Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Walijitoa kwa Kujipendea Katika Inchi ya Norvège

Walijitoa kwa Kujipendea Katika Inchi ya Norvège

MIAKA michache imepita, Roald na bibi yake Elsebeth, ambao ndoa yao imefanya zaidi ya miaka 40 walikuwa na maisha mazuri katika Bergen, muji mukubwa wa pili wa Norvège. Pamoja na binti wao Isabel na kijana wao Fabien, waliunga mukono kutaniko lao kwa uaminifu katika utendaji mbalimbali. Roald alikuwa muzee wa kutaniko na bibi yake alikuwa painia; Isabel na Fabien walikuwa wanahubiri kwa ukawaida.

Lakini, katika Mwezi wa 9, 2009, familia yao iliamua kufanya jambo fulani tofauti, ni kusema, kuhubiri muda wa juma moja katika eneo la mbali. Kwa hiyo, Roald na Elsebeth pamoja na Fabien, aliyekuwa na miaka 18 wakati huo, walisafiri mupaka Nordkyn, sehemu ya inchi yenye kuzunguukwa na maji iliyokuwa katika muji wa Finnmark juu ya Cercle Arctique. Katika jiji la Kjøllefjord, walihubiri pamoja na ndugu na dada wengine ambao wao pia walikuja katika eneo hilo la mbali ili kuhubiri. Roald anakumbuka: “Mwanzoni mwa juma hilo, nilijisikia kuwa mwenye kutosheka kwa kuwa nilipanga mambo yangu vizuri ili nitegemeze utendaji huo wa pekee kwa juma nzima.” Lakini, baadaye katika juma hilo, mambo yalibadilika. Kulitokea nini?

JAMBO AMBALO HATUKUTAZAMIA

Roald anaeleza hivi: “Bila kutazamia, Mario, painia katika Finnmark, alituuliza ikiwa tuko tayari kuhamia katika muji unaoitwa Lakselv ili kusaidia kutaniko moja huko lenye wahubiri 23.” Roald alishangazwa sana na jambo hilo ambalo hawakutazamia. Anaeleza hivi: “Elsebeth na mimi tulifikiria uwezekano wa kuhubiri mahali ambapo palikuwa na lazima ya wahubiri, lakini tulifikiria kufanya hivyo baadaye, wakati watoto wangekuwa wamekwisha toka nyumbani.” Hata hivyo, Roald alipokuwa akihuribi katika eneo hilo la mbali kwa siku chache, alitambua kwamba watu walikuwa na tamaa ya kujifunza juu ya Yehova. Walihitaji musaada wakati huo si wakati mwengine. Roald anakumbuka: “Ombi la Mario lilinisumbua sana na likanikosesha hata usingizi muda wa siku nyingi.” Kisha Mario akachukua Roald na familia yake katika motokari na kuwapeleka Lakselv, umbali wa kilometre 240 kusini mwa Kjøllefjord. Mario alipenda Roald na familia yake wajionee namna kutaniko la Lakselv ni ndogo na lina lazima ya musaada.

Walipofika Lakselv, Andreas, mumoja wa wazee wawili wa kutaniko hilo, alionyesha wageni hao eneo na Jumba la Ufalme. Kutaniko liliwakaribisha kwa uchangamufu na kuambia Roald na Elisebeth kwamba watafurahi ikiwa familia yao itahamia huko ili kuwasaidia kuhubiri habari njema ya Ufalme. Andreas aliwaambia kwa furaha kwamba wamekwisha kuwatafutia kazi! Roald na familia yake watafanya nini?

TUKUBALI AO TUKATAE?

