Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

 BIBLIA INABADILISHA MAISHA YA WATU

Nilikuwa na Bunduki Yangu Kila Mahali Nilienda

Nilikuwa na Bunduki Yangu Kila Mahali Nilienda
  • ALIZALIWA MWAKA WA: 1958

  • INCHI:ITALIA

  • ALIKUWA:MUSHIRIKI MWENYE JEURI WA KIKUNDI CHA WATU WABAYA

MAISHA YANGU YA ZAMANI

: Nilizaliwa na kukomalia katika sehemu zilizo karibu-karibu na muji wa Roma, eneo la watu maskini waliofanya kazi za kutumikiana. Maisha yalikuwa magumu. Sikujua mama yangu, na sikukuwa na uhusiano muzuri pamoja na baba yangu. Nilikomaa nikijifunza namna ya kuishi katika hali ngumu.

Nilipokuwa na miaka kumi, nilikuwa tayari nimeanza kuiba. Nilipokuwa na miaka 12, nilitoroka nyumbani kwa mara ya kwanza. Mara nyingi, baba yangu alinichukua kwenye makao makuu ya polisi na kunirudisha nyumbani. Nilibishana na watu kila mara kwa sababu nilikuwa mwenye jeuri na nilikasirikia kila mutu. Nilipokuwa na miaka 14, niliondoka nyumbani na sikurudia tena. Nilianza kutumia dawa za kulewesha na kuishi kwenye barabara. Kwa sababu sikukuwa na mahali pa kulala, nilikuwa ninaingia kwa nguvu ndani ya motokari na nilibakia humo mupaka asubuhi sana. Kisha nilitafuta mahali kwenye kuko maji ili ninawe.

Nilifikia kuwa na ufundi kabisa katika kuiba. Nilianza kunyanganya watu sakoshi ndogo, mupaka kuiba katika nyumba kubwa zenye vyumba vingi na nyumba kubwa za matajiri. Nilijulikana kuwa mwenye tabia mbaya na bila kukawia nilialikwa nijiunge na kikundi kimoja cha watu wabaya kilichojulikana sana, na hivyo kupitia kikundi hicho nilipata “nafasi” ya kuanza kuiba kwenye benki nyingi. Kwa sababu nilikuwa mwenye jeuri, mara moja nikakuwa mushiriki mwenye kuheshimiwa wa kikundi hicho. Nilikuwa na bunduki yangu kila mahali nilienda; nililala nayo chini ya kitu changu cha kuegemesha kichwa usiku (oreiller). Tabia kama vile jeuri, kutumia dawa za kulewesha, kuiba, usemi muchafu, na uasherati zikakuwa njia yangu ya maisha. Kila mara mapolisi walinitafuta. Nilikamatwa mara nyingi, na nilipitisha miaka mingi nikifungwa katika gereza na kufunguliwa.

BIBLIA ILIBADILISHA MAISHA YANGU:

Wakati fulani nilipofunguliwa katika gereza, niliamua kumutembelea mama yangu mudogo mumoja. Bila mimi kujua, yeye na watoto wake wawili walikuwa tayari Mashahidi wa Yehova. Walinialika niende  nao kwenye mikutano ya Mashahidi wa Yehova. Kwa sababu nilikuwa na hamu ya kujua mengi, niliamua kuenda nao. Tulipofika kwenye Jumba la Ufalme, nilikazia kwamba nitakaa pembeni ya mulango ili niweze kuona watu wanaotoka inje na wanaoingia ndani. Bila shaka, nilikuwa na bunduki yangu.

Mikutano hiyo ilibadilisha maisha yangu. Ninakumbuka kwamba wakati huo sikujiwazia kuwa kwenye dunia. Watu walionisalimia walikuwa na nyuso zenye kuchangamuka, zenye urafiki, na kicheko. Ninaendelea kukumbuka akilini namna Mashahidi walivyoonekana, macho yao yalionyesha kuwa ni watu waaminifu na wema. Hali hiyo ilikuwa tofauti kabisa na hali ya watu niliozoea kuishi nao!

Nilianza kujifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova. Nilipoendelea kujifunza, niliendelea kuona waziwazi kwamba ninapaswa kubadilisha kabisa namna yangu ya kuishi. Nilifuata shauri linalopatikana katika andiko la Methali 13:20 linalosema hivi: “Anayetembea na watu wenye hekima atakuwa na hekima, lakini anayeshirikiana na wajinga atapatwa na mabaya.” Nilitambua kwamba ilikuwa lazima nijitenge na kikundi hicho. Haikukuwa vyepesi kufanya hivyo, lakini kupitia musaada wa Yehova, niliweza.

Kwa mara ya kwanza katika maisha yangu, nilianza kuzuia matendo yangu

Nilijisafisha pia kimwili. Kwa kujikaza sana, niliacha kuvuta sigareti na kutumia dawa za kulewesha. Nilikata nywele zangu ndefu, niliondoa vitu vyangu vya masikio, na nikaacha kutumia usemi muchafu. Kwa mara ya kwanza katika maisha yangu, nilianza kuzuia matendo yangu.

Sikupenda hata siku moja kusoma na kujifunza, kwa hiyo, lilikuwa jambo ngumu kabisa kwangu kukaza akili na kujitoa kufanya funzo la Biblia. Lakini, nilipoendelea kufanya bidii, pole kwa pole nilifikia kumupenda Yehova, na jambo fulani lilianza kubadilika ndani yangu, zamiri yangu ilianza kunisumbua. Mara kwa mara, nilikuwa na mawazo mabaya juu yangu mwenyewe, nilikuwa na mashaka kwamba Yehova hawezi kunisamehe hata kidogo mabaya yote ambayo nilifanya. Katika nyakati hizo, nilikuwa ninafarijiwa sana kwa kusoma juu ya namna Yehova alimusamehe Mufalme Daudi kisha kufanya zambi nzito.—2 Samweli 11:1–12:13.

Tatizo lingine lilikuwa kuzungumuzia wengine juu ya imani yangu katika mahubiri ya nyumba kwa nyumba. (Mathayo 28:19, 20) Nilikuwa ninaogopa kwamba nitakutana na mutu fulani mwenye niliumiza ao kutendea vibaya kwa njia fulani wakati uliopita! Lakini, niliweza kushinda woga wangu pole kwa pole. Nilianza kutosheka kabisa kwa kusaidia wengine wajifunze juu ya Baba yetu muzuri wa mbinguni, anayesamehe sana.

FAIDA AMBAYO NIMEPATA:

Kujifunza juu ya Yehova kuliokoa maisha yangu! Wengi kati ya marafiki wangu wa zamani wamekufa ao wako katika gereza, lakini mimi nina maisha ya furaha na ninangojea kwa hamu wakati muzuri unaokuja. Nimejifunza kuwa munyenyekevu na mutiifu na kuzuia hasira yangu kali. Hilo linafanya nikuwe na uhusiano muzuri na watu wanaonizunguka. Nimefunga ndoa na mwanamuke mwenye sura nzuri anayeitwa Carmen, na ndoa yetu ni yenye furaha. Mimi na Carmen, tunapata furaha kubwa katika kusaidia wengine wajifunze juu ya Biblia.

Sasa ninafanya kazi ya uaminifu, wakati fulani kazi hiyo ingali inahusu benki, lakini kuliko kuiba kwenye benki, ninazisafisha!