Hamia kwenye habari

MISTARI YA BIBLIA YAFAFANULIWA

Waebrania 4:12—“Neno la Mungu Liko Hai na Linatenda Kazi”

Waebrania 4:12—“Neno la Mungu Liko Hai na Linatenda Kazi”

 “Kwa maana neno la Mungu liko hai nalo ni lenye nguvu na lina makali kuliko upanga wowote wenye makali pande mbili nalo huchoma hata kufikia kugawanya nafsi na roho, na viungo kutoka katika urojorojo, nalo linaweza kutambua fikira na makusudio ya moyo.”—Waebrania 4:12, Tafsiri ya Ulimwengu Mpya.

 “Neno la Mungu liko hai na linatenda kazi. Lina ukali kupita upanga ulio na makali sana na hukata hadi ndani yetu. Hukata ndani hadi sehemu ambayo nafsi na roho huwa zimeunganishwa pamoja. Neno la Mungu hukata hadi katikati ya maungio na mifupa yetu. Linahukumu mawazo na hisia ndani ya mioyo yetu.”—Waebrania 4:12, Agano Jipya: Tafsiri ya Kusoma-Kwa-Urahisi.

Maana ya Waebrania 4:12

 Ujumbe ambao Mungu amewapa wanadamu, ulioandikwa katika Biblia, una nguvu za kufunua mawazo na nia yetu. Ujumbe huo unaweza pia kuwasaidia watu wafanye mabadiliko mazuri maishani mwao.

 “Neno la Mungu liko hai.” Maneno “neno la Mungu” yanarejelea ahadi iliyotolewa na Mungu, au kusudi alilotangaza, lililoandikwa katika Biblia. a Sehemu muhimu ya kusudi hilo ni kwamba wanadamu watiifu waishi milele duniani kwa amani ya kweli na umoja.—Mwanzo 1:28; Zaburi 37:29; Ufunuo 21:3, 4.

 Neno la Mungu, au kusudi alilotangaza, “liko hai” katika maana gani? Kwanza kabisa, liko hai katika maana ya kwamba wale wanaoliamini wanapata tumaini na kusudi maishani. (Kumbukumbu la Torati 30:14; 32:47) Pia, liko hai kwa sababu Mungu aliye hai anafanya kazi ili kuhakikisha ahadi zake zinatimizwa kikamili. (Yohana 5:17) Tofauti na wanadamu, Mungu anapotoa ahadi hasahau kuihusu wala hawezi kushindwa kuitimiza. (Hesabu 23:19) Neno lake ‘halirudi kwake bila matokeo.’—Isaya 55:10, 11.

 “Neno la Mungu . . . ni lenye nguvu.” Maneno “ni lenye nguvu” yanaweza pia kutafsiriwa “linatenda kazi,” au “linatimiza chochote ambacho [neno hilo] limekusudiwa kutimiza.” Hivyo, chochote ambacho Yehova b Mungu anasema au kuahidi lazima litatimia. (Zaburi 135:6; Isaya 46:10) Kwa kweli, Mungu anaweza kutimiza ahadi zake katika njia ambazo hata hatuwezi kuwazia.—Waefeso 3:20. c

 Vilevile, neno la Mungu “ni lenye nguvu” kwa sababu linawasaidia wale wanaotambua thamani yake kufanya mabadiliko yanayofaa maishani mwao na pia katika nyutu zao. Mafundisho ya Mungu yanawaingia, yaani, yanaathiri kufikiri, maisha, na malengo yao. (Waroma 12:2; Waefeso 4:24) Katika maana hiyo, “neno la Mungu . . . pia linafanya kazi ndani” ya wale wanaokubali kuwa linatoka kwa Mungu.—1 Wathesalonike 2:13.

 “Neno la Mungu . . . lina makali kuliko upanga wowote wenye makali pande mbili.” Kwa njia ya mfano, neno la Mungu ni lenye makala kuliko upanga wowote uliotengenezwa na wanadamu kwa sababu ya uwezo wake wa kupenya ndani ya mioyo ya watu. Ujumbe wa Mungu unaweza kugusa fikira na mawazo ya mtu katika njia ambayo mafundisho ya wanadamu hayawezi. Hilo linaweza kuonekana katika maneno yanayofuata ya Waebrania 4:12.

