Hamia kwenye habari

MISTARI YA BIBLIA YAFAFANULIWA

2 Timotheo 1:7—“Mungu Hakutupa Roho ya Woga”

2 Timotheo 1:7—“Mungu Hakutupa Roho ya Woga”

 ““Kwa maana Mungu hakutupatia roho ya woga, bali roho ya nguvu na ya upendo na ya utimamu wa akili.”—2 Timotheo 1:7, Tafsiri ya Ulimwengu Mpya.

 “Maana Mungu hakutupa roho ya woga, bali ya nguvu na ya upendo na ya moyo wa kiasi.”—2 Timotheo 1:7, Union Version.

Maana ya 2 Timotheo 1:7

 Mungu anaweza kumsaidia mtu awe jasiri katika kufanya mema. Mungu hataki yeyote atende kwa woga, yaani, woga usiofaa unaomzuia mtu kufanya mambo yanayompendeza Mungu.

 Fikiria sifa tatu zinazotokana na Mungu zinazotajwa katika mstari huu ambazo zinaweza kutusaidia kushinda woga.

 “Nguvu.” Wakristo wamefaulu kumtumikia Mungu licha ya maadui hatari na hali ngumu. Hawajarudi nyuma kwa woga. (2 Wakorintho 11:23-27) Hilo linawezekanaje? Mtume Paulo alisema hivi: “Kwa mambo yote nina nguvu kupitia yule anayenipa nguvu.” (Wafilipi 4:13) Mungu anaweza kuwapa waabudu wake “nguvu zinazopita zile za kawaida” ili waweze kushinda changamoto zozote.—2 Wakorintho 4:7.

 “Upendo.” Kumpenda Mungu kwa dhati kunamsaidia Mkristo asimame imara na kufanya yaliyo sawa. Vivyo hivyo, kuwapenda wanadamu wengine kunamchochea Mkristo kutanguliza mahitaji ya wengine kabla ya mahitaji yake mwenyewe hata anapokabili upinzani au hatari. —Yohana 13:34; 15:13.

 “Utimamu wa akili.” Katika Biblia, utimamu wa akili unarejelea uwezo wa Mkristo wa kufanya maamuzi ya hekima yanayotegemea Biblia. Mtu aliye na utimamu wa akili anaweza kutenda kwa busara na usawaziko hata anapokabiliana na hali ngumu. Anaweza kufanya maamuzi yanayopatana na maoni ya Mungu, kwa kuwa anatambua kwamba uhusiano wake na Mungu ni muhimu zaidi kuliko jinsi watu wengine wanavyomwona.

Muktadha wa 2 Timotheo 1:7

 Mtume Paulo alimwandikia Timotheo, rafiki yake na mfanyakazi mwenzake, kitabu cha Biblia cha Timotheo ya Pili. Katika barua hiyo Paulo alimtia moyo kijana Timotheo aendelee kufanya kazi kwa bidii katika huduma. (2 Timotheo 1:1, 2) Huenda Timotheo alikuwa mwenye haya, na hilo lingeweza kumzuia kufanya yote ambayo angeweza katika kutaniko la Kikristo. (1 Timotheo 4:12) Lakini Paulo alimkumbusha Timotheo kwamba Timotheo alikuwa amepewa zawadi, yaani, mgawo wa pekee wa kutumikia kutaniko. Alimtia moyo Timotheo asisite kutumia mamlaka aliyopewa akiwa mwangalizi wa kutaniko, anapohubiri habari njema na anapovumilia mateso kwa ajili ya imani yake. —2 Timotheo 1:​6-8.

 Licha ya kwamba maneno hayo yaliandikwa kwa Timotheo, yanawahakikishia wote wanaotaka kumtumikia Mungu leo kwamba, Mungu atawapa msaada wanaohitaji ili wafaulu kumtumikia licha ya changamoto zozote.