Hamia kwenye habari

MSAADA KWA AJILI YA FAMILIA | KULEA WATOTO

Unaweza Kuzungumzaje na Watoto Wako Kuhusu Ubaguzi?

Unaweza Kuzungumzaje na Watoto Wako Kuhusu Ubaguzi?

 Tangu mtoto akiwa mdogo, huenda akagundua kwamba baadhi ya watu huwatendea wengine vibaya kwa sababu ya rangi au taifa wanalotoka. Unaweza kumsaidiaje mtoto wako asiathiriwe na maoni ya watu wanaowabagua wengine? Unaweza kufanya nini mtoto wako anapobaguliwa?

Katika makala hii

 Jinsi ya kuzungumza na mtoto kuhusu jamii mbalimbali

 Unaweza kumwambia hivi, Duniani kote kuna watu wenye mwonekano na tamaduni tofauti-tofauti. Kwa sababu hiyo, baadhi ya watu huwatendea wengine isivyofaa kwa kutegemea jinsi wanavyoonekana na jinsi wanavyotenda.

 Hata hivyo, Biblia inafundisha kwamba wanadamu wote wana asili moja. Yaani, tunaweza kusema kwamba sisi sote tuna undugu.

“[Mungu] alifanyiza kila taifa la watu kutoka kwa mtu mmoja.”​—Matendo 17:26.

 “Tuligundua kwamba watoto wetu waliposhirikiana na watu wa jamii tofauti-tofauti, walijionea kwamba kila mtu anastahili kupendwa na kuheshimiwa.”​—Karen.

 Jinsi ya kumfafanulia mtoto kuhusu ubaguzi

 Pindi moja ama nyingine, mtoto wako atasikia ripoti za habari kuhusu uhalifu unaochochewa na chuki au matendo mengine ya ubaguzi. Unaweza kumfafanuliaje mtoto wako kuhusu matukio hayo? Itategemea umri wa mtoto wako.

  •   Watoto wadogo. Dkt. Allison Briscoe-Smith alisema hivi kwenye jarida la Parents: “Ni rahisi kwa watoto wadogo kutofautisha mambo ya haki na yasiyo ya haki. Hilo linaweza kukupa fursa ya kuzungumza na mtoto wako kuhusu ubaguzi.”

“Mungu hana ubaguzi, lakini katika kila taifa mtu anayemwogopa na kutenda uadilifu anakubaliwa naye.”​—Matendo 10:34, 35.

  •   Watoto Wanaokaribia Umri wa Utineja. Watoto walio na umri wa kati ya miaka 6 na 12 ni wadadisi sana, na wanauliza maswali magumu. Jitahidi kuwapa majibu mazuri kadiri uwezavyo. Zungumza na watoto wako kuhusu mambo wanayojionea shuleni na kwenye vyombo vya habari na utumie fursa hiyo kuwaeleza kwamba ubaguzi ni kosa.

“Fikirini kwa upatano, muwe na hisia-mwenzi, upendo wa kindugu, huruma nyororo, na unyenyekevu.”​—1 Petro 3:8.

  •  Matineja. Vijana wana uwezo wa kuelewa masuala mazito. Mtoto wako anapokuwa tineja, huo ni wakati mzuri wa kuzungumzia ripoti za habari kuhusu ubaguzi.

“Watu wakomavu . . . wamezoeza nguvu zao za utambuzi kwa kuzitumia ili kutofautisha mambo yaliyo sawa na mambo yasiyo sawa.”​—Waebrania 5:14.

 “Tunazungumza na watoto wetu kuhusu ubaguzi kwa sababu ni jambo ambalo watakabiliana nalo katika pindi fulani hata iwe wanaishi wapi. Ikiwa hawataelezwa habari hizo wakiwa nyumbani, huenda wakaiga maoni ya watu wenye ubaguzi. Huenda watoto wetu wakapewa habari zisizo za kweli, na wasijue kama wanadanganywa.”​—Tanya.

 Unaweza kuwawekeaje mfano mzuri?

