Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

 Kichwa

Watu Wataharibisha Dunia Kabisa-Kabisa?

Watu Wataharibisha Dunia Kabisa-Kabisa?

‘Kizazi kinaenda, kizazi kinakuja; lakini dunia inasimama mupaka wakati usio na kipimo.’—MUFALME SULEMANI, ALIYEISHI KATI YA MWAKA WA 1001 NA 1100 MBELE YA KUZALIWA KWA YESU *

Kulingana na muandikaji huyo wa Biblia wa zamani, maisha mafupi ya mutu ni tofauti na dunia inayodumu milele. Kwa kweli, kwa maelfu ya miaka, vizazi vimekuja na vimepita, lakini Dunia imeonekana kuwa yenye nguvu na imara sana katika uwezo wake wa kutegemeza uzima mupaka sasa.

Katika miaka iliyofuata Vita ya Pili ya Ulimwengu, kumekuwa mabadiliko makubwa na ya haraka sana kuliko miaka ya mbele. Katika miaka 70 ao zaidi, watu wamefanya mabadiliko makubwa katika namna ya kusafiri, namna ya kupashana habari, na katika ufundi mwingine wa kiteknolojia, ambao umeleta mabadiliko makubwa katika mambo ya feza. Watu wengi wanaishi aina fulani ya maisha ambayo mbele waliwazia kwamba haiwezekane. Wakati huohuo, hesabu ya watu duniani imeongezeka mara tatu.

Lakini, mambo hayo yote hayakufanyika bila matokeo mabaya. Kazi za watu zinaharibisha dunia sana na hivi karibuni hilo litafanya mizunguko yake ya asili isitumike tena vizuri ili kutegemeza uzima. Kwa kweli, wanasayansi fulani wanasema kwamba tumeingia katika kipindi cha jeolojia kinachoitwa Anthropocene, ambamo watu wanaendelea kubadilisha dunia kwa njia kubwa sana.

Biblia ilitabiri wakati ambapo watu ‘wangeiharibu dunia.’ (Ufunuo 11:18) Watu fulani wanajiuliza ikiwa tunaishi sasa wakati huo. Watu wataharibisha tena dunia kwa kadiri gani? Dunia itafika katika hali isiyoweza kutengenezwa? Kwa kweli, je, watu wataharibisha dunia kabisa-kabisa?

DUNIA ITAFIKA KATIKA HALI ISIYOWEZA KUTENGENEZWA?

Dunia inakaribia kufika katika hali isiyoweza kutengenezwa? Wanasayansi fulani wanawaza kwamba matokeo ya mabadiliko yanaweza kuwa magumu kutabiri. Kwa sababu hiyo, wanaogopa kwamba labda tunakaribia “hali ngumu sana” ya dunia hii ambamo mabadiliko ya gafula na yasiyotazamiwa yanaweza kuleta matokeo hatari kabisa.

Kwa mufano, fikiria Majiwe Makubwa ya Barafu ya Antarktiki ya Mangaribi. Watu fulani wanawaza kwamba ikiwa joto linaendelea kuongezeka duniani, tutafikia hatua ambapo barafu hiyo itayeyuka bila kuweza kurekebishwa. Hiyo ni kwa sababu kwa kawaida sehemu ya juu ya barafu hiyo inapokea mishale ya jua na kuirudisha. Lakini barafu hiyo inapoyeyuka na kukonda, bahari iliyo chini, ambayo hairudishe mishale ya jua, inakuwa katika hatari. Eneo lenye giza la bahari linavuta joto mingi, kwa upande wake joto hilo linafanya barafu iyeyuke sana. Muzunguko huo wenye kuharibisha unaweza kuwa mugumu kukatiza. Kuongezeka kwa maji katika bahari kutokana na barafu inayoyeyushwa kunaweza kutokeza hatari kwa mamia ya mamilioni ya watu.

MAZINGIRA YANAENDELEA KUHARIBIKA SANA

Ufundi mbalimbali umetolewa ili kushugulikia “hali hatari ya sayari” ambayo tunapambana nayo leo. Ufundi mumoja ambao umetumiwa kwa muda murefu umeitwa maendeleo yasiyoharibisha mazingira, ni kusema, kufanya maendeleo katika mambo ya feza na ya watu bila kuharibisha mazingira. Ufundi huo umeleta matokeo gani?

