Hamia kwenye habari

Ziwa la Moto Ni Nini? Je, Ni Sawa na Moto wa Mateso au Gehena?

Ziwa la Moto Ni Nini? Je, Ni Sawa na Moto wa Mateso au Gehena?

Jibu la Biblia

 Ziwa la moto ni ziwa la mfano linalomaanisha uharibifu wa milele. Linamaanisha pia Gehena. Lakini, ni tofauti na moto wa mateso kwa kuwa neno linalotumiwa katika Biblia kuhusu moto huo linawakilisha kaburi la ujumla la wanadamu.

Si ziwa halisi

 Mistari mitano ya Biblia inayotaja “ziwa la moto” inalionyesha kuwa ziwa la mfano, si ziwa halisi. (Ufunuo 19:20; 20:10, 14, 15; 21:8) Wafuatao watatupwa ndani ya ziwa la moto:

Mfano wa uharibifu wa milele

 Biblia inasema kwamba ziwa la moto “linamaanisha kifo cha pili.” (Ufunuo 20:14; 21:8) Kifo cha kwanza kinachotajwa katika Biblia kilisababishwa na dhambi ya Adamu. Kifo hicho kinaweza kubadilishwa kupitia ufufuo na mwishowe kitamalizwa na Mungu.​—1 Wakorintho 15:21, 22, 26.

Hakuna mtu anayeweza kutoka katika ziwa la moto la mfano

 Ziwa la moto linawakilisha kifo cha aina tofauti, au cha pili. Ingawa kifo hicho kinawakilisha hali ya kutotenda kabisa, ni tofauti na kifo cha kwanza kwa sababu Biblia haisemi lolote kuhusu ufufuo kutokana na kifo cha pili. Kwa mfano, Biblia inasema kwamba Yesu ana “funguo za mauti na za kuzimu [au, moto wa mateso],” kuonyesha kwamba ana mamlaka ya kuwafungua watu kutokana na kifo kinacholetwa kutokana na dhambi ya Adamu. (Ufunuo 1:​18; 20:13, Union Version) Hata hivyo, Yesu hana funguo za ziwa la moto wala hakuna mtu aliye na funguo hizo. Ziwa hilo la mfano linawakilisha adhabu ya milele inayoletwa kupitia uharibifu wa milele.​—2 Wathesalonike 1:9.

Ina maana sawa na Gehena, Bonde la Hinomu

 Gehena (Kigiriki geʹen·na) inatajwa mara 12 katika Biblia. Kama lile ziwa la moto, Gehena ni neno linalowakilisha uharibifu wa milele. Ingawa watafsiri fulani hutumia neno hilo kumaanisha “moto wa mateso,” Gehena inatofautiana na moto wa mateso (Kiebrania sheʼohlʹ, Kigiriki haiʹdes).

Bonde la Hinomu

 Neno “Gehena” kihalisi linamaanisha “Bonde la Hinomu,” ambalo lilikuwa nje tu ya jiji la Yerusalemu. Katika nyakati za Biblia, wakaaji wa jiji hilo walitupa takataka katika bonde hilo. Walihakikisha kwamba moto uliwaka kila wakati ili kuteketeza takataka; funza walikula kitu chochote ambacho hakikufikiwa na moto.

 Yesu alitumia Gehena kuwakilisha uharibifu au kifo cha milele. (Mathayo 23:33) Alisema kwamba katika Gehena “funza . . . hafi na ule moto hauzimwi.” (Marko 9:​47, 48) Alikuwa akirejelea hali zilivyokuwa katika Bonde la Hinomu na pia kwenye unabii ulio katika Isaya 66:24, unaosema: “Wataenda na kuitazama mizoga ya wale watu waliokuwa wakinikosea; kwa maana funza walio juu yao hawatakufa na moto wao hautazimwa.” Mfano wa Yesu unafafanua, si mateso, bali kuangamizwa kabisa. Funza hao wanakula maiti na vilevile moto unateketeza maiti, si watu walio hai.

 Biblia haionyeshi kwamba kuna mtu anayeweza kutoka katika Gehena. “Ziwa la moto” na “Gehena ya moto” zinawakilisha, uharibifu wa milele.​—Ufunuo 20:14, 15; 21:8; Mathayo 18:9.

‘Wanateswaje mchana na usiku milele na milele’?

 Ikiwa ziwa la moto ni mfano wa uharibifu, kwa nini Biblia inasema kwamba Ibilisi, mnyama-mwitu, na yule nabii wa uwongo “watateswa mchana na usiku milele na milele”? (Ufunuo 20:10) Fikiria sababu nne kwa nini mateso hayo si mateso halisi:

  1.   Ili Ibilisi ateswe milele, angehitaji kuendelea kuishi milele. Hata hivyo, Biblia inasema ataangamizwa, au hataendelea kuwapo.​—Waebrania 2:​14.

  2.   Uzima wa milele ni zawadi kutoka kwa Mungu, si adhabu.​—Waroma 6:​23.

  3.   Mnyama-mwitu na yule nabii wa uwongo ni mifano tu ambayo haiwezi kuteswa kihalisi.

  4.   Muktadha wa Biblia unaonyesha kwamba mateso ya Ibilisi ni kizuizi au uharibifu wa milele.

 Neno linalotumiwa kurejezea “mateso” katika Biblia linaweza kumaanisha pia hali ya kuzuiwa. Kwa mfano, katika tafsiri nyingi, maneno “walinzi wa jela” yanatumiwa kuwakilisha neno la Kigiriki “watesaji” kwenye Mathayo 18:34, kuonyesha uhusiano kati ya maneno “mateso” na “kizuizi.” Vivyo hivyo, masimulizi yanayofanana kwenye Mathayo 8:​29 na Luka 8:​30, 31 yanahusianisha “mateso” na mahali panapoitwa “abiso.” Abiso ni mahali pa mfano ambapo hakuna utendaji au kifo. (Waroma 10:7; Ufunuo 20:​1, 3) Kwa kweli, kitabu cha Ufunuo kinatumia neno “mateso” mara kadhaa kwa njia ya mfano.​—Ufunuo 9:5; 11:10; 18:​7, 10.