Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

MAONI YA BIBLIA

Ndoa

Ndoa

Je, ndoa ni muungano tu wa watu wawili?

‘Kile ambacho Mungu ameunganisha mutu yeyote asikitenganishe.’​—Mathayo 19:6.

MAMBO AMBAYO BIBLIA INASEMA:

Mungu anaona ndoa kuwa si muungano tu wa watu wawili. Ndoa ni muungano mutakatifu kati ya mwanaume na mwanamuke. Biblia inasema hivi: ‘Tangu mwanzo wa kuumba Mungu aliwafanya mwanaume na mwanamuke. Kwa hiyo mwanaume atamuacha baba yake na mama yake, na hao wawili watakuwa mwili mumoja . . . Kwa hiyo kile ambacho Mungu ameunganisha mutu yeyote asikitenganishe.’ *​—Marko 10:6-9; Mwanzo 2:24.

Maneno, “kile ambacho Mungu ameunganisha [ao kuweka pamoja],” hayamaanishe kama Mungu ndiye anamuchagulia kila mutu bibi ao bwana mwenye kumufaa kabisa. Lakini, kwa kusema kwamba Muumbaji wetu ndiye aliyeanzisha mupango wa ndoa, Biblia inakazia uzito wa muungano huo. Bibi na bwana ambao wanaona ndoa kwa njia hiyo wanaichukua kuwa takatifu, kuwa muungano wenye kudumu, na hivyo wanakusudia kabisa kufanya ndoa yao ifanikiwe. Zaidi ya hayo, wanaongeza matumaini yao ya kufanikiwa wakati wanachunguza Biblia ili kupata muongozo wa kuwasaidia watimize madaraka yao ya bibi na bwana.

Mwanaume ana daraka gani?

‘Mume ni kichwa cha muke wake.’​—Waefeso 5:23.

MAMBO AMBAYO BIBLIA INASEMA:

Ili familia iwe nzuri, mutu fulani anapaswa kuchukua maamuzi ya mwisho kuhusu mambo mbalimbali. Biblia inamupatia bwana daraka hilo. Hata hivyo, hilo halimaanishe kwamba bwana anapaswa kuwa dikteta ao mwenye kuwaonea wengine katika familia. Pia, Biblia haimuruhusu bwana aepuke madaraka yake, kwa sababu akifanya hivyo bibi yake hawezi kumuheshimu na anaweza kumuwekea bibi yake muzigo usio wa lazima. Lakini, Mungu anamutazamia bwana afanye kazi kwa bidii ili kushugulikia mahitaji ya bibi yake na kumutendea kwa heshima akiwa rafiki wake wa nguvu sana na ambaye anatumainia. (1 Timotheo 5:8; 1 Petro 3:7) Andiko la Waefeso 5:28 linasema hivi: “Waume wanapaswa kuwa wakiwapenda wake zao kama miili yao wenyewe.”

Bwana ambaye anamupenda kabisa bibi yake anapendezwa na uwezo wake mbalimbali na vipawa vyake na anaheshimu maoni yake, zaidi sana maoni yake kuhusu mambo ambayo yanaelekea familia. Bwana hapaswe kukazia namna yake ya kufanya mambo kwa sababu tu yeye ndiye kichwa cha familia. Wakati Abrahamu, mutu wa Mungu, alikataa shauri nzuri la bibi yake juu ya jambo fulani lililohusu familia yao, Yehova Mungu alimuambia hivi: “Sikiliza sauti yake.” (Mwanzo 21:9-12) Abrahamu alitii kwa unyenyekevu, na familia yake ilipata amani na ikawa na umoja, na pia Mungu akawabariki.

Mwanamuke ana daraka gani?

“Wake, jitiisheni kwa waume zenu wenyewe.”​—1 Petro 3:1.

MAMBO AMBAYO BIBLIA INASEMA:

Mbele ya kumuumba mwanamuke kwa ajili ya mwanaume, Mungu alisema hivi: ‘Si vema huyo mwanaume aendelee kuwa peke yake. Nitamufanyia musaidizi, awe kikamilisho chake.’ (Mwanzo 2:18) Kikamilisho ni kitu ambacho kinakamilisha kitu ao kukifanya kiwe kamili. Kwa hiyo, Mungu hakumuumba mwanamuke sawa na mwanaume, ao kuwa mutu wa kushindana naye, lakini alimuumba ili awe kikamilisho chake. Wakiwa pamoja, wangeweza kutimiza daraka lao walilopewa na Mungu la kuzaa watoto na kujaza dunia na watu walio kama wao.​—Mwanzo 1:28.

Ili kumusaidia mwanamuke atimize daraka lake, Mungu alimupatia sifa nzuri sana za kimwili, kiakili, na za kimoyoni. Anapotumia sifa hizo kwa hekima na upendo, anachangia sana kuleta mafanikio katika ndoa yake na anamusaidia bwana yake kujisikia kuwa mwenye kutulia na mwenye kuwa na usalama wa moyoni. Mungu anamuona mwanamuke muzuri kama huyo kuwa mwenye kustahili kusifiwa. *​—Methali 31:28, 31.

^ Biblia inaruhusu kuvunja ndoa ikiwa tu bibi ao bwana anafanya uzinifu.​—Mathayo 19:9.

^ Bibi na bwana watapata mashauri ya kuwasaidia juu ya ndoa na maisha ya familia katika habari zinazotolewa kwa ukawaida katika gazeti Amuka! chini ya kichwa “Musaada kwa Familia.”