Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Mwanamuke Anapopambana na Matatizo ya Kipindi cha Kuacha Kuona Mwezi

Mwanamuke Anapopambana na Matatizo ya Kipindi cha Kuacha Kuona Mwezi

“Nililemewa na huzuni bila sababu ao bila kutazamia. Nililia na kujiuliza ikiwa nilikuwa ninapatwa na wazimu.”​—Rondro, * aliye na miaka 50.

“Unaamuka asubuhi na unakuta vitu vinavurugika katika nyumba yako. Hauwezi kupata vitu vyako vya pekee. Mambo ambayo ulikuwa unafanya kwa urahisi, sasa yanaonekana kuwa magumu, na haujue ni kwa sababu gani.”​—Hanta, aliye na miaka 55.

WANAWAKE hao hawakuwa wagonjwa. Lakini walikuwa wanapitia kipindi cha kuacha kuona mwezi, ni kusema, mabadiliko ya kawaida katika maisha ya mwanamuke na mwisho wa uwezo wake wa kuzaa. Ikiwa wewe ni mwanamuke, je, unakaribia kipindi hicho cha maisha yako? Je, uko tayari katika kipindi hicho? Hata uwe katika kipindi gani, kadiri wewe na watu ambao unapenda munavyojua kuhusu kipindi hicho, ndivyo mutakuwa na uwezo wa kupambana na matatizo ambayo yanatokana na kipindi hicho.

Kuingia Katika Kipindi cha Kuacha Kuona Mwezi

Kuingia katika kipindi cha kuacha kuona mwezi, ambacho kinaitwa pia kipindi kinachotangulia (ao kinachokaribia) kuacha kuona mwezi, kunatia ndani kipindi kinachotangulia hali ya kuacha kuona mwezi na kipindi chenyewe cha kuacha kuona mwezi. * Hata hivyo, katika usemi wa kawaida, maneno, “kuacha kuona mwezi” mara nyingi yanamaanisha kipindi chote ambacho mwanamuke hawezi tena kuona mwezi.

Wanawake wengi wanaanza kipindi kinachotangulia kuacha kuona mwezi wanapokuwa na miaka kati ya 41 na 50, lakini wengine wanaingia katika kipindi hicho wakiwa na miaka kati ya 51 na 60. Katika hali nyingi, mwanamuke anaacha kuona kipindi cha mwezi pole kwa pole. Kwa sababu homoni hazitengenezwe kwa ukawaida, mwanamuke anaweza kuruka vipindi vyake vya mwezi, anaweza kutokwa damu kwa vipindi visivyo vya kawaida, ao hata kutokwa damu kwa muda murefu zaidi. Wanawake wachache wanaacha kuona kipindi chao cha mwezi kwa gafula ao bila kutazamia.

Kitabu fulani kinasema kwamba “wanawake wanatofautiana kuhusiana na kipindi cha kuacha kuona mwezi.” (Menopause Guidebook) Kitabu hicho kinasema pia hivi: “Kwa kawaida kusikia joto katika mwili ndiyo hali yenye kusumbua inayotokana na kipindi cha kuacha kuona mwezi,” na hali hiyo yenye kusumbua “inaweza kufuatwa na baridi kali.” Alama hizo zinaweza kumukosesha mwanamuke usingizi ao kumuletea uzaifu katika mwili. Hali hiyo yenye kusumbua inadumu muda gani? Kulingana na kitabu ambacho kimetajwa hapo juu, “wanawake fulani wanapatwa na vipindi vya joto ya gafula katika mwili kwa mwaka mumoja ao miaka miwili wanapokaribia kuingia katika kipindi cha kuacha kuona mwezi. Wengine wanasumbuliwa na hali hiyo kwa miaka mingi, lakini wanawake wachache sana wanaeleza kuwa walipatwa na vipindi hivyo vya joto kwa muda wote uliobaki wa maisha yao.” *

Kwa sababu ya kubadilika​-badilika kwa kiwango cha homoni, mwanamuke anaweza pia kuwa na hali ya moyoni yenye kubadilika​-badilika, na hilo linaweza kumufanya awe mwenye kulia-lia, kukosa uwezo wa kukazia uangalifu juu ya jambo fulani na kusahau-sahau. Kitabu hichohicho kinasema, “Inaelekea sana kwamba si kila mwanamuke anasumbuliwa na matatizo hayo yote.” Kwa kweli, wanawake fulani wanapata matatizo machache na hali fulani zenye kusumbua, na wengine hawapate tatizo lolote.

