 2:15-17.

 Shetani na ulimwengu wake walijaribu kumzuia Yesu asitimize mapenzi ya Mungu, ambayo yalitia ndani kuwafundisha wengine kumhusu Mungu na kutoa uhai wake mkamilifu kuwa fidia. (Mathayo 20:28; Luka 4:13; Yohana 18:37) Lakini Yesu hakuruhusu ulimwengu uathiri kufikiri kwake na kumfanya aache kumtumikia Mungu. Aliendelea kuwa mwaminifu hadi kifo. Hivyo, Yesu angeweza kusema kwamba ameushinda ulimwengu na kwamba Shetani, “mtawala wa ulimwengu” hakuwa na “uwezo” juu yake.—Yohana 14:30.

 Yesu alitumia mfano wake mwenyewe kuwaonyesha wafuasi wake kwamba wao pia wangeweza kuendelea kuwa waaminifu kwa Mungu hata utimilifu wao ulipojaribiwa. Ni kana kwamba Yesu alikuwa akiwaambia: “Ikiwa mimi ninaweza kuushinda ulimwengu, ninyi pia mnaweza.”

Muktadha wa Yohana 16:33

 Yesu alisema maneno hayo usiku kabla ya kifo chake. Akijua kwamba angekufa baada ya muda mfupi, alitumia nafasi hiyo ya mwisho kuwashauri mitume wake waaminifu. Aliwaambia kweli fulani muhimu: Hawatamwona tena, na watateswa, au hata kuuawa. (Yohana 15:20; 16:2, 10) Kwa kuwa maneno hayo yangewafanya mitume wake waogope, Yesu alimaliza kwa kuwaambia maneno ya Yohana 16:33 ili kuwatia moyo na kuwapa uhakikisho.

 Maneno na mfano wa Yesu unaweza kuwatia moyo wafuasi wake leo. Wakristo wote wanaweza kuendelea kuwa waaminifu kwa Mungu licha ya mateso.

a Maneno ya Kigiriki “kupitia kwangu” yanaweza pia kutafsiriwa “katika muungano nami.” Yanatokeza wazo kwamba wanafunzi wa Yesu wangeweza kufurahia amani kwa kuendelea kuwa na umoja naye.

b Neno “ulimwengu” linatumiwa kwa njia hiyo kwenye Yohana 15:19 na 2 Petro 2:5.