Mara moja kijana wao Fabien alionyesha mawazo yake, alisema hivi: “Sina nia ya kuhamia hapa.” Wazo la kuacha rafiki zake ambao walikomalia pamoja katika kutaniko la huko kwao na kuishi katika muji mudogo halikumuvutia. Tena, alikuwa hajamaliza mazoezi yake ya kuwa électricien. Lakini wakati binti yao Isabel (aliyekuwa na miaka 23) alipoulizwa kile yeye anawaza, alisema hivi: “Hilo ndilo jambo ambalo nimetaka kufanya sikuzote!” Aliongeza tena hivi: “Lakini, nilipofikiria sana jambo hilo, nilijiuliza, ‘je, ni wazo nzuri kabisa? Nitaacha rafiki zangu? Je, haingekuwa vizuri nibaki tu katika kutaniko langu ambamo mambo yanaendeka vizuri?’ ” Sasa Elsebeth yeye aliwaza nini? Yeye anasema: “Nilifikiri kwamba huo ni mugao ambao Yehova amepatia familia yetu, lakini nilifikiria pia kuhusu nyumba yetu tuliyotengeneza upya na vitu vyote vilivyo ndani ambavyo tulitesekea muda wa miaka 25.”

(Kuume) Elsebeth na Isabel

Mwishoni mwa juma hilo la utendaji wa pekee, Roald na familia yake walirudi Bergen, lakini waliendelea kufikiria ndugu na dada zao wa Lakselv, waliokuwa wanaishi umbali wa kilometre 2 100. Elisebeth anasema hivi: “Nilisali mara nyingi kwa Yehova na niliendelea kuzungumuza na marafiki tuliokutana nao huko kwa kutumiana picha na habari za mahubiri.” Roald anasema hivi: “Ilichukua wakati ili wazo la kuhama liniingie kabisa. Pia, nilipaswa kufikiria ikiwa ingewezekana tuhame na kuwa na uwezekano wa kutosheleza mahitaji yetu. Nilisali sana kwa Yehova na kuzungumuza na familia yangu na ndugu wenye uzoefu sana.” Fabien anakumbuka: “Kadiri ninavyofikiria jambo hilo, ndivyo ninavyotambua kama sikuwa na sababu yoyote ya kukataa. Mara kwa mara nilisali kwa Yehova, na tamaa ya kuhama iliongezeka.” Na kuhusu Isabel? Ili awe tayari, alianza kufanya upainia katika kutaniko lao. Kisha miezi sita ya upainia, wakati huo alifanya sana funzo lake la pekee, basi akajisikia kuwa tayari ili kufanya mabadiliko makubwa, ni kusema kuhamia mahali palipo na lazima ya wahubiri.

KUCHUKUA HATUA

Kwa kuwa tamaa yao ya kuhubiri mahali palipo na lazima ya wahubiri iliongezeka, familia hiyo ilichukua hatua fulani ili kufikia muradi wao. Roald alikuwa na kazi nzuri ya kimwili yenye mushahara munono na aliipenda sana, lakini aliomba mapumuziko ya mwaka muzima. Hata hivyo, mukubwa wake wa kazi alimuomba aendelee kutumika kama mufanyakazi wa muda wakati huo, ni kusema, awe anatumika majuma mawili na kupumuzika majuma sita. Roald anasema hivi: “Mushahara wangu ulipunguka sana, lakini mambo yaliendeka vizuri.”

Elsebeth anaeleza hivi: “Bwana yangu aliniomba nitafute nyumba katika Lakselv na kupangisha nyumba yetu ya Bergen. Ilichukua wakati mwingi na jitihada nyingi, lakini tulifanikiwa. Kisha muda mufupi, watoto wetu wakapata kazi isiyochukua wakati wote.” Elsebeth anaongeza hivi: “Na walitusaidia kulipia garama za chakula na usafirishaji.”

Isabel anasema hivi: “Kwa kuwa muji tulimohamia ni mudogo sana, shida yangu ilikuwa kupata kazi ya kunitegemeza katika kazi yangu ya upainia. Wakati mwengine ilionekana kama hakukuwa na tumaini la kupata kazi.” Hata hivyo, alipata kazi mbalimbali ndogo kenda zisizochukua wakati wote katika mwaka wa kwanza; Isabel aliweza hivyo kulipia garama zake. Namna gani kuhusu Fabien? Yeye anasema: “Kisha kumaliza masomo yangu ya électricien, nilihitaji kutumika ili kuelewa kazi yangu zaidi. Nilifanya hivyo katika Lakselv. Baadaye, nilifanya mashindano na nikapata kazi ya électricien isiyonichukua wakati wote.”