Jambo la kuhuzunisha ni kwamba, kama vile tu kuharibika kwa mambo ya feza ulimwenguni, mazingira ya dunia yanaendelea pia kuharibika sana. Watu wanaendelea kuharibisha mali ya asili ya dunia haraka sana kuliko namna inavyoweza kujirekebisha yenyewe. Kuna jambo linaloweza kufanywa? Mwanaekolojia (mutu aliyesoma uhusiano kati ya viumbe na mazingira) mumoja alisema hivi waziwazi: “Kwa njia fulani, hatuna muongozo juu ya namna ya kushugulikia dunia yetu vizuri.” Hilo linapatana kabisa na maelezo haya ya Biblia: “Mwanadamu anayetembea hana uwezo wa kuongoza hatua yake.”—Yeremia 10:23.

Kwa upande mwengine, Biblia inatuhakikishia kwamba Mungu, Muumbaji, hataruhusu watu waharibishe mazingira ya dunia yetu. Katika andiko la Zaburi 115:16, tunasoma hivi: “Dunia [Mungu] amewapa wana wa binadamu.” Kwa kweli, dunia yetu ni “zawadi njema” kutoka kwa Baba yetu wa mbinguni. (Yakobo 1:17) Tunaweza kutazamia zawadi ya Mungu iwe ya muda tu, kama vile ilikuja na tarehe ya mwisho ya matumizi? Hapana kabisa! Hilo linaonekana wazi kupitia namna dunia iliumbwa.

KUSUDI LA MUUMBAJI JUU YA DUNIA

Kitabu cha Biblia cha Mwanzo kinatoa maelezo mengi juu ya namna Mungu aliumba dunia kwa ufundi. Kwanza, kitabu hicho kinaeleza kwamba dunia ilikuwa “bila umbo, na ukiwa, na giza lilikuwa juu ya uso wa kilindi cha maji.” Hata hivyo, maelezo ya waziwazi yanatolewa kuhusu “maji” yaliyo kwenye dunia yanayotegemeza uzima. (Mwanzo 1:2) Kisha Mungu akasema: “Kuwe na nuru.” (Mwanzo 1:3) Ni wazi kwamba mishale ya jua ilipenya ao kuingia ndani ya angahewa la dunia, na mwangaza ukaonekana duniani kwa mara ya kwanza. Kisha, kitabu hicho kinaeleza kutokea kwa inchi kavu na bahari. (Mwanzo 1:9, 10) Baadaye, “majani, mimea inayozaa mbegu . . . na miti inayozaa matunda” vikatokea. (Mwanzo 1:12) Vitu vilivyohitajiwa kwa ajili ya utendaji mbalimbali na mifumo ya lazima kwa uzima, kama vile usanidimwanga (photosynthèse) vikatokezwa. Mungu alifanya matayarisho hayo makubwa kwa kusudi gani?

Nabii Isaya wa zamani alisema kuwa Mungu ndiye ‘Mufanyizaji wa dunia na Mutengenezaji wake, Yeye aliyeifanya imara, ambaye hakuiumba tu bila sababu, ambaye aliiumba ili ikaliwe na watu.’ (Isaya 45:18) Kwa kweli, kusudi la Mungu ni kwamba dunia iikaliwe na watu milele.

Jambo la kuhuzunisha ni kwamba watu wametumia vibaya zawadi nzuri ya Mungu mupaka kuiharibisha. Lakini, kusudi la Muumbaji halijabadilika. Mwanaume mumoja wa zamani alisema hivi: ‘Mungu si mwanadamu kwamba aseme uongo, Wala si mwana wa binadamu kwamba ajute. Je, yeye mwenyewe amelisema naye hatalitenda, Na je, yeye amesema naye hatalitimiza?’ (Hesabu 23:19) Kwa hiyo, kuliko kuacha dunia iharibiwe, wakati wa Mungu wa “kuwaharibu wale wanaoiharibu dunia” unakaribia sana.—Ufunuo 11:18.

