Hamia kwenye habari

Inamaanisha Nini Kuzaliwa Tena?

Inamaanisha Nini Kuzaliwa Tena?

Jibu la Biblia

 Maneno “kuzaliwa tena” yanamaanisha kuanzisha upya uhusiano kati ya Mungu na mtu aliyezaliwa tena. (Yohana 3:3, 7) Mungu huwafanya kuwa watoto wake wale wanaozaliwa tena. (Waroma 8:15, 16; Wagalatia 4:5; 1 Yohana 3:1) Wanakuwa sehemu ya familia ya Mungu, kama tu hali inavyobadilika kwa watoto wanaofanywa kuwa watoto kisheria.​—2 Wakorintho 6:18.

Kwa nini mtu huzaliwa tena?

 Yesu alisema hivi: “Mtu asipozaliwa tena, hawezi kuuona ufalme wa Mungu.” (Yohana 3:3) Kwa hiyo, kuzaliwa tena kunamtayarisha mtu kutawala na Kristo katika Ufalme wa Mungu. Ufalme huo unatawala kutoka mbinguni, kwa hiyo Biblia inasema ‘kuzaliwa upya’ kunamsaidia mtu kupata urithi ambao “umewekwa akiba mbinguni.” (1 Petro 1:3, 4) Wale waliozaliwa tena wanapewa usadikisho wa kwamba ‘watatawala pamoja wakiwa wafalme’ pamoja na Kristo.​—2 Timotheo 2:12; 2 Wakorintho 1:21, 22.

Mtu anazaliwa tena kwa njia gani?

 Yesu alipozungumzia jambo hilo, alisema kwamba wale wanaozaliwa tena wanazaliwa “kwa maji na roho.” (Yohana 3:5) Maneno hayo yanamaanisha kubatizwa kwa maji kisha kubatizwa kwa roho takatifu.​—Matendo 1:5; 2:1-4.

 Yesu alikuwa mtu wa kwanza kuzaliwa tena. Alibatizwa kwenye Mto Yordani, kisha Mungu akamtia-mafuta (au, akambatiza) kwa roho takatifu. Kwa hiyo, Yesu akazaliwa tena kwa roho takatifu akiwa mwana wa Mungu na akiwa na tumaini la kuishi tena mbinguni. (Marko 1:9-11) Mungu alitimiza tumaini hilo kwa kumfufua Yesu akiwa kiumbe wa roho.​—Matendo 13:33.

 Wengine wanaozaliwa tena wanabatizwa pia kwa maji kabla ya kupokea roho takatifu. a (Matendo 2:38, 41) Baada ya kupokea roho hiyo wanakuwa na tumaini hakika la kuishi mbinguni, tumaini ambalo Mungu atatimiza kupitia ufufuo.​—1 Wakorintho 15:42-49.

Maoni yasiyo sahihi kuhusu kuzaliwa tena

 Uwongo: Mtu anapaswa kuzaliwa tena ili aokolewe au ili awe Mkristo.

 Ukweli: Dhabihu ya Kristo inaandaa wokovu si tu kwa wale waliozaliwa tena ili watawale na Kristo mbinguni bali pia kwa ajili ya raia wa kidunia wa Ufalme wa Mungu. (1 Yohana 2:1, 2; Ufunuo 5:9, 10) Kikundi hicho cha pili cha Wakristo kina nafasi ya kuishi milele katika Paradiso duniani.​—Zaburi 37:29; Mathayo 6:9, 10; Ufunuo 21:1-5.

 Uwongo: Mtu anaweza kuamua ikiwa atazaliwa tena.

 Ukweli: Kila mtu anaweza kuamua ikiwa anataka kuwa na uhusiano na Mungu na kupata wokovu. (1 Timotheo 2:3, 4; Yakobo 4:8) Hata hivyo, Mungu huchagua ni nani atakayezaliwa tena, au kutiwa mafuta kwa roho takatifu. Kulingana na Biblia, kuzaliwa tena ‘hakutegemei yule anayetaka, bali hutegemea Mungu.’ (Waroma 9:16) Maneno “kuzaliwa tena” yanaweza pia kutafsiriwa “kuzaliwa kutoka juu,” jambo linalothibitisha kwamba wale wanaozaliwa tena wanachaguliwa “kutoka juu,” au kutoka kwa Mungu.​—Yohana 3:3.

a Kisa cha Kornelio na waliokuwa pamoja naye ndiyo pindi moja tu ambapo jambo hili lilitendeka kwa njia tofauti.​—Matendo 10:44-48.