Namna ya Kupambana na Kipindi Hicho

Mabadiliko madogo katika hali ya maisha yanaweza kupunguza hali fulani zenye kusumbua. Kwa mufano, wanawake wenye kuvuta tumbaku wanaweza kupunguza vipindi vya kupatwa na joto katika mwili kwa kuacha kuvuta tumbaku. Wanawake wengi wanafaidika pia kwa kufanya mabadiliko fulani ya chakula, kwa mufano kupunguza ao kuacha kunywa pombe, kuacha kutumia kahawa, na kuacha vikolezo fulani ao vyakula vya sukari, ambavyo vinaweza kuchochea vipindi vya joto katika mwili. Bila shaka, ni jambo la maana kula vizuri, ni kusema, kula kwa kiasi na kula vyakula mbalimbali.

Kufanya mazoezi ya mwili kunaweza pia kusaidia sana ili kupunguza matatizo yanayotokana na kipindi cha kuacha kuona mwezi. Kwa mufano, kunaweza kupunguza hali ya kukosa usingizi na kunaweza pia kuleta mabadiliko ya maana katika namna ya kujisikia moyoni, kunaweza kuleta nguvu katika mifupa na kumusaidia mutu kuwa na afya nzuri. *

Zungumuzia Waziwazi Tatizo Lako

Rondro ambaye alitajwa hapo juu anasema hivi: “Si lazima mutu ateseke kimya​-kimya. Ikiwa unaongea waziwazi na watu ambao unapenda, hawataogopa sana wakati wanaona mambo yanayokupata.” Kwa kweli, wanaweza kukuvumilia zaidi na kukuelewa. Andiko la 1 Wakorintho 13:4 linasema kwamba “upendo huvumilia, hufadhili.”​—Habari Njema kwa Watu Wote.

Wanawake wengi wanafaidika pia kupitia sala, na hata wale wenye kusumbuliwa na tatizo la kuingia katika kipindi cha kuacha kuona mwezi. Biblia inatuhakikishia kwamba ‘Mungu anatufariji sisi katika mateso yetu yote.’ (2 Wakorintho 1:4, La Sainte Bible en swahili de la R.D. Congo) Kujua kwamba kipindi cha kuacha kuona mwezi ni cha muda tu kunatufariji pia. Kwa vyovyote, wanawake ambao wanaendelea kutunza afya yao vizuri wanaweza kufurahia maisha mazuri kwa miaka mingi.

^ Majina yamebadilishwa.

^ Waganga wanasema kwamba kipindi cha kuacha kuona mwezi kinatokea kisha mwanamuke kufanya miezi 12 bila kuona kipindi chake cha mwezi.

^ Matatizo fulani ya afya, kutia ndani ugonjwa wa koo, magonjwa yanayotokezwa na bakteria, na dawa fulani, yanaweza pia kumufanya mwanamuke asikie joto katika mwili. Ni jambo la hekima kuchunguza hali hizo mbele ya kuamua kwamba vipindi vya joto katika mwili vinatokana na kipindi cha kuacha kuona mwezi.

^ Ili kuwasaidia wagonjwa wapambane vizuri na matatizo ya kuingia katika kipindi cha kuacha kuona mwezi, waganga wanaweza kuwaandikia dawa mbalimbali, kama vile dawa za kuongeza homoni, dawa za kuongeza nguvu katika mwili, na dawa za kuzuia hali ya kushuka moyo. Gazeti Amuka! halipendekeze dawa ao matunzo yoyote.