DUNIA NI MAKAO YETU MILELE

Katika Mahubiri yake ya Mulimani yenye kujulikana sana, Yesu Kristo alisema hivi: ‘Wenye furaha ni wale walio na tabia-pole, kwa kuwa watairiti dunia.’ (Mathayo 5:5) Nyuma ya hapo, katika mahubiri hayohayo, Yesu alionyesha njia ambayo itatumiwa ili kulinda dunia isiharibiwe. Aliwaagiza wafuasi wake wasali hivi: “Ufalme  wako na uje. Mapenzi yako na yatendeke duniani kama ilivyo mbinguni.” Kwa kweli, Ufalme wa Mungu, ao serikali yake, utatimiza kusudi la Mungu juu ya dunia.—Mathayo 6:10.

Juu ya mabadiliko makubwa ambayo Ufalme utaleta, Mungu anasema hivi: “Tazama! Ninafanya vitu vyote kuwa vipya.” (Ufunuo 21:5) Hilo linamaanisha kwamba Mungu atabadilisha dunia hii na kuleta dunia ingine mupya? Hapana, kwa sababu dunia yenyewe haina ubaya wowote. Kuliko kufanya hivyo, Mungu ataondoa watu wanaotia dunia katika hali mbaya, “wale wanaoiharibu dunia,” ni kusema, serikali za watu zinazotawala leo. Serikali hizo zitabadilishwa na ‘mbingu mupya na dunia mupya,’ maana yake serikali mupya ya mbinguni, Ufalme wa Mungu, utakaotawala juu ya jamii mupya ya watu duniani.—Ufunuo 21:1.

IIi kuondoa uharibifu wa mazingira uliotokezwa na watu, Mungu atarekebisha mazingira ya dunia ili yaendelee kutegemeza uzima. Mutunga-zaburi alieleza mambo Mungu atafanya. Aliongozwa na roho ya Mungu kuandika hivi: “Umeielekezea dunia fikira zako, ili uipatie wingi; Unaitajirisha sana.” Dunia itakuwa paradiso, itakuwa na hali nzuri ya hewa, na zaidi ya yote, baraka za Mungu, na itatoa chakula kingi.—Zaburi 65:9-13.

Kulingana na Pyarelal, muandishi wa Mohandas Gandhi, marehemu Mohandas Gandhi, kiongozi wa kiroho aliyekuwa Muhindi, alisema hivi: “Dunia inatoa mazao ya kutosha ili kutosheleza mahitaji ya kila mutu lakini si pupa ya kila mutu.” Ufalme wa Mungu utashugulikia sababu kubwa ya matatizo ya dunia kwa kuleta mabadiliko katika mioyo ya watu. Nabii Isaya alitabiri kwamba wakati wa utawala wa Ufalme, watu ‘hawatasababisha mazara [ao mabaya] yoyote wala kusababisha uharibifu wowote’ kati yao ao kuelekea dunia. (Isaya 11:9) Kwa kweli, leo mamilioni ya watu wa hali zote tayari wanajifunza kanuni za juu za Mungu. Wanafundishwa kumupenda Mungu na jirani, kuonyesha roho ya shukrani, kuhangaikia mazingira, kulinda mali za asili za dunia na kuishi kwa njia yenye kupatana na kusudi la Muumbaji kuelekea dunia na watu. Wanatayarishwa ili kuishi katika paradiso duniani.—Mhubiri 12:13; Mathayo 22:37-39; Wakolosai 3:15.

Mungu hataruhusu dunia hii nzuri sana ihabiriwe kabisa-kabisa

Habari ya uumbaji iliyo katika kitabu cha Mwanzo inamalizika kwa maneno haya: “Mungu akaona kila kitu alichokuwa amefanya na, tazama! kilikuwa chema sana.” (Mwanzo 1:31) Kweli, Mungu hataruhusu dunia hii nzuri sana ihabiriwe kabisa-kabisa. Tunatiwa moyo kujua kwamba Yehova Mungu, Muumbaji mwenye upendo, anatayarisha mambo mazuri sana juu ya dunia yetu wakati unaokuja. Anaahidi hivi: “Waadilifu [ao wenye haki] wenyewe wataimiliki dunia, Nao watakaa milele juu yake.” (Zaburi 37:29) Wewe pia unaweza kuwa kati ya “waadilifu,” ambao wataita dunia makao yao milele.

^ fu. 3 Maneno ya kitabu cha Mhubiri 1:4 katika Biblia.