Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Unaweza Kumuona Mungu Asiyeonekana?

Unaweza Kumuona Mungu Asiyeonekana?

“MUNGU ni Roho,” hawezi kuonekana kwa macho ya wanadamu. (Yohana 4:24) Lakini, Biblia inaonyesha kwamba kuna watu walimuona Mungu kwa njia fulani. (Waebrania 11:27) Hilo lingewezekana namna gani? Unaweza kweli kumuona “Mungu asiyeonekana”?—Wakolosai 1:15.

Linganisha hali yetu na hali ya mutu aliye kipofu tangu kuzaliwa. Je, kuwa kwake kipofu kunamuzuia kuelewa mambo yanayomuzunguka? Sivyo kabisa-kabisa. Mutu aliye kipofu anapata habari kupitia njia mbalimbali zinazomuwezesha kutambua watu, vitu, na mambo yanayotendeka karibu naye. Mwanaume mumoja kipofu alisema hivi: “Uwezo wa kuona hauko katika macho. Unapatikana katika akili.”

Vilevile, hata ikiwa hauwezi kumuona Mungu kwa macho halisi, unaweza kumuona kwa “macho ya moyo” wako. (Waefeso 1:18) Chunguza njia tatu za kufanya hivyo.

“ZINAONEKANA WAZIWAZI TANGU KUUMBWA KWA ULIMWENGU”

Mutu aliye kipofu mara nyingi ana uwezo wa hali ya juu wa kusikia na kugusa, anatumia uwezo huo ili kutambua vitu vyenye hawezi kuona. Vilevile, unaweza kutumia uwezo wako mbalimbali (kugusa, kunusa, kusikia, na njia zingine) ili kuchunguza vitu vinavyotuzunguka na kuona Mungu asiyeonekana aliyeviumba. ‘Sifa zake ambazo hazionekane, zinaonekana waziwazi tangu kuumbwa kwa ulimwengu na kuendelea, kwa sababu zinaeleweka kwa vitu vilivyofanywa.’—Waroma 1:20.

Kwa mufano, fikiria dunia, makao yetu. Dunia iliumbwa kwa ajili yetu si ili tu tupate riziki kwa shida lakini ili tufurahie maisha. Tunaposikia upepo mutulivu, tunapojinyoosha ili kuota jua, tunapoonja tunda tamu, ao kusikia nyimbo za ndege zenye kutuliza, tunafurahi sana. Zawadi hizo zinaonyesha kwamba Muumbaji wetu anatuhangaikia, anatupenda, na ni mukarimu, sivyo?

Unaweza kujifunza nini juu ya Mungu kupitia mambo unayoona katika ulimwengu wenye kuonekana? Jambo moja ni hili: Mbingu zinafunua uwezo wa Mungu. Mambo wanasayansi walivumbua hivi karibuni yanaonyesha kwamba ulimwengu unaendelea kupanuka lakini pia kwamba unafanya hivyo kwa mwendo wa haraka sana! Unapoangalia anga usiku, jiulize hivi: Nguvu inayoongoza upanuzi na mwendo wa haraka sana wa ulimwengu inatoka wapi? Biblia inatuambia kwamba Muumbaji ana ‘wingi wa nguvu zenye musukumo.’ (Isaya 40:26) Vitu Mungu aliumba vinatuonyesha kwamba yeye ni “Mweza-Yote,” Yule mwenye ‘kuinuliwa katika nguvu.’—Ayubu 37:23.

YULE “AMBAYE AMEELEZA JUU YAKE”

Mama mumoja aliye na watoto wawili wenye kuwa na tatizo la kuona anasema hivi: “Mazungumuzo ni jambo moja kati ya mambo ya maana yanayowasaidia kujifunza. Uwaambie kila jambo unaloona na kusikia, [na] ujitayarishe kuendelea kutoa maelezo. Wewe ndiye macho yao.” Vilevile, hata ikiwa ‘hakuna mwanadamu ambaye amemuona Mungu wakati wowote,’ Yesu, Mwana wa Mungu, “aliye kifuani pa Baba, ndiye ambaye ameeleza juu yake.” (Yohana 1:18) Kwa sababu Yesu ndiye kiumbe cha kwanza cha Mungu, na mwana wa pekee wa Mungu, alifikia kuwa “macho” yetu ya kutusaidia kuona mbinguni. Kupitia yeye tunapata habari juu ya Mungu asiyeonekana.

Soma mambo machache kati ya yale Yesu, aliyefanya miaka mingi sana pamoja na Baba yake, alieleza juu ya Mungu:

  • Mungu anatumika bila kuchoka. ‘Baba yangu anaendelea kufanya kazi mupaka sasa.’—Yohana 5:17.