NAMNA WENGINE WALIVYOPANUA UTUMISHI WAO

(Kuume) Marelius na Kesia wanahubiria mwanamuke mumoja Musami katika inchi ya Norvège

Marelius na bibi yake, Kesia, wao pia walipenda kutumikia mahali palipokuwa na lazima zaidi ya wahubiri. Marelius ambaye sasa ana miaka 29 anasema hivi: “Hotuba zinazotolewa kwenye Mikusanyiko na sehemu za kuuliza watu maulizo kuhusu kazi ya upainia zilinichochea nifikiri sana kuhusu kupanua utumishi wangu.” Hata hivyo, bibi yangu Kesia, ambaye ana sasa miaka 26, hakupendezwa na wazo la kuhamia mbali na jamaa yetu. Yeye anasema hivi: “Niliogopa sana wazo la kuwa mbali na watu ninaowapenda.” Zaidi ya hilo, Marelius, alitumika sana ili kulipa feza alizojikopesha ili kununua nyumba yao. Marelius anasema hivi: “Kwa musaada wa Yehova na sala nyingi za kumuomba atusaidie tufanye mabadiliko, tuliweza kuhama.” Kwanza walitumia wakati mwingi kujifunza Biblia. Kisha, wakauzisha nyumba yao, wakaacha kazi zao za kimwili, na katika Mwezi wa 8, 2011, wakahamia katika muji wa Alta, kaskazini mwa Norvège. Wao ni mapainia huko na ili kulipia garama zao, Marelius anafanya kazi ya comptable na Kesia anatumika katika magazini.

Knut na bibi yake Lisbeth, ambao ndoa yao imefanya miaka 30 na kitu, waliguswa na habari zilizo katika Kitabu cha Mwaka kuhusu wale wanaotumika mahali palipo na lazima zaidi ya wahubiri wa Ufalme. Lisbeth anasema hivi: “Habari hizo zilitufanya tufikirie kutumikia katika inchi ya kigeni, lakini nilisita kwa sababu nilifikiri kwamba mutu tu wa kawaida kama mimi haweze kufanya jambo hilo.” Lakini, walifanya hatua fulani ili kufikia muradi wao. Knut anasema hivi: “Tuliuzisha nyumba yetu na, ili kuchunga feza tulizopata, tulihamia katika nyumba mahali mama yangu alikaa. Baadaye, ili kupata hamu ya kutumikia katika inchi ya kigeni, tulihamia katika kutaniko la Kiingereza katika Bergen kwa mwaka mumoja, mahali ambapo tulibaki pamoja na mama yake na Lisbeth.” Haikukawia, Knut na Lisbeth walikuwa tayari kuhama, na walihamia mbali, katika inchi ya Uganda, Afrika. Wanarudi Norvège miezi miwili kwa mwaka ili kufanya kazi ya kimwili. Kufanya hivyo kunawasaidia kuwa na feza inayosaidia kuishi na kuhubiri kwa wakati wote huko Uganda.

‘ONJENI MUONE YA KUWA YEHOVA NI MWEMA’

“Familia yetu imekuwa na uhusiano muzuri sana.”—Roald

Mambo yalikuwa namna gani juu ya wafanyakazi hao wenye kujipendea? Roald anasema hivi: “Tunatumia wakati mwingi sana tukiwa pamoja katika familia katika eneo hili la mbali kuliko vile tulifanya tulipokuwa huko Bergen. Familia yetu imekuwa na uhusiano muzuri sana. Ni baraka kabisa kuona namna watoto wetu wanavyofanya maendeleo. Tena, tuna maoni yanayofaa sasa kuhusu vitu vya kimwili. Hatuvione tena kama tulivyokuwa tunaviona zamani.”

