Hamia kwenye habari

Je, Wanyama Wanaenda Mbinguni?

Je, Wanyama Wanaenda Mbinguni?

Jibu la Biblia

 Biblia inafundisha kwamba kati ya viumbe wote duniani, ni wanadamu wachache tu watakaoenda mbinguni. (Ufunuo 14:1, 3) Wataenda huko ili watawale wakiwa wafalme na makuhani pamoja na Yesu. (Luka 22:28-30; Ufunuo 5:9, 10) Wanadamu wengi duniani watafufuliwa ili waishi katika paradiso duniani.—Zaburi 37:11, 29.

 Biblia ina sababu nzuri za kutotaja kwamba kuna mbingu kwa ajili ya wanyama vipenzi au mbingu kwa ajili ya mbwa. Wanyama hawawezi kuchukua hatua zinazohitajiwa kustahili kupata “mwito wa mbinguni.” (Waebrania 3:1) Hatua hizo zinatia ndani kupata ujuzi, kuonyesha imani, na kutii amri za Mungu. (Mathayo 19:17; Yohana 3:16; 17:3) Ni wanadamu tu walioumbwa wakiwa na taraja la kuishi milele.—Mwanzo 2:16, 17; 3:22, 23.

 Ili waende mbinguni, viumbe duniani wanahitaji kufufuliwa. (1 Wakorintho 15:42) Biblia ina masimulizi kadhaa yanayohusu ufufuo. (1 Wafalme 17:17-24; 2 Wafalme 4:32-37; 13:20, 21; Luka 7:11-15; 8:41, 42, 49-56; Yohana 11:38-44; Matendo 9:36-42; 20:7-12) Hata hivyo, kila mmoja aliyefufuliwa alikuwa mwanadamu, bali si mnyama.

 Je, wanyama wana nafsi?

 Hapana. Biblia inasema kwamba wanyama na wanadamu ni nafsi. (Hesabu 31:28) Mwanadamu wa kwanza, Adamu, alipoumbwa, hakupewa nafsi bali “akawa nafsi hai.” (Mwanzo 2:7, maelezo ya chini) Nafsi inafanyizwa na vitu viwili: “mavumbi ya ardhi” na “pumzi ya uhai.”

 Je, nafsi zinaweza kufa?

 Ndiyo, Biblia inafundisha kwamba nafsi zinaweza kufa. (Mambo ya Walawi 21:11, maelezo ya chini; Ezekieli 18:20) Wanapokufa, wanyama na wanadamu wanarudi kwenye mavumbi ya ardhi. (Mhubiri 3:19, 20) Kwa maneno mengine, hawapo tena. a

 Je, wanyama wanatenda dhambi?

 Hapana. Kutenda dhambi ni kufikiri, kuhisi, au kufanya kitu ambacho kinavunja viwango vya Mungu. Ili kutenda dhambi, kiumbe anahitaji kufanya uamuzi, lakini wanyama hawana huo uwezo. Kawaida wanatenda kulingana na silika wakati wa maisha yao mafupi. (2 Petro 2:12) Mwishoni mwa maisha yao, wanakufa, hata ikiwa hawatendi dhambi.

 Je, ni sawa kuwatesa wanyama?

 Hapana. Mungu aliwapa wanadamu mamlaka juu ya wanyama lakini hawana haki ya kuwatesa. (Mwanzo 1:28; Zaburi 8:6-8) Mungu anajali masilahi ya kila mnyama kutia ndani ndege wadogo. (Yona 4:11; Mathayo 10:29) Aliwaamuru waabudu wake wawatendee wanyama kwa fadhili.—Kutoka 23:12; Kumbukumbu la Torati 25:4; Methali 12:10.

a Kwa habari zaidi, tazama sura ya 6 ya kitabu Biblia Inatufundisha Nini?