Hamia kwenye habari

MISTARI YA BIBLIA YAFAFANULIWA

Wagalatia 6:9—“Hivyo, Tusichoke Katika Kutenda Mema”

Wagalatia 6:9—“Hivyo, Tusichoke Katika Kutenda Mema”

 “Basi tusife moyo katika kufanya mema, kwa maana kwa wakati unaofaa tutavuna ikiwa hatutachoka kabisa.”​—Wagalatia 6:9, Tafsiri ya Ulimwengu Mpya.

 “Hivyo, tusichoke katika kutenda mema, kwa kuwa tutavuna kwa wakati wake tusipokata tamaa.”​—Wagalatia 6:9, Neno: Maandiko Matakatifu.

Maana ya Wagalatia 6:9

 Mtume Paulo anawatia moyo Wakristo waendelee kufanya mema, au mambo mazuri machoni pa Mungu. Wakifanya hivyo wanaweza kuwa na uhakika kwamba Mungu atawathawabisha.

 “Basi tusife moyo.” Maneno hayo yanaweza kutafsiriwa kuwa “hivyo, tusichoke.” Maneno ya lugha ya awali yanaweza pia kutokeza wazo la kutovunjika moyo au kupoteza shauku yetu. Mtume Paulo alitumia neno “tusife” na hilo linamaanisha kwamba yeye pia alipambana na hali ya kuvunjika moyo pindi fulani.​—Waroma 7:21-24.

 “Kufanya mema,” au mambo mazuri kunatia ndani mambo yote ambayo Mkristo anapaswa kufanya katika utumishi wake kwa Mungu. Hilo linahusisha mambo yote ambayo mtu anafanya ili kuwasaidia waabudu wenzake na watu wengine pia.​—Wagalatia 6:10.

 “Kwa wakati unaofaa tutavuna ikiwa hatutachoka kabisa.” Paulo anawakumbusha wasomaji wake kwamba muda unahitajika ili kupata matokeo ya kufanya mema, kama tu mkulima anavyosubiri mimea ikue. Paulo anapozungumzia mavuno, anaunganisha wazo lililo katika mstari huu wa 9 na wazo lililo katika mstari wa 7 unaosema: “Maana lolote analopanda mtu, ndilo atakalovuna pia.” Kwa maneno mengine, Mkristo anapofanya mema machoni pa Mungu, atavuna thawabu kubwa, kutia ndani uzima wa milele.​—Waroma 2:6, 7; Wagalatia 6:8.

Muktadha wa Wagalatia 6:9

 Inaelekea mtume Paulo aliandika barua hii kuanzia mwaka wa 50 hadi 52 W.K kwa Wakristo walioishi Galatia. Kusudi lake lilikuwa kuwalinda Wakristo kutokana na uvutano wa watu waliodai kuwa Wakristo lakini ukweli ni kwamba watu hao walikuwa wakipotosha ukweli kumhusu Yesu. (Wagalatia 1:6, 7) Walimu hao wa uwongo walikuwa wakisema kwamba Wakristo walipaswa kutii Sheria ambayo Mungu alilipatia taifa la kale la Israeli kupitia Musa. (Wagalatia 2:15, 16) Paulo alieleza kwamba kusudi la Sheria lilikuwa limeshatimia hivyo waabudu wa kweli wa Mungu hawakuwa chini ya Sheria hiyo tena.​—Waroma 10:4; Wagalatia 3:23-25.

 Kwa hiyo, Paulo alipowatia moyo waabudu wenzake waendelee “kufanya mema” hakuwa akirejelea kutii Sheria ya Musa. Badala yake, aliwahimiza “[kutimiza] sheria ya Kristo,” ambayo inatia ndani yote ambayo Yesu alifundisha kuhusu kuwafanyia wengine mema.—Wagalatia 6:2; Mathayo 7:12; Yohana 13:34.

 Tazama video hii fupi inayoonyesha muhtasari wa kitabu cha Wagalatia.