Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

NJIA YA MAISHA YENYE FURAHA

Afya ya Kimwili na Uwezo wa Kuvumilia

Afya ya Kimwili na Uwezo wa Kuvumilia

MAGONJWA YENYE KUKAWIA AO ULEMAVU FULANI VINAWEZA KUWA NA MATOKEO YA MUBAYA SANA JUU YA MAISHA YA MUTU. Kisha kupata ugonjwa wa kupooza, Ulf, mwanaume mumoja mwenye zamani alikuwa na nguvu na afya ya muzuri alisema hivi: “Nilivunjika moyo sana. Nilipoteza nguvu na ujasiri wangu . . . Nilijisikia kuwa nimefika ‘mwisho.’”

Mambo yenye yalimupata Ulf yanatukumbusha kuwa hakuna mutu mwenye kuwa na mamlaka juu ya afya yake. Hata hivyo, tunaweza kuchukua hatua fulani zenye kufaa ili kupunguza hatari ya kuwa na afya ya mubaya. Lakini, tutafanya nini ikiwa afya yetu inakuwa ya mubaya? Je, hilo linaonyesha kama hatutakuwaka tena na furaha? Kama vile tutaona, jibu ni hapana. Lakini, tufikirie kwanza kanuni fulani zenye zinasaidia kuwa na afya ya muzuri.

UKUWE “MWENYE KIASI KATIKA MAZOEA.” (1 Timotheo 3:2, 11) Ni wazi kwamba kuzoea kula ao kunywa pombe kupita kiasi ni mubaya kwa afya yetu​—na kunapoteza feza nyingi! ‘Usikuwe kati ya watu wanaokunywa divai mno [ao, nyingi sana], kati ya watu wanaokula nyama kwa ulafi, kwa maana mulevi na mulafi watakuwa maskini.’​—Methali 23:20, 21.

USICHAFUE MWILI WAKO. “Acheni tujisafishe wenyewe kila unajisi [ao, uchafu] wa mwili na roho.” (2 Wakorintho 7:1) Watu wanachafua miili yao wakati wanatafuna tumbako ao kuivuta ao wakati wanatumia mubaya pombe ao dawa za kulewesha. Kwa mufano, Vituo vya Kugombanisha Magonjwa katika États-Unis vinasema kwamba kuvuta tumbako, “kunaleta magonjwa na ulemavu na kunaharibisha karibu kila kiungo cha mwili.”

UONE MWILI NA UZIMA WAKO KUWA ZAWADI ZA MAANA SANA. “Kupitia kwake [Mungu] tuna uhai na tunaenda na kuwako.” (Matendo 17:28) Kuelewa maneno hayo kunatuchochea kuepuka hatari zenye hazina maana ikuwe tuko kwenye kazi, tunatembeza motokari, ao wakati tunachagua mambo ya kujifurahisha. Ni jambo la maana kuwa na afya ya muzuri kuliko kuwa na ulemavu kwa sababu ya kujifurahisha kwa wakati kidogo!

ZUIA TABIA ZA MUBAYA. Kuko uhusiano wa karibu kati ya mawazo na mwili wetu. Kwa hiyo, ujikaze kuepuka mahangaiko yenye hayana maana, kuzuia kasirani kali, wivu, na tabia zingine zenye hatari. Zaburi 37:8 inasema ‘Acha hasira na uache gazabu.’ Tena tunasoma hivi: “Musihangaike kamwe [ao, hata kidogo] juu ya kesho, kwa maana kesho itakuwa na mahangaiko yake yenyewe.”​—Mathayo 6:34.

UJIKAZE KUKAZA AKILI JUU YA MAMBO YA MUZURI. Andiko la Methali 14:30 linasema hivi: ‘Moyo mutulivu ni uzima wa mwili wenye nyama.’ Biblia inasema tena hivi: “Moyo wenye shangwe [ao, furaha] ni dawa nzuri.” (Methali 17:22) Maneno hayo yanapatana na mambo yenye sayansi inasema. Munganga mumoja katika Écosse alisema, “Ikiwa uko mwenye furaha, hautagonjwa-gonjwa sana kama wale wenye kukosa furaha.”

KOMALISHA UVUMILIVU. Kama vile Ulf mwenye tulizungumuzia, pengine kile tunaweza tu kufanya ni kuvumilia magumu yenye kuendelea. Hata hivyo, tunaweza kuchagua namna tutavumilia. Watu fulani wanavunjika moyo sana, na hilo linafanya mambo yakuwe mubaya zaidi. Andiko la Methali 24:10 linasema, ‘Ikiwa unajionyesha kuwa umevunjika moyo siku ya taabu, nguvu zako zitakuwa chache [ao, kidogo].’

Pengine kisha tu kujisikia kuwa wenye kuvunjika moyo, watu wengine wanaweza tena kuwa na furaha. Wanajipatanisha na hali. Wanapata njia za kupambana na hali hiyo. Ulf alijikuta katika hali hiyo. Anasema kuwa kisha kusali sana na kufikiri juu ya ujumbe wa Biblia wenye kutia moyo “alianza kuona njia za kupambana na magumu yake kuliko vizuizi.” Zaidi ya hilo, kama tu watu wengi wenye wanapatwa na majaribu makubwa, alijifunza mambo ya maana kuhusu huruma na kujitia pa nafasi ya wengine, mambo yenye yalimuchochea kutolea watu wengine ujumbe wa Biblia wenye kutia moyo.

Mutu mwengine mwenye aliteseka sana ni mwanaume mumoja mwenye kuitwa Steve. Wakati alikuwa na miaka 15, alipatwa na aksidenti yenye ilimufanya apooze kuanzia shingo mupaka miguu. Wakati alifikia miaka 18, mikono yake ilianza tena kutumika. Kisha alienda kwenye masomo ya juu, na huko alianza bila kukawia kutumia dawa za kulewesha, pombe, na kufanya uasherati. Hakukuwa na tumaini. Lakini wakati alianza kujifunza Biblia, hilo lilimufanya aone maisha kwa njia tofauti na lilimusaidia kuacha tabia zake za mubaya. Alisema, “Sikujisikia tena kama mwenye kukosa kitu fulani. Sasa maisha yangu yanajaa amani, furaha, na kutosheka.”

Mambo yenye Steve na Ulf walisema yanatukumbusha maneno ya Zaburi 19:7, 8: ‘Sheria ya Yehova ni kamilifu, inairudisha nafsi. . . . Maagizo kutoka kwa Yehova ni manyoofu [ao, yenye haki], yanafanya moyo ushangilie [ao, ufurahi sana]; amri ya Yehova ni safi, inafanya macho yangae.’