 Watoto hujifunza kwa kuiga, hivyo ukiwa mzazi uwe makini kuhusu jinsi unavyozungumza na kutenda. Kwa mfano:

  •   Je, wewe hufanya mizaha kuhusu watu wa jamii nyingine au kuwadharau? Taasisi ya American Academy of Child and Adolescent Psychiatry inasema hivi: “Watoto wako wanakutazama na kukusikiliza hivyo watakuiga.”

  •   Je, unafurahia kuwa na watu kutoka sehemu nyingine ulimwenguni? Alanna Nzoma ambaye ni daktari wa watoto anasema hivi: “Ikiwa unataka watoto wako wawe na urafiki pamoja na watu wa malezi mbalimbali wanapaswa kukuona ukifanya hivyo pia.”

“Waheshimuni watu wa namna zote.”​—1 Petro 2:17.

 “Kwa miaka mingi familia yetu imewaalika wageni kutoka maeneo mbalimbali ulimwenguni. Tulijifunza kuhusu chakula chao, muziki wao, na hata tulivaa mavazi yao ya kitamaduni. Tulipozungumza na watoto wetu kuhusu watu, hatukukazia walikuwa wa jamii gani. Hatukujigamba kwamba utamaduni wetu ni bora kuliko wa wengine.”​—Katarina.

 Mtoto anapobaguliwa na wengine

 Hata ingawa watu wengi wanazungumza kuhusu usawa, kuna ubaguzi mwingi ulimwenguni. Inamaanisha kwamba huenda mtoto wako akatendewa isivyo haki, hasa ikiwa watu wa jamii yenu si wengi katika eneo hilo. Ikiwa hilo litatokea . . .

 Pata habari kamili. Je, mtu huyo alikusudia kufanya hivyo au alizungumza bila kufikiri tu? (Yakobo 3:2) Je, mkosaji anapaswa kushughulikiwa au jambo hilo linaweza kupuuzwa?

 Ni wazi kwamba, ni muhimu kuwa na usawaziko. Biblia inatoa ushauri huu wenye hekima: “Usikasirike haraka.” (Mhubiri 7:9) Ubaguzi ni tatizo kubwa lakini haimaanishi kwamba kila mara mtu anapokutendea isivyo haki, anafanya hivyo kwa sababu anachukia jamii yako.

 Ukweli ni kwamba hali zinatofautiana, kwa hiyo ni vizuri kuchunguza kilichotokea kabla ya kuchukua hatua yoyote.

“Yeyote anayejibu kabla ya kusikia ukweli wa mambo, huo ni upumbavu na aibu kwake.”​—Methali 18:13.

 Baada ya kupata habari kamili jiuize:

  •   ‘Mtoto wangu ataathiriwaje ikiwa atafikiri kwamba kila mtu ana ubaguzi au kila mara mtu anapomtukana anafanya hivyo kwa sababu ya chuki ya kijamii?’

  •   ‘Je, mtoto wangu atanufaika kwa kufuata ushauri huu wa Biblia: “Usitie moyoni kila neno linalosemwa na watu”?’​—Mhubiri 7:21.

“Usawaziko wenu na ujulikane kwa watu wote.”​—Wafilipi 4:5.

 Vipi ikiwa ubaguzi ulikuwa wa kukusudia? Msaidie mtoto wako kuelewa kwamba hali inaweza kuwa nzuri au mbaya zaidi ikitegemea jinsi atakavyoishughulikia. Wakati fulani mtu anayewadhihaki, kuwaonea, au kuwatukana wengine, anataka tu kuwakasirisha. Katika hali kama hiyo jambo bora zaidi litakuwa ni kumpuuza tu.

“Pasipo na kuni moto huzimika.”​—Methali 26:20.

 Kwa upande mwingine, ikiwa ni salama kwa mtoto wako kufanya hivyo, anaweza kuongea na mtu aliyekosea. Labda mtoto wako anaweza kusema hivi (kwa upole), “Sidhani kama jambo ulilosema au kutenda lilikuwa la fadhili.”

 Vipi ikiwa unataka kuripoti jambo hilo? Ikiwa unahisi uhai wa mtoto wako upo hatarini, ama kwa sababu nyingine yoyote unahisi kwamba hali hiyo haipaswi kupuuzwa, jihisi huru kuzungumza na walimu au hata kutoa ripoti kwa polisi ikihitajika.