Elsebeth aliona ulazima wa kujifunza luga nyingine. Sababu gani? Eneo la kutaniko la Lakselv linatia ndani jiji la Karasjok, katika eneo la Wasami, ambao ni wenyeji wa majimbo ya kaskazi mwa Norvège, Suède, Finlande, na Russie. Kwa hiyo, ili kuwahubiria wenyeji hao kwa urahisi, Elsebeth alianza kujifunza luga ya Kisami. Sasa anaweza kuzungumuza luga hiyo. Je, anafurahia eneo lake mupya? Akiwa na kicheko mudomoni anasema hivi: “Ninajifunza Biblia na watu sita. Ningependa tena kuwa wapi isipokuwa hapa!”

Fabien, ambaye sasa ni painia na mutumishi wa huduma, anaeleza kwamba yeye na Isabel walisaidia vijana watatu katika kutaniko lao mupya waliokuwa na lazima ya kutiwa moyo ili waongeze utendaji wao katika kutaniko. Vijana wote hao watatu wanahubiri sasa kwa ukawaida. Wawili kati yao wamebatizwa na walifanya upainia musaidizi katika Mwezi wa 3, 2012. Mumoja wao, ambaye wakati fulani alikuwa muzaifu kiroho, alishukuru Fabien na Isabel kwa kuwa walimusaidia awe tena na nguvu katika kweli. Fabien anasema hivi: “Nilifurahi sana aliposema hivyo. Ni furaha kabisa kumusaidia mutu kama huyo!” Isabel anasema hivi: “Katika mugao huu, ‘nilionja kabisa na kuona ya kuwa Yehova ni mwema.’” (Zab. 34:8) Anaongeza hivi: “Zaidi ya yote, kutumikia mahali hapa ni jambo lenye kufurahisha sana!”

Marelius na Kesia, sasa wana maisha ya kawaida lakini wao ni matajiri kiroho. Kutaniko katika Alta, mahali ambapo walihamia, lina sasa wahubiri 41. Marelius anasema hivi: “Tunapokumbuka maisha yetu ya zamani, tunatiwa moyo sana kuona namna maisha yetu yamebadilika sana. Tunamushukuru Yehova kwa kuwa ametuwezesha kuwa mapainia hapa. Hakuna jambo linalotosheleza kama hilo.” Kesia anaongeza hivi: “Nilijifunza kumutegemea tu Yehova, na ametutunza vizuri. Nimetambua pia kwamba kuishi mbali na jamaa yangu kunanisaidia nisamini sana wakati tunaopitisha pamoja. Sijawahi kusikitikia uamuzi tuliochukua.”

(Kushoto) Knut na Lisbeth wanajifunza na familia moja katika inchi ya Uganda

Na maisha ya Knut na Lisbeth yako namna gani huko Uganda? Knut anaeleza hivi: “Ilichukua wakati ili kuzoea hali mupya na desturi za watu. Mara kwa mara tulipata matatizo ya kupata maji, kura, na tulikuwa na matatizo ya estoma, lakini tunajifunza Biblia na watu wengi!” Lisbeth anasema hivi: “Karibu na mahali tunapoishi, kuna maeneo ambamo watu hawajasikia hata kidogo habari njema ya Ufalme. Tunapoenda katika maeneo hayo, tunakuta watu wanaosoma Biblia, na wanatuomba tuwafundishe. Kufundisha watu wanyenyekevu hao Biblia ni furaha isiyoweza kulinganishwa na kitu chochote!”

Kiongozi wetu, Yesu Kristo, ni mwenye furaha sana anapotazama kutoka mbinguni namna kazi aliyoanzisha inavyoendelea na kufika katika maeneo mengi zaidi ya dunia! Ndiyo, watumishi wote wa Mungu ni wenye furaha sana kwa kujitoa ili kuheshimu amri ya Yesu ya ‘kufanya wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote.’​—Mt. 28:19, 20.