Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Muganga wa Figo Anaeleza Imani Yake

Muganga wa Figo Anaeleza Imani Yake

SEHEMU YA KUULIZA MAULIZO | CÉLINE GRANOLLERAS

Muganga wa Figo Anaeleza Imani Yake

Muganga Céline Granolleras, ni muganga anayeshugulika zaidi sana na magonjwa ya figo huko Ufaransa. Miaka zaidi ya 20 kisha kuwa muganga, alifikia uamuzi wa kwamba kuna Muumbaji anayetuhangaikia. Gazeti Amuka! lilimuuliza juu ya kazi yake na imani yake.

Tuambie kuhusu maisha yako wakati ulikuwa mutoto.

Familia yangu ilihamia huko Ufaransa kutoka Hispania nilipokuwa na miaka kenda. Wazazi wangu walikuwa Wakatoliki, lakini wakati nilikuwa na miaka 16 niliacha kumuamini Mungu. Kwangu, dini halikuwa jambo la maana katika maisha. Ikiwa mutu aliniuliza namna gani uzima ulianza ikiwa hakuna Mungu, nilimujibu, “Kwa sasa, wanasayansi hawezi kufasiria jambo hilo, lakini siku moja wataweza kulifasiria.”

Ni nini kilikufanya ujifunze magonjwa ya figo?

Nilisomea kwenye masomo ya kiganga ya Montpellier, huko Ufaransa. Mwalimu mumoja kwenye masomo hayo ya juu aliongea nami juu ya elimu fulani ya kiganga inayoshugulika na figo. Kazi hiyo ilitia ndani uchunguzi kuhusu namna ya kutunza watu walio na magonjwa ya figo. Hiyo ndiyo kazi ambayo nilitaka kufanya. Katika mwaka wa 1990, nilianza kushiriki katika kufanya uchunguzi juu ya matumizi ya homoni inayoitwa érythropoïétine (EPO) ambayo inachochea mwili wetu kutengeneza chembe nyekundu za damu ndani ya mifupa yetu. Wakati huo, uchunguzi huo ulionekana kuwa jambo jipya.

Ni nini kilichokufanya uanze kufikiri juu ya Mungu?

Katika mwaka wa 1979, bwana yangu, Floréal, alianza kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova. Lakini mimi sikuwa mwenye kupendezwa. Nilipokuwa mutoto, nilichoshwa na mambo ya dini. Hata hivyo, bwana yangu na watoto wangu wakakuwa Mashahidi wa Yehova, na kisha, karibu marafiki wetu wote walikuwa Mashahidi wa Yehova. Mumoja kati yao anayeitwa Patricia alinishauria nianze kusali. Alisema, “Ikiwa hakuna mutu yeyote mbinguni, sala yako haitakuwa na matokeo yoyote. Lakini ikiwa kuna mutu fulani mbinguni, utaona jambo ambalo litatokea.” Miaka fulani kisha hapo, nilianza kujiuliza maisha yana maana gani, na nikakumbuka maneno ya Patricia. Nilianza kusali ili kuelewa maisha yana maana gani.

Ni nini kilikufanya ujiulize maisha yana maana gani?

Shambulizi la wagaidi la majengo ya World Trade Center huko New York lilinifanya nijiulize sababu gani kuna maovu mengi sana kati ya wanadamu. Nilifikiri hivi: ‘Musimamo mukali wa kidini unahatarisha wakati wetu ujao. Lakini hapa ninazungukwa na Mashahidi wa Yehova ambao ni watu wenye amani. Wao hawana musimamo mukali wa kidini. Wanafuata Biblia. Labda ninapaswa kuchunguza mambo ambayo Biblia inasema.’ Kwa hiyo, nilianza kujisomea Biblia mimi mwenyewe.

Ukiwa muganga, je, ilikuwa vigumu kwako kuamini kwamba kuna Muumbaji?

Hapana. Nilivutiwa sana na namna mwili wetu ulivyoumbwa kwa njia ya ajabu sana. Kwa mufano, namna figo zetu zinavyosawazisha kiasi cha chembe nyekundu katika damu yetu ni jambo la kushangaza sana.

Sababu gani unasema hivyo?

Kama unavyojua, chembe nyekundu za damu zinabeba oksijeni ao hewa ya lazima kwa uzima ndani ya mwili. Ikiwa unapoteza damu nyingi ao ikiwa unapanda juu sana, mwili wako utakosa oksijeni. Figo zetu zina uwezo wa kupima kiasi cha oksijeni. Zikitambua kwamba oksijeni inapunguka katika damu, zinachochea mwili utengeneze homoni ya EPO, na kiasi cha cha EPO katika damu kinaweza kuongezeka mupaka mara elfu moja. Homoni ya EPO inachochea urojorojo wa ndani ya mifupa kutengeneza chembe nyekundu nyingi zaidi, ambazo zinabeba oksijeni nyingi ndani ya mwili. Hilo ni ajabu kabisa! Inashangaza kwamba nilijifunza jambo hilo miaka kumi mbele nivutiwe sana kwa kujua kuwa ni Mungu tu ndiye angeweza kuumba mufumo huo muzuri sana.

Ulikuwa na maoni gani juu ya Biblia?

Nilikuwa nimesoma vitabu vingi sana vya historia na hadisi nyingi zenye kujulikana sana, lakini nilitambua mara moja kwamba Biblia ilikuwa tofauti na vitabu vingine. Mashauri ya Biblia ni yenye kufaa, hilo linaonyesha kwamba inapaswa kuwa ilitoka kwa mutu fulani aliye na hekima zaidi kuliko mwanadamu. Tabia za Yesu zilinivutia sana. Niliona kwamba alikuwa mutu aliyeishi kwelikweli. Angeweza kujisikia namna tunavyojisikia, na alikuwa na marafiki. Kwa sababu sikupenda kutumia vichapo vya Mashahidi wa Yehova, nilifanya uchunguzi katika ensaiklopedia mbalimbali na katika vichapo vingine wakati maulizo yalitokea.

Ulifanya uchunguzi juu ya mambo gani?

Nilivutiwa na mambo mengi, kwa mufano namna Biblia ilivyotabiri mbele ya wakati mwaka wa ubatizo wa Yesu. Inaonyesha bila kukosea miaka ambayo ingepita kati ya mwaka wa 20 wa utawala wa Artashasta mutawala wa Uajemi na mwaka ambao Yesu angejitokeza kuwa Masiya. * Nimezoea kufanya uchunguzi, uchunguzi ni sehemu ya kazi yangu. Kwa hiyo, nilifanya uchunguzi katika vitabu vya historia ili kuhakikisha miaka ya utawala wa Artashasta na miaka ya huduma ya Yesu. Mwishowe, niliona kwamba unabii huo wa Biblia ulitimia na kwamba unapaswa kuwa uliongozwa na roho ya Mungu.

[Maelezo ya chini]

^ Soma kitabu Biblia Inafundisha Kabisa Nini? kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova, ukurasa wa 197-199.

[Wazo la fungu kwenye ukurasa 13]

Nilifanya uchunguzi katika vitabu vya historia . . . Mwishowe, niliona kwamba unabii huo wa Biblia ulitimia

[Wazo la fungu kwenye ukurasa 13]

Nilivutiwa sana kwa kujua kuwa ni Mungu tu ndiye angeweza kuumba mufumo huo muzuri sana