Hamia kwenye habari

MISTARI YA BIBLIA YAFAFANULIWA

Mithali 16:3—“Mkabidhi BWANA Kazi Zako”

Mithali 16:3—“Mkabidhi BWANA Kazi Zako”

 “Mkabidhi Yehova lolote unalofanya, na mipango yako itafanikiwa.”​—Methali 16:3, Tafsiri ya Ulimwengu Mpya.

 “Mkabidhi BWANA kazi zako, na mawazo yako yatathibitika.”​—Mithali 16:3, Union Version.

Maana ya Methali 16:3

 Methali hii inawahakikishia wale wanaomwabudu Mungu wa kweli kwamba kazi zao au mipango yao itafanikiwa ikiwa wataonyesha kwamba wanamtegemea Mungu kwa kutafuta mwongozo wake na kuufuata.

 “Mkabidhi Yehova lolote unalofanya.” Kabla ya kufanya maamuzi, kwa unyenyekevu watumishi wa Yehova a humwomba mwongozo. (Yakobo 1:5) Kwa nini? Sababu moja ni kwamba, kwa kawaida wanadamu hawana uwezo wa kuamua mambo yatakayowapata maishani. (Mhubiri 9:11; Yakobo 4:13-15) Kwa kuongezea, huenda wasiwe na hekima inayohitajika ili kutekeleza mipango yao. Hivyo, kwa busara wengi humkabidhi Mungu mambo yao. Wanafanya hivyo wanapomwomba mwongozo na kutenda kulingana na mapenzi yake yaliyofunuliwa katika Neno lake Biblia.​—Methali 3:5, 6; 2 Timotheo 3:16, 17.

 Maneno “Mkabidhi BWANA b kazi zako” kihalisi yanamaanisha “mvingirishie BWANA kazi zako.” Kitabu kimoja cha marejeo kinasema kwamba maneno hayo yanaleta picha ya “mtu [ambaye] anatua mzigo aliokuwa amebeba na kuutwika mgongoni mwa mtu mwingine ambaye ana nguvu zaidi na uwezo wa kuubeba.” Wale ambao kwa unyenyekevu wanamtumaini Mungu wanaweza kuwa na uhakika kwamba atawasaidia na kuwategemeza.​—Zaburi 37:5; 55:22.

 Maneno “lolote unalofanya” hayamaanishi kwamba Mungu anakubaliana na mipango yote inayofanywa na watu na kuibariki. Ili watu wapate baraka za Yehova, ni lazima mipango yao ipatane na viwango vyake na pia mapenzi yake. (Zaburi 127:1; 1 Yohana 5:14) Mungu anabariki utii na si kutotii. Kwa kweli, yeye “huivuruga mipango ya waovu.” (Zaburi 146:9) Lakini kwa upande mwingine, anawasaidia wale wanaojitiisha kwake kwa kuheshimu viwango alivyoweka katika Biblia.​—Zaburi 37:23.

 “Na mipango yako itafanikiwa.” Tafsiri nyingine zinasema, “mawazo yako yatathibitika.” Katika Maandiko ya Kiebrania ambayo mara nyingi yanaitwa Agano la Kale, neno lililotafsiriwa “yatathibitika” linaleta maana ya kuweka msingi na mara nyingi linatumiwa kurejelea jinsi vitu ambavyo Mungu ameumba vilivyo imara. (Methali 3:19; Yeremia 10:12) Vivyo hivyo, Mungu atathibitisha kabisa mipango ya wale wanaofanya yaliyo mema machoni pake na atawasaidia kuwa na maisha yenye usalama, utulivu, na furaha.​—Zaburi 20:4; Methali 12:3.

Muktadha wa Methali 16:3

 Methali hii iliandikwa na Mfalme Sulemani, ambaye pia aliandika sehemu kubwa ya kitabu cha Methali. Sulemani alitunga maelfu ya methali kwa sababu alikuwa na hekima kutoka kwa Mungu. —1 Wafalme 4:29, 32; 10:23, 24.

 Katika sura ya 16, Sulemani anaanza kwa kumsifu Mungu kwa sababu ya hekima yake na anaonyesha jinsi Mungu anavyowachukia watu wenye kiburi. (Methali 16:1-5) Sura hiyo inamfanya msomaji aelewe jambo muhimu ambalo linapatikana tena na tena katika kitabu cha Methali, yaani, wanadamu wanaweza kuwa na hekima ya kweli na kufanikiwa ikiwa tu ni wanyenyekevu na wanamruhusu Mungu aongoze hatua zao. (Methali 16:3, 6-8, 18-23) Ukweli huo muhimu unarudiwa tena na tena kwenye Biblia.​—Zaburi 1:1-3; Isaya 26:3; Yeremia 17:7, 8; 1 Yohana 3:22.

 Tazama video hii fupi inayoonyesha muhtasari wa kitabu cha Methali.

a Yehova ni jina la kibinafsi la Mungu. (Zaburi 83:18) Ona makala “Yehova Ni Nani?

b Katika utangulizi, Biblia ya Union Version inasema kwamba inapotumia neno “BWANA” (kwa herufi kubwa) neno hilo linaonyesha jina takatifu la Mungu. Ili kujua utata ambao wasomaji wanapata kwa sababu tafsiri nyingi zimeondoa jina hilo, ona makala iliyo katika sehemu ya Mistari ya Biblia Yafafanuliwa, yenye kichwa “Isaya 42:8​—‘Mimi Ni BWANA.’”