 “Neno la Mungu . . . huchoma hata kufikia kugawanya nafsi na roho, na viungo kutoka katika urojorojo.” Katika Biblia, neno “nafsi” linaweza kurejelea jinsi mtu anavyoonekana kwa nje, na “roho” inaweza kurejelea jinsi mtu alivyo kikweli kwa ndani. (Wagalatia 6:18) Kwa njia ya mfano, “neno la Mungu” hupenya kufikia “urojorojo,” yaani, hisia na mawazo yetu ya ndani kabisa. Kwa kuwa mafundisho ya Yehova yanafunua jinsi tulivyo kikweli kwa ndani, mahali ambapo hakuna mwanadamu anaweza kuona, yanatuchochea kufanya mabadiliko mazuri maishani. Kufanya hivyo kunamletea Muumba wetu shangwe nasi pia tunapata shangwe.

 “Neno la Mungu . . . linaweza kutambua fikira na makusudio ya moyo.” Mawazo halisi ya mtu, makusudio au nia yake, hufunuliwa kwa kutegemea jinsi anavyotenda baada ya kulisikia neno la Mungu, kwa kuwa neno hilo linaweza kuathiri tabia au mwenendo wake. Kwa mfano, mtu anapotenda kwa njia inayofaa baada ya kulisikia neno la Mungu na kufanya mabadiliko maishani mwake, anaonyesha kwamba yeye ni mnyenyekevu na mnyoofu. Anataka kumfurahisha Muumba wake. Kwa upande mwingine, akijaribu kulikosoa neno la Mungu, huenda akawa anaonyesha sifa zisizofaa, kama vile kiburi au ubinafsi. Huenda anajaribu kutetea mwenendo ambao Mungu anachukia.—Yeremia 17:9; Waroma 1:24-27.

 “Kitabu kimoja cha marejeo kinaeleza kwamba neno la Mungu linatusaidia kufahamu hisia, mawazo, na nia yetu ya ndani kabisa.” Mungu anaweza kuona kila sehemu ya akili na moyo wetu na neno lake linaweza kufichua mawazo na hisia zetu. Waebrania 4:13 inasema hivi: “Vitu vyote viko uchi navyo vimefunuliwa wazi machoni pa yule ambaye tunapaswa kutoa hesabu kwake.”

Muktadha wa Waebrania 4:12

 Mtume Paulo aliandika kitabu cha Biblia cha Waebrania katika mwaka wa 61 W.K. hivi. Ilikuwa barua iliyoongozwa na roho ya Mungu kwa Wakristo Wayahudi walioishi Yerusalemu na Yudea.

 Katika sura ya 3 na 4, Paulo anaeleza jinsi mfano wa Waisraeli wa kale ni onyo kwa Wakristo. (Waebrania 3:8-12; 4:11) Yehova aliahidi kuwaokoa Waisraeli kutoka utumwani na kuwapeleka kwenye nchi ambayo ‘wangekaa kwa usalama.’ (Kumbukumbu la Torati 12:9, 10) Hata hivyo, Waisraeli waliotoka Misri walionyesha tena na tena kwamba hawakuwa na imani katika ahadi za Mungu na walivunja amri zake tena na tena. Kwa sababu hiyo, ‘hawakuingia katika pumziko la Mungu,’ yaani, hawakuwa na uhusiano wenye amani pamoja na Mungu. Badala yake, walikufa wakiwa nyikani. Ingawa wazao wao waliirithi Nchi ya Ahadi, wao pia walikosa kumtii Yehova tena na tena. Hatimaye, hilo lilifanya taifa hilo lipatwe na madhara makubwa.—Nehemia 9:29, 30; Zaburi 95:9-11; Luka 13:34, 35.

 Paulo anaeleza kwamba Wakristo wanapaswa kujifunza kutokana na mfano mbaya wa Waisraeli hao ambao hawakuwa waaminifu. Tofauti nao, sisi tunaweza kuingia katika pumziko la Mungu kwa kutii neno lake na kwa kuwa na imani kamili katika ahadi zake.—Waebrania 4:1-3, 11.

 Tazama video hii fupi uone muhtasari wa kitabu cha Waebrania.

a Katika Waebrania 4:12, maneno “neno la Mungu” hayarejelei Biblia kihususa. Hata hivyo, kwa kuwa Mungu alihakikisha kwamba ahadi zake ziliandikwa katika kitabu hicho, Waebrania 4:12 inaweza kumaanisha Biblia.

b Yehova ni jina la kibinafsi la Mungu. (Zaburi 83:18) Ona makala “Yehova Ni Nani?