Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

“Ninakataa Kukaza Akili Juu ya Ugonjwa Wangu”

“Ninakataa Kukaza Akili Juu ya Ugonjwa Wangu”

“Nilikuwa na lazima ya mutu wa kunisaidia kupanda na kushuka kwenye kitanda. Kutembea kuliniletea maumivu sana. Shingo yangu ilifungana kwa hiyo singeweza kunywa dawa za kupunguza maumivu yangu. Niliota vidonda vyenye vilikataa kupona, na vimoja kati yavyo baadaye vilioza. Nilikuwa na vidonda kwenye estoma na nilikuwa na kiungulia chenye maumivu makali. Sikujua ni nini ilikuwa inanifikia. Nilikuwa tu na miaka kumi.”—Elisa.

Hata ikiwa ana magumu, Elisa anafurahia kufundisha watu juu ya Biblia

SCLERODERMA, neno linalomaanisha “ngozi ngumu” ni ugonjwa unaosumbua watu milioni 2 na nusu hivi duniani pote. Aina inayoonekana mara nyingi kwa watoto ni scleroderma ya sehemu fulani tu ya mwili, ambayo mara nyingi inatia ndani kufanya chembe za ngozi ziwe ngumu.

Lakini, Elisa, alipokuwa na miaka kumi alivumbuliwa na aina ya scleroderma ya mwili wote, ugonjwa huo unaweza kuwa na matokeo mabaya si juu ya ngozi tu lakini pia juu ya namna viungo vya ndani vinafanya kazi, kutia ndani figo, moyo, mapafu, na viungo vinavyochangia kumengenya chakula katika mwili. Wanganga waliwaza kuwa matunzo yatamuongezea Elisa miaka tano tu ya maisha. Sasa, miaka 14 hivi imepita lakini Elisa angali muzima. Hata ikiwa hajapona, anaendelea kuwa na mawazo mazuri juu ya maisha. Gazeti Amuka! lilizungumuza naye juu ya ugonjwa wake na namna anapata nguvu ya kuvumilia.

Ni wakati gani ulijua kwa mara ya kwanza kuwa afya yako haiko muzuri?

Wakati nilikuwa na miaka kenda, niliumia kwenye kiwiko cha mukono wangu, na kidonda hicho kilikuwa kinauma sana. Kidonda hicho kiliendelea kuwa kikubwa, na kilikataa kupona. Uchunguzi wa damu ulionyesha kuwa nilikuwa na scleroderma ya mwili wote. Kwa sababu afya yangu iliendelea kuharibika haraka, tulikuwa na lazima ya kutafuta munganga anayejua kutunza scleroderma.

Mulipata munganga huyo?

Tulipata munganga wa magonjwa ya baridi-yabisi (rhumatisme). Aliambia wazazi wangu kwamba matunzo ya kemikali yangezuia scleroderma yangu ili isikuwe kali sana na kuniongezea miaka tano ya maisha na kama kulikuwa uwezekano wa kupunguza ugonjwa huo. Tatizo ni kwamba matunzo ya kemikali yangeharibisha uwezo wa mwili wangu wa kujikinga wenyewe. Hata baridi ingekuwa mubaya sana.

Inaonekana kuwa jambo mbaya sana halikutokea.

Hapana—jambo la kufurahisha ni kuwa ningali muzima! Hata hivyo, wakati nilikuwa na miaka karibu 12, nilianza kusikia maumivu makali katika kifua; maumivu hayo yangeendelea kwa dakika 30, wakati fulani nilisikia maumivu hayo mara mbili kwa siku. Yalikuwa maumivu makali sana na yalinifanya nilie kwa sauti kubwa.

Ni nini ilikuletea maumivu hayo?

Wanganga walivumbua kuwa kiasi changu cha hemoglobini kilikuwa chini sana na kuwa moyo wangu ulitumika sana ili kusukuma damu katika ubongo. Kisha kutunzwa kwa majuma machache, maumivu hayo yalipunguka. Lakini ninakumbuka kama wakati huo nilifikiri kuwa jambo lolote linaweza kutokea siku yoyote ile. Nilijisikia kuwa muzaifu sana kuliko wakati mwengine wowote, ilikuwa kama vile nilishindwa kupambana na mambo yaliyokuwa yananifikia.

Kumepita sasa miaka 14 tangu ulivumbuliwa na ugonjwa huo. Afya yako iko namna gani leo?

Ninaendelea kuishi na maumivu, na niko na magonjwa mengi yanayoletwa na scleroderma. Magonjwa hayo yanatia ndani vidonda, magonjwa ya mapafu, na kiungulia cha maumivu makali sana. Lakini, ninakataa kukaza akili juu ya ugonjwa wangu ao kupoteza wakati nikiwa na huzuni. Niko na mambo mengine ya kufanya.

Kama vile mambo gani?

Ninapenda kuchora, kushona mavazi, na kutengeneza vitu vya mapambo. Lakini, jambo la maana zaidi, kwa sababu mimi ni Shahidi wa Yehova, ninafanya kazi ya kufundisha watu Biblia. Hata wakati sina uwezo wa kutembelea watu nyumbani kwao, ninasindikiza Mashahidi wengine wanaojifunza Biblia na watu katika eneo letu. Nimepata hata watu ninaojifunza nao Biblia mimi mwenyewe. Kazi ya kuhubiri inafanya maisha yangu yakuwe na kusudi.

Sababu gani unafanya kazi hii hata ikiwa una magumu yako mwenyewe ya kupambana nayo?

Ninajua kuwa habari ninayotangazia watu ni ya lazima na ni yenye faida. Tena, nina furaha nyingi ninapojikaza sana kuwasaidia wengine katika njia hiyo. Na ninajisikia hata kuwa mwenye afya ya muzuri! Katika muda huo mufupi, ninasahau kuwa niko mugonjwa.

Namna gani Biblia inakusaidia kuwa na mawazo ya muzuri?

Inanikumbusha kuwa mateso yangu na mateso ya watu wengine pia ni ya muda tu. Andiko la Ufunuo 21:4 linasema kama kwa wakati wake ambao ameweka, Mungu “atafuta [atapanguza] kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala maombolezo wala kilio wala maumivu hayatakuwapo tena.” Kufikiri juu ya maandiko mengine yenye kufanana na andiko hilo kunanisaidia niamini zaidi ahadi za Mungu juu ya wakati muzuri sana unaokuja wa watu walio na magonjwa yasiyopona na watu wengine wote.