  • Mungu anajua mambo tuliyo nayo lazima. ‘Mungu Baba yenu anajua ni vitu gani munavyohitaji hata kabla hamujamuomba.’—Mathayo 6:8.

  •  Mungu anatutimizia kwa upendo mambo tuliyo nayo lazima. ‘Baba yenu aliye mbinguni analichomoza jua lake juu ya watu waovu na wema na ananyesha mvua juu ya watu waadilifu [wenye haki] na wasio waadilifu [wasio haki].’—Mathayo 5:45.

  • Mungu anamuona kila mumoja wetu kuwa mutu wa maana. ‘Je, shomoro wawili hawauzwe kwa sarafu ya samani ndogo? Na bado hakuna hata mumoja wao atakayeanguka chini bila Baba yenu kujua. Lakini nywele zenyewe za kichwa chenu zimehesabiwa zote. Kwa hiyo musiogope: Ninyi ni bora kuliko shomoro wengi.’—Mathayo 10:29-31.

MWANADAMU ALIYEFUNUA TABIA ZA MUNGU ASIYEONEKANA

Mara nyingi watu walio vipofu wanaelewa mambo kwa njia tofauti na zile za watu wanaoona vizuri. Kipofu anaweza kuona kivuli kama nafasi nzuri inayozuiliwa na joto la jua, si kama nafasi yenye giza isiyokuwa na mwangaza wa jua. Kama vile tu mutu aliye kipofu kabisa hawezi kuona kivuli wala mwangaza wa jua, sisi pia hatuwezi kuelewa Yehova kwa uwezo wetu wenyewe. Kwa hiyo, Yehova alitutolea mwanadamu aliyetuonyesha sifa zake kwa ukamilifu.

Mwanadamu huyo ni Yesu. (Wafilipi 2:7) Yesu alitueleza juu ya Baba yake na pia alituonyesha namna Mungu iko. Filipo, mufuasi wa Yesu, alisema hivi: “Bwana, tuonyeshe Baba.” Yesu alimujibu hivi: ‘Yule ambaye ameniona mimi amemuona Baba pia.’ (Yohana 14:8, 9) Unaweza “kuona” nini juu ya Baba kupitia matendo ya Yesu?

Yesu alikuwa muchangamufu, munyenyekevu, na mwenye kukaribiwa kwa vyepesi. (Mathayo 11:28-30) Tabia yake yenye kufurahisha ilifanya watu wamukaribie. Yesu alisikia maumivu ya watu wengine, na alifurahi pamoja nao. (Luka 10:17, 21; Yohana 11:32-35) Unapoendelea kusoma na kusikia masimulizi ya Biblia juu ya Yesu, ujaribu kuwazia mambo yaliyotukia na uyaone katika akili yako kuwa mambo yaliyotendeka kwelikweli. Ikiwa unatafakari (kufikiri sana) juu ya namna Yesu aliwatendea watu, utaona sifa nzuri sana za Mungu waziwazi zaidi na utamukaribia.

KUKUSANYA HABARI ZOTE PAMOJA

Muandikaji mumoja, aliandika hivi juu ya namna kipofu anavyoona ulimwengu: “Anapata habari kwa sehemu-sehemu, kupitia njia mbalimbali (kugusa, kunusa, kusikia, na njia zingine), na anapaswa kukusanya habari hizo pamoja ili ziwe kitu kimoja.” Vilevile, unapotazama vitu Mungu aliumba, unaposoma mambo Yesu alisema juu ya Baba yake, na kuchunguza namna Yesu alionyesha sifa za Mungu, unaweza kuona katika akili yako namna Yehova iko. Utamuona kuwa mutu anayeishi kwelikweli.

Ayubu, aliyeishi nyakati za zamani, alifikia kumuona Yehova hivyo. Kwanza, alisema bila ‘kuelewa.’ (Ayubu 42:3) Lakini kisha kuchunguza kwa uangalifu maajabu ya uumbaji wa Mungu, Ayubu alisema hivi: “Nimesikia habari zako kwa fununu, lakini sasa jicho langu mwenyewe linakuona wewe.”—Ayubu 42:5.

‘Ukimutafuta Yehova, ataacha umupate’

Wewe pia unaweza kufanya hivyo. ‘Ukimutafuta [Yehova], ataacha umupate.’ (1 Mambo ya Nyakati 28:9) Mashahidi wa Yehova watafurahi kukusaidia umutafute na kumupata Mungu asiyeonekana.